2014-03-01 09:02:50

Ziara ya Kardinali Tauran nchini Benin inalenga kukoleza majadiliano ya kidini


Majadiliano ya kidini kati ya waamini wa dini mbali mbali nchini Benin; Mafundisho Yakinifu kuhusu Majadiliano ya kidini kati ya Wakristo na Waislam pamoja na waamini wa dini za jadi ni kati ya mambo msingi yakayojadiliwa na Kardinali Jean Lous Tauran wakati wa safari yake ya kikazi nchini Benin, kuanzia tarehe 2 Machi hadi tarehe 5 Machi 2014. Majiundo haya makini yanaratibiwa na Padre Didier Affolabi kutoka Benin..

Kardinali Tauran anatarajiwa pia kukutana na kuzungumza na Baraza la Maaskofu Katoliki Benin, ili kuwashirikisha uzoefu na mang'amuzi yake kuhusu mikakati ya majadiliano ya kidini. Kardinali pia atakutana na kuzungumza na viongozi wa dini mbali mbali nchini Benin pamoja na kuangalia sifa za mwamini wa dini ya asili ambaye anaheshimiwa kuwa ni "mtakatifu".

Jumatano ya Majivu, siku ya kufunga na kufanya toba, Kardinali Tauran atatembelea Kanisa kuu la Benin, lango la watu waliokuwa wamekata tamaa kwa kusafirishwa kwenda utumwani. Hili ni eneo linalokumbusha madhara ya biashara ya utumwa kwa utu na heshima ya binadamu. Hapa historia inaonesha kwamba, kuna mamillioni ya watu waliosafirishwa kwenda utumwani.

Akiwa nchini Benin, Kardinali Tauran atapata nafasi ya kuadhimisha Ibada ya Misa Takatifu kwenye Seminari kuu ya Mtakatifu Gallo na baadaye atakwenda kusali kwenye kaburi la Kardinali Bernadin Gantin, kutoka Benin, Kardinali na Mwafrika wa kwanza kupewa dhamana ya kuongoza Baraza la Kipapa la haki na amani, kunako mwaka 1976 na baadaye alikuwa ni Dekano wa Makardinali.

Itakumbukwa kwamba, hata Baba Mtakatifu mstaafu Benedikto XVI alipotembelea Benin ili kuzindua Waraka wa Dhamana ya Afrika, Africae Munus alitembelea na kusali kwenye kaburi la Kardinali Bernadin Gantin, ambaye walifanya naye utume kwa miaka mingi mjini Vatican.







All the contents on this site are copyrighted ©.