Uchunguzi unafanywa kuhusu uhakika wa miili ya Mapadre waliotekwa nyara DRC!
Hadi sasa hakuna habari za uhakika kuhusu mahali walipo Mapadre watatu wa Shirika
la Assumption waliotekwa nyara kunako Mwezi Oktoba, 2012 nchini DRC. Habari zisizothibitishwa
bado zinabainisha kwamba, kuna kaburi la pamoja ambalo limegunduliwa likiwa na masalia
ya mwili wa Padre Jean Pierre Ndulani ambaye kwa miaka kadhaa alikuwa anatekeleza
utume wake nchini Scotland na mwaka 2012 akarejea nchini kwao na hapo akakumbana
na mkasa wa kutekwa nyara na watu wasiojulikana hadi leo hii.
Akizungumza na
Shirika la Habari za Kimissionari, FIDES, Askofu Melchisedech Sikuli Paluku wa Jimbo
Katoliki Butembo-Ben, mahali ambako Wamissionari watatu waliotekwa nyara walikuwa
wanafanya shughuli zao za kichungaji anasema, kuna haja kwa watu kuvuta subira kwani
kuna makuburi mawili yaliyopatikana yakiwa na miili kadhaa, lakini haijafahamika ikiwa
kama kuna miili pia ya Mapadre waliotekwa nyara. Viongozi wa Kanisa wanaendelea kufanya
uchunguzi wa kina ili kubainisha ukweli wa mambo.
Wamissionari waliotekwa nyara
ni Padre Jean Pierre Ndulani, Padre Anselme Wasikundi pamoja na Padre Edmond Bamutute,
walitekwa nyara hapo tarehe 21 Oktoba 2012 walipokuwa katika Parokia ya Notre Dame
des Pauvres, Kilometa 70 kutoka Makao makuu ya Jimbo Katoliki la Butembo Beni, lililoko
nchini DRC.