Shukrani walimu wote mnaofundisha kwenye shule za Kanisa Katoliki
Katika kazi ya kuelimisha, familia zinamjenga mtu katika ukamilifu wa utu wake kulingana
na hali zake zote, ukiwepo upande wa kijamii. Familia zinaunda Jumuiya ya upendo na
mshikamano, ili kuwezesha kufundisha na kurithisha tunu msingi za kitamaduni, kimaadili,
kijamii, kiroho na kidini, tunu ambazo ni muhimu sana kwa maendeleo na ustawi wa wanafamilia
wake na kwa jamii husika. Familia ndiyo shule ya kwanza ya fadhila za kijamii.
Kanisa
Katoliki limekuwa ni mdau mkubwa katika sekta ya elimu sehemu mbali mbali za dunia
kwani hii ni sehemu ya utume wake wa Uinjilishaji unaopania kumkomboa mtu mzima: kiroho
na kimwili. Kanisa linaendelea kuwekeza katika sekta ya elimu, ambayo leo hii inakabiliana
na changamoto kubwa kutoka katika Jamii.
Baba Mtakatifu Francisko katika ujumbe
wake kwa watumiaji wa mitandao ya kijamii anawashukuru wale wote wanaofundisha katika
shule zinazomilikiwa na kuendeshwa na Kanisa Katoliki sehemu mbali mbali za dunia.
Uelimishaji ni kitendo cha upendo ni sawa na kumpatia mtu zawadi ya maisha.