2014-02-28 09:32:27

Sifa za Askofu!


Dhamana na utume wa Baraza la Kipapa kwa ajili ya Maaskofu, mwelekeo mpana wa utume wa Baraza mintarafu mpango wa Mungu, Kanisa la Kitume ni chemchemi ya Sakramenti ya daraja takatifu; Askofu anapaswa kuwa ni shahidi wa Kristo Mfufuka; Ukuu wa Mungu katika uchaguzi wa Maaskofu wapya; Maaskofu wanapaswa kuwa ni wachamungu, watu wa sala na wachungaji wema. Haya ni mambo makuu ambayo Baba Mtakatifu Francisko amekazia kwa wajumbe wa Baraza la Kipapa kwa ajili ya Maaskofu, wakati alipokutana nao, Alhamisi tarehe 27 Februari 2014 mjini Vatican.

Baba Mtakatifu anasema, Kanisa linahitaji viongozi wakweli na waadilifu; watu wanaoweza kujitosa kimasomaso kwa ajili ya watu wa Mungu waliokabidhiwa kwao. Kanisa halihitaji mameneja, bali Askofu ambaye ni shahidi wa ufufuko wa Kristo; mtu mnyenyekevu na jasiri; Kanisa halihitaji wapambanaji, bali viongozi wanyenyekevu watakaopandikiza mbegu ya haki, ukweli na amani.

Baba Mtakatifu amewakumbusha wajumbe wa Baraza la Kipapa kwa ajili ya Maaskofu dhamana na utume wao kwa ajili ya Makanisa mahalia kwa ajili ya kufanya uteuzi wa Maaskofu wapya; wawe kweli ni watu walioteuliwa na Kristo kwa njia ya Roho Mtakatifu kwa ajili ya Kanisa lake. Watu ambao watazingatia mahitaji ya Makanisa mahalia kwa kusoma alama za nyakati. Askofu awe ni mtu mwenye uwezo wa kuunganisha nguvu na rasilimali iliyopo kwa ajili ya ustawi na maendeleo ya Jimbo husika. Ustawi na maendeleo ya Kanisa yanategemea kwa kiasi kikubwa uteuzi wa Maaskofu mahalia.

Baba Mtakatifu anasema hakuna Askofu ambaye anaweza kukidhi viwango vinavyohitajika kwa kila Kanisa mahalia, kwani kila Jimbo lina mazingira na changamoto zake zinazopaswa kufanyiwa kazi kwa ukamilifu. Hapa kuna haja kwa Baraza la Kipapa lililopewa dhamana hiii kuvuka hali ya upendeleo, mvuto na mguso wa mtu, mahali anapotoka mtu au mielekeo mbali mbali ya kijamii ili kukidhi matakwa ya Mungu kwa ajili ya watu wake. Kanisa linahitaji Maaskofu wenye mwono na mwelekeo mpana zaidi wa Mungu, na wala si watu wanaotishwa na malimwengu.

Baba Mtakatifu anawataka wale wanaofanya kazi katika Baraza la Kipapa kwa ajili ya Maaskofu kutekeleza wajibu wao kwa kuzingatia: weledi, huduma na utakatifu wa maisha. Wanaweza kupata dira na mwanga wa kufanya uchaguzi wa Maaskofu wapya kwa kufanya rejea kwenye msingi wa Kanisa la Kitume, kwani ustawi na maendeleo ya Kanisa daima uko kwenye msingi wake wa kitume kwa kujenga na kudumisha umoja na mshikamano miongoni mwa Watu wa Mungu. Huu ndio mwendelezo wa Mapokeo ya Kitume unaooneshwa miongoni mwa Maaskofu. Watu wamekwishaonja katika hija ya maisha yao madhara ya utengano, sasa wanataka kuona Kanisa ambalo limeshikamana katika umoja na udugu.

Baba Mtakatifu anasema, Askofu anapaswa kuwa ni shahidi wa Kristo Mfufuka. Shahidi ambaye anashikamana na Kanisa na maisha yake ya kitume na shughuli za kichungaji hayana budi kuwa ni kielelezo amini cha Kristo Mfufuka. Awe na ujasiri wa kuyamimina maisha yake kwa ajili ya Kristo na Kanisa lake, kwani hivi ni sehemu ya vinasaba vya Askofu wa Jimbo.

Askofu awe ni mtu mwenye uwezo wa kuyasadaka maisha yake, kwani Uaskofu si mali yake binafsi bali ni kwa ajili ya Kanisa na Kondoo aliokabidhiwa na Mama Kanisa; ni kwa ajili ya jirani zake na hasa zaidi wale wanaosukumizwa pembezoni mwa Jamii.

Baba Mtakatifu anasema, katika mchakato wa kumtafuta Askofu haitoshi kuangalia sifa zake za kibinadamu: akili, uwezo wake wa darasani au katika shughuli za kichungaji; haya ni mambo msingi lakini zaidi, Askofu mtarajiwa hana budi kuwa ni mtu mkomavu wa kimaadili na utu wema; aliyefundwa akafundika katika misingi ya maisha ya Kikristo; mwaminifu, mkweli, muwazi na mwenye uwezo wa kuongoza kwa kuonesha dira na mwelekeo wa maisha kwa Familia ya Mungu atakayokabidhiwa.

Sifa hizi hazina budi kujionesha kwa namna ya pekee katika ushuhuda wa Kristo Mfufuka, anayepaswa kupewa kipaumbele cha kwanza. Atambue wajibu na dhamana yake mbele ya Mwenyezi Mungu na umuhimu wa kudumisha umoja na mshikamano miongoni mwa Maaskofu wengine. Mtu mwenye uwezo wa kufanya maamuzi na wengine na wala si kubaki peke peke kama kisiwa! Baba Mtakatifu anakiri kwamba, si kila Askofu mtarajiwa anaweza kuwa na sifa zote hizi kwa mkupuo! Jambo la msingi ni kuwa makini katika kufanya uteuzi wa Maaskofu wapya.

Ukuu na utukufu wa Mungu unapaswa kupewa kipaumbele cha kwanza na kwamba, uteuzi hauwezi kuchukuliwa kutokana na mtu kujisikia au uchunguzi uliofanywa. Ili kuweza kuwa na uhakika wa maamuzi magumu yaliyopaswa kuchukuliwa, anasema Baba Mtakatifu kuna haja ya mhusika kuweka wazi dhamiri yake mbele ya Mwenyezi Mungu kwa kuzingatia umoja na mshikamano miongoni mwa Maaskofu.

Maaskofu hawana budi kwanza kabisa kuwa ni watangazaji wa Habari Njema ya Wokovu kwani imani lazima itangazwe. Kanisa linahitaji viongozi watakaolinda na kuendeleza Mafundisho tanzu ya Kanisa yanayojikita katika upendo na uhuru kamili unaopata chimbuko lake kutoka katika Injili. Kanisa haliwahitaji viongozi wanaojitafuta wenyewe au wanaopigana kulinda masilahi yao binafsi; bali Kanisa linawataka watu wanyenyekevu na wasiopenda makuu; watu wenye imani na wa kweli katika maisha yao, watu wanaotambua dhamana walioyokabidhiwa na Mwenyezi Mungu kwa ajili ya Kanisa.

Baba Mtakatifu anasema Askofu anapaswa kuwa ni mtu mvumilivu anayetambua kwamba, kamwe magugu hayataweza kumea na kukua kiasi hata cha kuharibu ngano bora iliyoko shambani. Askofu daima anapaswa kuwa ni mtu mwenye imani na matumaini; mtu asiye ogopa kujisadaka kwani anatambua kwamba, hii ni kazi ya Mungu ambayo imeanimishwa kwake. Kamwe Askofu hapaswi kujikatia tamaa, bali mtu anayejiweka mbele ya Mungu daima kwa njia ya sala, kiasi hata za kujadiliana na Mungu bila kuchoka, kwa hakika anasema Baba Mtakatifu Kristo atamwonesha dira na njia ya kufuata.

Baba Mtakatifu akizungumza na wajumbe wa Baraza la Kipapa kwa ajili ya Maaskofu anasema, Kanisa linahitaji Askofu mkweli na mwaminifu; mhudumu wa Neno na kwamba urithi mkubwa anaoweza kuliachia Kanisa mahalia si: dhahabu wala almasi, bali utakatifu wa maisha. Maaskofu katika maisha yao, waoneshe ushuhuda wa utakatifu wa Mungu uliojificha ndani mwao. Daima wawe ni watu wanaojisadaka kwa ajili ya Familia ya Mungu bila ya kujitumbukiza katika mazoea yanayoweza kuwaharibia kazi na kuwafanya kukimbia majukumu yao ya kichungaji kwa kuelemewa na mazoea.

Baba Mtakatifu anasema, utume na dhamana ya Askofu unahitaji udumifu unaojidhihirisha katika maisha ya kila siku. Waamini wapate nafasi katika moyo na maisha ya Askofu wao, kielelezo cha Kristo na Kanisa lake. Kwa njia hii, Askofu ataweza kuzima kiu ya maisha ya kiroho kwa watu wake. Hivi ndivyo Baba Mtakatifu alivyofanya rejea kwenye Mtaguso mkuu wa Trento, ambao amewataka wajumbe wa Baraza la Kipapa kwa ajili ya Maaskofu kuufanyia kazi kwa ajili ya ustawi na maendeleo ya Kanisa la Kristo. Baba Mtakatifu anahitimisha hotuba yake ambayo imetoa dira na mwongozo kwa ajili ya kufanya uteuzi wa Maaskofu wapya kwa ajili ya Makanisa mahalia. Ana uhakika kwamba, Yesu Kristo ataendelea kufanya hija na Kanisa lake!

Hotuba hii imehaririwa na
Padre Richard A. Mjigwa, C.PP.S.
Idhaa ya Kiswahili ya Radio Vatican.







All the contents on this site are copyrighted ©.