Mtambo wa kuhakiki na kusimamia mawasiliano ya simu wazinduliwa Tanzania
Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Jakaya Mrisho Kikwete, Alhamisi, Februari
27, 2014, amezindua Mtambo wa Kuhakiki na Kusimamia Mawasiliano ya Simu (Telecommunications
Traffic Monitoring System –TTMS) katika sherehe fupi lakini ya kufana iliyofanyika
Makao Makuu ya Mamlaka ya Mawasiliano Tanzania (TCRA) mjini Dar Es Salaam.
Mtambo
huo unalenga kuhakiki na kusimamia mawasiliano ya simu zinazoingia nchini kutoka nje
ya nchi kwa kubaini jinsi matumizi ya simu yanavyofanyika, kubaini bei zinazotozwa
na faida inayopatikana pamoja na kuihakikishia Serikali mapato yake stahiki.
TCRA
imeupata mtambo huo wenye gharama ya dola za Marekani milioni 25 bila kuununua moja
kwa moja. Mtambo huo umenunuliwa na kufungwa na Kampuni ya SGS ya Uswisi ikishirikiana
na Kampuni ya JVG ya hapa nchini. Kampuni hiyo itausimamia na kuuendesha mtambo huo
kwa miaka mitano chini ya utaratibu wa “Jenga, Endesha na Hamisha – Build, Operate
and Transfer”kipindi ambako itaweza kurudisha gharama zake kabla ya kuukabidhi kwa
TCRA.
Mkurugenzi Mkuu wa TCRA, Profesa John Nkoma amemwambia Rais Kikwete katika
sherehe hizo kuwa ufungaji wa mtambo huo hautaongeza bei ya mawasiliano kwa watumiaji
wa simu. Badala yake, amesema Profesa Nkoma, Serikali itanufaika kwa kupata kiasi
cha dola za Marekani milioni moja kwa mwezi ikiwa ni gawio lake kutokana na faida
itakayotokana na mtambo huo mpya.
Tayari TCRA imekwishakabidhi kwa Serikali
dola milioni moja za mwezi uliopita na katika sherehe ya leo, Profesa Nkoma ameikabidhi
Hazina mfano wa hundi yenye thamani ya sh 1,684, 357. 283 (sawa na dola milioni moja)
kwa mwezi wa Februari. Amesema kuwa fedha yake tayari imewekwa kwenye Akaunti ya Mfuko
wa Hazina.
Akizungumza kwenye sherehe hiyo, Rais Kikwete ameeleza mafanikio
yaliyopatikana katika sekta ya mawasiliano katika miaka tisa iliyopita na jinsi gharama
za mawasiliano zilivyopungua katika kipindi hicho kutokana na hatua mbali mbali zilizochukuliwa
na serikali na hasa ujenzi wa Mkongo wa Mawasiliano wa Taifa. Amesema kuwa matumizi
ya simu yameongezeka kutoka laini za simu milioni 3.6 mwaka 2005 hadi kufikia laini
milioni 28 mwishoni mwa mwezi uliopita wakati watumiaji wa Internet wameongezeka kutoka
milioni 4.9 mwaka 2011 hadi kufikia milioni tisa wa sasa.
Kuhusu gharama za
simu, Rais amesema kuwa gharama hizo zimepungua kwa asilimia 57 kati ya mwaka 2009
na 2013 kwa upande wa simu wakati punguzo hilo kwa upande wa internet ni asilimia
75.