2014-02-27 15:09:59

Ujenzi wa tasaufi ya umoja isaidie mchakato wa hija ya majadiliano ya kidini na kiekumene


Mshikamano wa upendo miongoni mwa wafuasi wa Kristo ndiyo kauli mbiu iliyoongoza mkutano wa Maaskofu rafiki wa Chama cha Kitume cha Wafokolari kutoka sehemu mbali mbali za dunia waliokuwa wamekutanika mjini Gastel Gandolfo. Ni tukio ambalo pamoja na mambo mengine linalenga kujenga na kuimarisha umoja na udugu, kwa kushirikishana tunu msingi za maisha ya kiroho na kichungaji mintarafu karama ya umoja wa Kanisa. Maaskofu wanapaswa kutekeleza dhamana hii kwa ajili ya ustawi na maendeleo ya Kanisa zima.

Watu wana kiu na hamu ya kutaka kuona na kusikia ushuhuda wa maisha ya watu ambao wamejitoa bila ya kujibakiza kwa ajili ya Kristo na Kanisa lake; ndugu wanaopendana na kuheshimiana licha ya tofauti zao za tabia, mahali wanapotoka na umri wao. Mwelekeo huu unaibua changamoto ya umoja na mshikamano wa Kanisa zima, kwani upendo wa Kristo una nguvu ya kuweza kuleta maboresho ya nguvu katika mahusiano ya watu; watu wanasikia mwaliko wa kumtambua Kristo kati yao, tayari kujiondoa kutoka katika ubinafsi wao, ili kukutana na wengine, tayari kuwashirikisha matumaini waliyopokea kutoka kwa Kristo kama zawadi kubwa!

Ni maneno ya Baba Mtakatifu Francisko wakati alipokutana na Kundi la Maaskofu rafiki wa Chama cha Kitume cha Wafokolari, siku ya Alhamisi, tarehe 27 Februari 2014. Kanisa linapaswa kuwa ni nyumba na shule ya umoja, changamoto kubwa katika mapambazuko ya Millenia ya tatu ya Ukristo, kwa kuendelea kuwa waaminifu kwa Kristo na kujibu kwa umakini mkubwa kilio cha watu na mategemeo yao; jambo la msingi ni kujenga na kudumisha kwanza tasaufi ya umoja na mshikamano.

Hiki kiwe ni kikolezo makini cha elimu na majiundo ya maisha ya Kikristo; mahali ambapo wahudumu wa Mafumbo ya Mungu, watawa na watekelezaji wa mikakati ya shughuli za kichungaji wanafundwa bila kusahau sehemu zote zinazojikita katika majiundo makini ya maisha ya kifamilia na Jumuiya ya Kikristo.

Baba Mtakatifu Francisko anabainisha kwamba, ujenzi wa Kanisa kama nyumba na shule ya umoja ni kielelezo makini cha mikakati ya Uinjilishaji Mpya, ili wote waweze kuwa wamoja chini ya Kristo. Hii ndiyo nguvu ya Roho Mtakatifu inayookoa na kuleta mvuto. Ujenzi wa tasaufi ya umoja inasaidia katika mchakato wa uimarishaji wa hija ya majadiliano ya kidini na kiekumene.

Baba Mtakatifu amewashukuru Maaskofu rafiki wa Chama cha Kitume cha Wafokolari kwa kumtembelea mjini Vatican, kama sehemu ya mchakato wa kujenga na kuimarisha mshikamano na umoja miongoni mwa Maaskofu pamoja kukuza upendo na ujasiri wa matumaini mapya. Baba Mtakatifu Francisko amewaambia Maaskofu hao kwamba, anatumainia sala zao katika maisha na utume wake kama Khalifa wa Mtakatifu Petro.







All the contents on this site are copyrighted ©.