Sinodi za Maaskofu ni jukwaa makini la kukutana ili kusikiliza kilio cha waamini katika
maisha na utume wao!
Kardinali Lorenzo Baldisseri, Katibu mkuu wa Sinodi za Maaskofu anasema, Sekretarieti
ya Sinodi ya Maaskofu imekwishapokea sehemu kubwa ya majibu ya maswali dodoso yaliyotumwa
kwenye Mabaraza ya Maaskofu Katoliki, sehemu mbali mbali za dunia. Majibu haya yanaonesha
kilio kikuu cha baadhi ya waamini wanaojisikia kwamba, wametengwa na Mama Kanisa kutokana
na kujikuta wanaishi maisha ambayo ni kinyume cha Mafundisho, Sheria, Kanuni na Nidhamu
ya Sakramenti za Kanisa.
Maadhimisho ya Sinodi Maalum ya Maaskofu kwa ajili
ya Familia iliyoitishwa na Baba Mtakatifu Francisko ni cheche za mwelekeo mpya wa
Maadhimisho ya Sinodi unaoonesha mshikamano na umoja miongoni mwa Maaskofu katika
kukabiliana na changamoto za kichungaji zinazoendelea kuibuliwa katika maisha na utume
wa Kanisa katika ulimwengu mamboleo na maendeleo ya sayansi na teknolojia.
Majibu
yaliyotolewa na Mabaraza ya Maaskofu Katoliki, Vikundi na watu binafsi ni changamoto
kubwa kwa Mama Kanisa kuwaendelea watu mahali waliko ili kuwasikiliza na kuwatekelezea
yale yanayokera katika hija ya maisha yao ya kiroho na kiutu. Umefika wakati kwa viongozi
wa Kanisa kuwaendelea watu wao huko waliko badala ya kutunga sera na mikakati ya kichungaji
wakiwa wamejifungia ofisini kwao. Waguswe na kuonja hali halisi ya maisha na changamoto
za watu mitaani, vigangoni, parokiani na majimboni.
Kardinali Lorenzo Baldisseri
anasema kwamba, sehemu kubwa ya majibu ya maswali dodoso yaliyotumwa kutoka kwenye
Mabaraza ya Maaskofu Katoliki yametolewa muhtasari, lakini bado Maaskofu wameonesha
utajiri mkubwa wa majibu na mchango wa waamini na wote walioguswa na maisha na utume
wa Kanisa katika masuala ya ndoa na familia kwenye tovuti za Mabaraza ya Maaskofu
Katoliki. Hii inaonesha kwamba, watu wengi wameguswa na changamoto za maisha na utume
wa Kanisa kwa ajili ya familia, kiasi cha kushiriki kikamilifu katika mchakato wa
kujibu maswali dodoso yaliyotumwa na Sekretarieti ya Sinodi ya Maaskofu.
Mchakato
wa hija ya Maadhimisho ya Sinodi ya Maaskofu umefungua ukurasa mpya wa majadiliano
ya kina kati ya Kanisa na Waamini, kiasi cha kuanza kuona imani na matumaini kwa wale
waliokuwa wameanza kuchoka na kujikatia tamaa ya maisha ya kiroho. Wengi wanasema
wanaendelea kuchangamotishwa na Baba Mtakatifu Francisko katika maisha na utume wake
kama Khalifa wa Mtakatifu Petro. Ni kiongozi anayeguswa na mahangaiko ya watu sehemu
mbali mbali za dunia.
Kardinali Lorenzo Baldisseri anasema, kwa sasa Sekretarieti
imeanza kuandaa Hati ya Kufanyia Kazi, Instrumentum Laboris itakayotumiwa na Mababa
wa Sinodi wakati wa Maadhimisho ya Sinodi Maalum ya Maaskofu.
Baba Mtakatifu
Francisko anaendelea kuhimiza umuhimu wa Sinodi za Maaskofu katika maisha na utume
wa Kanisa, kama kielelezo makini cha umoja na mshikamano miongoni mwa Maaskofu katika
utekelezaji wa mikakati ya kichungaji ndani ya Kanisa. Ikumbukwe kwamba, Sinodi ya
Maaskofu kuhusu Familia itaadhimishwa katika awamu mbili: Awamu ya kwanza inajadili
matatizo na changamoto zinazojitokeza katika maisha na utume wa Kanisa kuhusiana na
familia.
Awamu ya Pili itakayoadhimishwa mwaka 2015 itakuwa na dhamana ya
kutoa mapendekezo kwa Khalifa wa Mtakatifu, ili aweze kutoa mwelekeo wa jumla kwa
ajli ya maisha na utume wa Kanisa katika utume wa Ndoa na Familia. Makardinali wamejadili
kwa kina na mapana kuhusu changamoto za maisha na utume wa Familia katika mwanga wa
Uinjilishaji Mpya. Baba Mtakatifu Francisko amewaandikia wanandoa na familia barua
ya wazi, akiwataka kusali kwa ajili ya mchakato mzima wa Maadhimisho ya Sinodi ya
Maaskofu kuhusu Familia wakitambua kwamba, wao ndio wahusika wakuu.
Hii ni
changamoto kwa Maaskofu kujenga na kuimarisha mshikamano miongoni mwao na Mapadre
ambao ni wasaidizi wao wa karibu katika kufundisha, kutakatifuza na kuwaongoza watu
wa Mungu bila kuwasahau watawa na waamini walei. Changamoto za kichungaji zinazolikabili
Kanisa katika ujumla wake zinapaswa kushughulikiwa katika mtazamo wa utume na dhamana
ya Kanisa katika Uinjilishaji Mpya.