2014-02-27 09:36:29

Jitokezeni kushiriki katika mchakato wa uchaguzi mkuu nchini Namibia


Baraza la Maaskofu Katoliki Namibia linawaalika waamini na watu wote wenye mapenzi mema nchini humo kujitokeza kwa wingi ili kushiriki kwenye mchakato wa uchaguzi mkuu unaotarajiwa kufanyika nchini humo mwaka 2014. Wananchi wengi wamekwishaanza kujiandikisha kama sehemu ya mchakato wa maandalizi ya zoezi zima la kupiga kura mwezi Novemba. RealAudioMP3

Maaskofu wanasema, ushiriki wa wananchi katika mchakato wa upigaji kura ni muhimu katika kuimarisha zoezi zima la demokrasia pamoja na utekelezaji wa haki na demokrasia shirikishi, ili hata sauti ya wananchi iweze kusikika kwa njia ya kupiga kura. Hii ni haki ambayo wananchi wa Namibia hawana sababu yoyote ya kuipuuzia. Waamini na wananchi katika ujumla wao wanahimizwa kupiga kura kwa kuongozwa na dhamiri nyofu.

Baraza la Maaskofu Katoliki Namibia linaitaka Serikali na Tume ya uchaguzi nchini Namibia kuhakikisha kwamba, wanazingatia: ukweli na uwazi, kanuni na maadili ya uchaguzi mkuu. Tume iendelee kuwahamasisha wananchi kushiriki katika zoezi zima la uchaguzi nchini Namibia pamoja na kutoa elimu ya uraia. Kuna haja ya kuboresha pia daftari la wapiga kura na kwamba, siku ya uchaguzi watu washiriki kikamilifu katika zoezi hili kwa uhuru, amani na utulivu.

Vyama na wagombea wote wahakikishe kwamba, wanazingatia sheria, kanuni na maadili ya uchaguzi mkuu, ili uchaguzi uweze kuwa huru na wa haki. Wagombea wapewe nafasi sawa katika vyombo vya habari ili waweze kufafanua sera na malengo ya vyama vyao ikiwa kama wananchi watawapatia ridhaa ya kuongoza nchi ya Namibia.

Kwa wale watakaoshindwa kwa uhalali wakubali matokeo. Baada ya uchaguzi vyama vya siasa vihakikishe kwamba, amani, umoja na mshikamano wa kitaifa vinaendelezwa na kamwe wananchi wasigawanywe kwa misingi ya kisiasa, kikabila wala udini. Ujumbe wa Baraza la Maaskofu Katoliki Namibia umetiwa sahihi na Askofu mkuu Liborius Ndumbukuti Nashemba, Rais wa Baraza la Maaskofu Katoliki Namibia.








All the contents on this site are copyrighted ©.