2014-02-26 08:46:46

Wanandoa tokeni kifua mbele kuinjilisha na kuyatakatifuza malimwengu!


Huduma kubwa inayotekelezwa na Mama Kanisa kwa wanandoa wakristo ni kuwaita na kuwasindikiza katika hija ya maisha na utume wao wa ndoa na familia, ili kutambua na hatimaye kushirikishana ile furaha inayobubujika kutoka katika Sakramenti ya Ndoa. Hii ni zawadi kubwa kwa wanandoa Wakristo kutoka kwa Kristo aliyeteswa, akafa na kufufuka kutoka katika wafu. RealAudioMP3
Katika ulimwengu wa utandawazi, maendeleo ya sayansi na teknolojia, ni jukumu la wanandoa wenyewe kusimama kidete na kutoka kifua mbele kwa ajili ya kuinjilisha na kuyatakatifuza malimwengu kwa njia ya ushuhuda wa maisha adili yanayosimikwa katika imani, matumaini na mapendo kwa Kristo na Kanisa lake.
Ni wajibu wa Familia za Kikristo kuwa ni sehemu ya Habari Njema kwa watu wa mataifa waliokata tamaa na kutopea katika ukanimungu, ili watu wengine waweze kuonja ile furaha ya kufunga ndoa ya Kikristo, kama zawadi kubwa katika maisha ya mwamini, tayari kushiriki katika kazi ya uumbaji ambayo Mwenyezi Mungu amemkabidhi mwanadamu!
Hivi ndivyo anavyoandika Askofu mkuu Francesco Pio Tamburrino wa Jimbo kuu la Foggia-Bovino, Italia katika barua yake ya kichungaji, kama sehemu ya Maadhimisho ya Jubilee ya miaka mia mbili tangu Jimbo hili lilipowekwa chini ya ulinzi na usimamizi Familia Takatifu ya Yesu, Maria na Yosefu. Familia ni mada ambayo kwa sasa ni kati ya changamoto za kichungaji kwa Mama Kanisa wakati huu wa Mapambazuko ya Millenia ya tatu ya Ukristo.
Wanandoa wanakumbushwa ile siku ya furaha na vigelegele walipokuwa wamevalia mavazi meupe, wakimeta meta mbele ya waamini na kupeana ahadi ya uaminifu na udumifu katika Sakramenti ya Ndoa, hadi pale kifo kitakapowatengenisha. Lakini, jambo la kusikitisha ni kuona kwamba, familia nyingi za Kikristo kwa sasa zinakabiliana na majanga ya utengnano.
Nchini Italia anasema Askofu mkuu Francesco Pio Tamburrino, ndoa nyingi zinaweza kudumu kwa takribani miaka kumi na tano, baada ya hapo, wanandoa wanachokana na kuanza kusakamana kwa vitimbwi na hatimaye, ndoa yenyewe kuvunjika. Licha ya majanga yote haya familia bado ni nguzo msingi ya maisha ya kijamii, ingawa kwa sasa kuna mitazamo hasi hata kuhusiana na ndoa na familia.
Hizi ni changamoto za kichungaji zinazofanyiwa kazi sasa na Mama Kanisa, kwani kuna uhusiano mkubwa kati ya dhamana ya Uinjilishaji Mpya na Familia, ndiyo maana, Baba Mtakatifu Francisko ameitisha Sinodi Maalum ya Maaskofu kwa ajili ya Familia, itakayoadhimishwa Mwezi Oktoba, 2014 mjini Vatican. Wanafamilia wanakumbushwa kwamba, wamepewa dhamana na wajibu ambao wameuhifadhi katika sahani ya udongo.
Familia ni tabernakulo ya Injili ya Uhai, changamoto kwa wanandoa na familia kujitajirisha kwa tafakari ya kina ya Neno la Mungu na Maisha ya Kisakramenti. Hiki ni chombo ambacho kinatumika mara kwa mar ana hivyo kinahitaji uvumilivu unaojikita katika fadhila ya unyenyekevu, kwani Mwenyezi Mungu amependa kuwateuwa watu wa kawaida ili kuendeleza kazi ya uumbaji na ukombozi wa mwanadamu.
Familia ni chombo ambacho kiko wazi mbele ya Mungu ili kutekeleza kazi zake na kwamba, thamani na utakatifu wa maisha ya ndoa na familia vinapata chimbuko lake kutoka kwa Mwenyezi Mungu. Yeye ndiye muasisi wa maisha ya ndoa na familia na hivyo kuwekwa katika historia ya ukombozi. Familia ni hazina inayohifadhi Fumbo la Upendo wa Mungu kwa mwanadamu.
Ni hazina inayotishiwa na utamaduni wa kifo na ukanimungu. Lakini, waamini wakumbuke kwamba, hazina hii bado inaendelea kulindwa na Mwenyezi Mungu anayehitaji ushirikiano wa wanandoa na familia pamoja na Kanisa.







All the contents on this site are copyrighted ©.