2014-02-26 11:13:38

Msiwapotoshe watu kwa kuandika habari za uvumi usiokuwa na msingi!


Baba Mtakatifu mstaafu Benedikto XVI amewataka waamini na watu wenye mapenzi mema kuwapuuza wale wanaoonesha mashaka kuhusu uamuzi wake wa kung'atuka kutoka katika kiti cha Khalifa wa Mtakatifu Petro. Huu ni uamuzi ambao ameufanya kwa hiyari yake mwenyewe na kwa ajili ya ustawi na maendeleo ya Kanisa la Kristo.

Haya ni majibu ambayo yameandikwa kwenye Gazeti "La Stampa" linalochapishwa kila siku nchini Italia baada ya vyombo kadhaa vya habari ndani na nje ya Italia kuonesha mwelekeo potofu kuhusu uamuzi wa Baba Mtakatifu Benedikto XVI kung'atuka kutoka madarakani, takribani mwaka mmoja uliopita, yaani hapo tarehe 11 Februari 2013.

Baba Mtakatifu mstaafu ameyaandika majibu haya kwa mkono wake mwenyewe, kwa ufupi, lakini kwa usahihi mkubwa. Anasema huu ni uamuzi ambao ameufanya kwa uhuru na utashi kamili na wala hakuna shinikizo kutoka sehemu yoyote ile kama ambavyo baadhi ya vyombo vya habari vinataka kuwaaminisha watu.

Anasema, anaendelea kuvaa mavazi meupe na kutumia jina la Benedikto wa kumi na sita kwa sababu za kichungaji na wala hakuna mwingiliano wowote na utume wa Khalifa wa Mtakatifu Petro unaoendelezwa na Papa Francisko. Hapa vyombo vya habari anasema Baba Mtakatifu Mstaafu Benedikto XVI vinataka kupotosha waamini.







All the contents on this site are copyrighted ©.