2014-02-26 14:07:03

Msiogope kupokea Sakramenti ya Mpako wa Wagonjwa ili kukabiliana kwa imani na matumaini Fumbo la mateso na kifo!


Kwa mpako Mtakatifu wa Wagonjwa na Sala za Makuhani, Kanisa lote huwakabidhi wagonjwa na wazee kwa Bwana aliyeteswa ba kutukuzwa ili awainue na kuwaokoa. Na kwa hakika, Kanisa linawahimiza wajiunge kwa hiari na mateso na kifo cha Kristo ili kutoa mchango wao kwa mafao ya Taifa la Mungu.

Mama Kanisa anapenda kutafakari mang'amuzi ya ugonjwa na mateso mintarafu huruma ya Mungu inayojionesha kwa Yesu ambaye ni kielelezo cha Msamaria Mwema. Mama Kanisa kwa kuiga mfano wa Msamaria mwema katika kufundisha na kuponya kwa njia ya Mpako Mtakatifu wa Wagonjwa."Mtu wa kwenu amekuwa hawezi? Na awaite wazee wa Kanisa, nao wamwombee, na kumpaka mafuta kwa jina la Bwana". Hivi ndivyo Mama Kanisa ameendelea kutekeleza utume wake kwa wagonjwa kwa njia ya sala ya Makuhani na Mpako Mtakatifu.

Sakramenti ya Mpako Mtakatifu wa Wagonjwa, ndiyo mwendelezo wa Katekesi iliyotolewa na Baba Mtakatifu Francisko, Jumatano tarehe 26 Februari 2014 kwenye Uwanja wa Kanisa kuu la Mtakatifu Petro mjini Vatican. Anasema, kwa njia ya Maadhimisho ya Sakramenti ya Mpako Mtakatifu wa Wagonjwa, Kanisa linawasindikiza waamini wake ili kukabiliana na Fumbo la Mateso na Kifo.

Baba Mtakatifu anawaalika waamini na watu wenye mapenzi mema kutambua na kuthamini Sakramenti ya Mpako Mtakatifu wa Wagonjwa hasa katika tamaduni ambazo zinashindwa kuzungumzia kweli hizi ambazo zinagusa maisha ya binadamu.

Waamini watambue na kuthamini Sakramenti hii kama kielelezo cha mshikamano wa maisha ya kiroho na Kanisa zima, kwa kutambua uwepo endelevu wa Yesu anayewaimarisha wafuasi wake katika imani na matumaini, akiwakumbusha kwamba, hakuna kitu kinachoweza kuwatenga na nguvu yake inayookoa, si dhambi wala kifo.

Baba Mtakatifu ametambua uwepo wa wajumbe wa mkutano mkuu wa SIGNIS unaoendelea mjini Roma. Hiki ni kikundi cha Wanahabari Wakatoliki 300 kutoka katika nchi 80, kinachotafakari kuhusu "Vyombo vya Habari katika Utamaduni wa amani: kutengeneza taswira na vijana wa kizazi kipya".

Baba Mtakatifu amewasalimia wanafunzi na marafiki wa Chuo Kikuu cha Kipapa cha Canada kinachoadhimisha kumbu kumbu ya Miaka 125 tangu kilipoanzishwa. Anaendelea kuwahimiza waamini kuhakikisha kwamba, wanapokuwa na mgonjwa au mzee ambaye yuko katika hatari ya kufa, wasisite kumwita Padre ili aweze kumpatia Mpako Mtakatifu wa Wagonjwa. Kwa njia hii, Yesu Kristo Mkombozi na Bwana wa maisha, atakuwa karibu na wagonjwa hawa.

Yesu yupo katika kila Sakramenti ya Kanisa na kwa njia hii anawashirikisha waamini maisha na huruma yake. Waamini wajitahidi kumfahamu ili hatimaye, waweze kumhudumia kwa njia ya wagonjwa. Tarehe 27 Februari, Kanisa linafanya kumbu kumbu ya Mtakatifu Gabrieli mteseka, changamoto kwa vijana kuwa ari na mwamko wa kutaka kuwa kweli ni wafuasi wa Kristo.

Baba Mtakatifu anawaalika wagonjwa kutolea shida na mahangaiko yao huku wakijishikamanisha na Kristo. Wanandoa wapya wajitahidi kuhakikisha kwamba, Injili inakuwa ni dira na mwongozo wa maisha yao.







All the contents on this site are copyrighted ©.