2014-02-26 11:59:38

Maboresho ya uchumi wa Kanisa ni kwa ajili ya mafao na ustawi wa maendeleo ya maskini na wote wanaosukumizwa pembezoni mwa Jamii


Kardinali George Pell, Mwenyekiti wa Sekretarieti ya Kipapa ya Uchumi na Fedha anasema, ikiwa kama Vatican itafanikiwa kuboresha hali yake ya uchumi na fedha, huu utakuwa ni msaada mkubwa katika maisha na utume wa Kanisa kwa ajili ya maskini na wote wanaosukumizwa pembezoni mwa Jamii.

Kardinali Pell kwa miaka kumi na miwili amekuwa ni Askofu mkuu wa Jimbo kuu la Sydney, Australia kwa sasa anajiandaa kufunga vilago, tayari kumsaidia Baba Mtakatifu Francisko katika mchakato wa maboresho ya maisha na utume wa Kanisa mjini Vatican hasa katika masuala ya fedha na uchumi.

Kardinali Pell anasema kwamba, Sekretarieti ya uchumi itakayosimamiwa na Baraza la Kipapa la Uchumi itakuwa na dhamana ya kutunga sera, kudhibiti mapato na matumizi ya Vatican na Taasisi zake. Katika kipindi cha miezi mitatu, Sekretarieti itapembua na kuchambua hali ya fedha na kuweka bajeti ya kila Baraza la Kipapa na Taasisi za Vatican, kwa kuzingatia vigezo vya ukweli, uwazi na uwajibikaji. Lengo ni kurahisisha shughuli sanjari na kuondokana na urasimu usiokuwa na tija.

Baraza la Kipapa la Uchumi litaundwa na Makardinali wanane na Waamini Walei saba. Kanisa katika masuala ya uchumi na fedha halina budi kusaidiwa na wataalam waliobobea ili liweze kutekeleza dhamana yake kikamilifu. Ni matumaini ya Kardinali Pell kwamba, Baba Mtakatifu Francisko ataweza kumpatia Kikosi kazi kikamilifu, tayari kuanza kuchapa kazi ambayo kwake imekuwa ni heshima kubwa kwake. Kanisa halina budi kushirikiana na wataalam pamoja na kutumia wataalam wa uchumi na fedha kwa ajili ya ustawi na maendeleo ya Kanisa.







All the contents on this site are copyrighted ©.