Viongozi wa Kanisa wamepewa dhamana ya kuwaongoza watu wa Mungu katika hija ya furaha
na utakatifu wa maisha!
Ninyi nyote ni wa Kristo na Kristo ni wa Mungu ni maneno ya Mtakatifu Paulo kwa Wakorintho
waliokuwa wamegawanyika na kuwataka kuachana na mawazo hayo potofu kwa kutambua kwamba,
Mitume ni sehemu ya Jumuiya ya Waamini na Jumuiya nzima ni mali ya Kristo na wala
si vinginevyo.
Majimbo, Parokia pamoja na vyama vyote vya kitume ndani ya
Kanisa vina utu na heshima ile ile inayobubujika kutoka katika Sakramenti ya Ubatizo,
inayowawezesha wote kujisikia kuwa ni Watoto wa Mungu na ndugu zake Kristo!
Hii
ni sehemu ya tafakari iliyotolewa na Baba Mtakatifu Francisko wakati wa Sala ya Malaika
wa Bwana, Jumapili iliyopita tarehe 23 Februari 2014 mara baada ya kuadhimisha Ibada
ya Misa Takatifu na Makardinali kumi na tisa waliosimikwa wakati wa Maadhimisho ya
Siku kuu ya Ukulu wa Mtakatifu Petro, Jumamosi iliyopita kwenye Kanisa kuu la Mtakatifu
Petro mjini Vatican.
Baba Mtakatifu anasema, wale wote waliopokea daraja kwa
ajili ya kuwaongoza watu wa Mungu, kuhubiri pamoja na kuadhimisha Mafumbo ya Kanisa,
watambue kwamba, wamepewa dhamana ya kuwahudumia Watu wa Mungu, kwa kuwasaidia kufanya
hija ya furaha na utakatifu wa maisha na kamwe si wamiliki wa dhamana hii kwa ajili
ya mafao yao binafsi.
Baba Mtakatifu anasema, Mama Kanisa anawadhaminisha na
kuwaalika Makardinali wapya kutolea ushuhuda amini katika maisha na shughuli zao za
kichungaji. Ibada ya kuwasimika Makardinali wapya pamoja na adhimisho la Ibada ya
Misa Takatifu, jumapili iliyopita ni matukio yaliyoonesha Ukatoliki wa Kanisa la Kiulimwengu,
kwa kuwa na Makardinali wanaowakilisha Makanisa mbali mbali mbali, wote wakimzunguka
Khalifa wa Mtakatifu Petro kama kielelezo cha umoja na mshikamano wa Kanisa.
Baba
Mtakatifu anawaalika Makardinali kushirikiana naye katika mchakato wa ujenzi wa umoja
na mshikamano wa Kanisa kwani umoja ni muhimu zaidi kuliko kinzani na vita kwani umoja
ni amri na utashi wa Kristo mwenyewe! Mambo mengine ni mapungufu ya binadamu ambayo
kamwe hayapaswi kuendekezwa. Siku mbili za Mkutano wa Baraza la Makardinali imekuwa
ni fursa ya kuimarisha: imani, umoja na mapendo kwa Kristo na Kanisa lake.
Baba
Mtakatifu anawaalika waamini pamoja na watu wote wenye mapenzi mema, kuendelea kuwasindikiza
Makardinali wapya kwa njia ya sala na sadaka zao, ili waweze kutekeleza dhamana kwa
Jumuiya iliyokabidhiwa mikononi mwao na Mama Kanisa. Viongozi wa Kanisa wanahitaji
kusindikizwa na sala ili kuweza kuwaongoza, kuwatakatifuza na kuwafundisha watu wa
Mungu kwa ari na moyo mkuu.
Viongozi wa Kanisa ni wahudumu wa Kanisa na kwamba,
familia yote ya Mungu inapaswa kutoa ushuhuda unaoonesha uaminifu wao kwa Kristo na
Kanisa lake. Kwa pamoja wafanye hija ya kinabii kwa kutekeleza matamanio ya maisha
ya kiroho yanayooneshwa na watu wa nyakati hizi.