2014-02-24 11:15:20

Madhabahu ya Mashahidi wa Uganda, Namgongo, Uganda kuboreshwa zaidi


Baraza la Maaskofu katoliki Uganda limekamilisha mkakati wa ujenzi wa Hoteli ya Kisasa itakayo kuwa na ghorofa tatu na vyumba 75 kwenye Madhabahu ya Mashahidi wa Uganda, Namgongo. Lengo ni kutaka kuboresha huduma kwa mahujaji wanaomiminika kila Mwaka ifikapo tarehe 3 Juni kwa ajili ya Sherehe ya Mashahidi wa Uganda.

Hayo yamesemwa hivi karibuni na Askofu mkuu Cyprian Kizito Lwanga wa Jimbo kuu la Kampala wakati wa Maadhimisho ya Jubilee ya Miaka 135 ya Ukristo nchini Uganda; Ibada ambayo ilifanyika kwenye eneo la Kigungu, Entebe, Uganda. Madhabahu ya Mashahidi wa Uganda, Namgongo kimekuwa ni kivutio kikubwa cha mahujaji kutoka sehemu mbali mbali ndani na nje ya Uganda wanaokwenda kushuhudia mahali ambapo Mashahidi wa Uganda waliweza kuyamimina maisha yao kwa kuthubutu kuwa waaminifu kwa Kristo na Kanisa lake dhidi ya madhulumu na nyanyaso zilizotolewa na Mfalme Kabaka Mwanga wa, kwenye miaka 1880.

Ujenzi wa Hoteli hii inakadiriwa kugharimu kiasi cha Shilingi za Uganda billioni 2.5 hadi utakapokamilika. Hoteli iliyopo kwa sasa itaboreshwa zaidi ili kukidhi viwango vya kimataifa. Askofu mkuu Lwanga anasema, mradi huu ni sehemu ya vitega uchumi vya Baraza la Maaskofu Katoliki nchini Uganda.







All the contents on this site are copyrighted ©.