2014-02-24 10:10:49

Harambee ya kununua vifaa tiba kwa ajili ya wodi ya Watoto, Hospitali ya Muhimbili


Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Jakaya Mrisho Kikwete Jumamosi, Februari 22, 2014, aliongoza harambee ya kupatikana kwa zaidi ya sh milioni 600 kwa ajili ya ununuzi wa vifaa vya kisasa vya matibabu kwa ajili ya Wodi ya Watoto katika Hospitali ya Taifa, Muhimbili, Dar Es Salaam.

Katika halfa hiyo iliyofanyika kwenye Hoteli ya Golden Tulip, Dar Es Salaam, Rais Kikwete pia ameahidi kuendeleza kuongoza jitihada za kupatikana kwa kiasi cha sh milioni 328 ambazo zinahitaji kukamilisha hesabu ya sh. 929, 915,000 ambazo ndizo zilikuwa lengo la halfa hiyo.

Halfa hiyo pia iliwakutanisha viongozi wakuu wa awamu tatu za uongozi wa juu wa Tanzania ambako Rais wa Pili wa Tanzania, Mzee Ali Hassan Mwinyi na Rais wa Tatu za Tanzania, Mzee Benjamin William Mkapa walikuwa wenyeji wa halfa hiyo kwa nyadhifa zao kama walezi wa Chama cha Madaktari wa Watoto Tanzania (PAT).

Uchangiaji katika halfa hiyo ulikuwa wa aina tatu – kuna fedha taslimu milioni 55.4 zilizochangwa moja kwa moja, kuna ahadi za uchangiaji na kuna wachangiaji walioamua kuwa watatoa fedha za kununua vifaa mbali mbali vinavyohitajika katika Wodi hiyo ambayo gharama yake inakadiriwa kufikia dola za Marekani 570,500.

Katika halfa hiyo, Ikulu ya Rais Kikwete imetoa mchango wa kununua mashine iitwayo “Infant Radiant Warmer” yenye thamani ya dola za Marekani 15,300 wakati Taasisi ya Wanawake na Maendeleo (WAMA) inayoongozwa na Mama Salma Kikwete imechangia ununuzi wa mashine iitwayo Compressor Nebulizer ambayo gharama yake ni dola za Marekani 12,000.








All the contents on this site are copyrighted ©.