Balozi Fulgence Kazaura, Mkuu wa Chuo Kikuu cha Dar es Salaam, amefariki dunia!
Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Jakaya Mrisho Kikwete ameelezea mshituko
na masikitiko yake kufuatia kifo cha Mkuu wa Chuo Kikuu cha Dar Es salaam (UDSM),
Balozi Fulgence Kazaura kilichotokea nchini India, Jumamosi, Februari 22, 2014.
Katika
salamu zake za rambirambi kwa Waziri wa Elimu na Mafunzo ya Ufundi, Mheshimiwa Dkt.
Shukuru Kawambwa, Rais Kikwete amesema: “Nimepokea kwa mshituko, masikitiko na huzuni
taarifa ya kifo cha Mkuu wa Chuo Kikuu cha Dar es Salaam, Balozi Flugence Kazaura,
ambacho nimejulishwa kuwa kimetokea katika Kituo cha Matibabu ya Kansa katika mji
wa Chennai, nchini India.”
“Kwa hakika, kifo cha Mzee Kazaura siyo kwamba kimekipokonya
Chuo Kikuu cha Dar es Salaam kiongozi hodari na mwenye visheni kubwa, lakini kifo
hicho kimeondolea Tanzania mmoja wa watumishi hodari wa umma. Mzee Kazaura pia alikuwa
mtumishi mwaminifu na mwadilifu kwa nchi yake na sote tunaendelea kwa kumkumbuka kwa
sifa hizo na mchango wake mkubwa katika utumishi wa umma,” amesema Rais Kikwete na
kuongeza:
“Alithibitisha sifa hizo katika nafasi zote alizozishikilia katika
maisha yake tokea alipokuwa Katibu Mkuu katika wizara mbali, hadi alipokuwa Balozi
wa Tanzania Makao Makuu ya Umoja wa Ulaya (EU) na nchini Ubelgiji, hadi alipoteuliwa
Mshauri Maalum wa Uchumi wa Rais, hadi alipokuwa Naibu Katibu Mkuu wa Jumuia ya Afrika
Mashairiki (EAC) katika uongozi mbali mbali za Bodi za mashirika ya umma na binafsi
na hata kwenye nafasi yake ya Ukuu wa Chuo Kikuu cha Dar Es salaam kwa miaka tisa.
Tutaendelea kumkumbuka.”
Ameongeza Rais Kikwete: “Nakutumia wewe Waziri wa
Elimu na Mafunzo ya Ufundi, Dkt. Shukuru Kawambwa salamu zangu za rambirambi kufuatia
msiba huu mkubwa. Aidha, kupitia kwako naitumia jumuia nzima ya Chuo Kikuu cha Dar
Es Salaam pole nyingi kwa kuondokewa na kiongozi wao.”
“Nakuomba pia unifikisshie
salamu zangu za pole nyingi kwa familia ya Mzee Kazaura. Wajulishe kuwa naungana nao
katika kuomboleza kifo cha Mzee wetu huyu na kwamba msiba wao ni msiba wangu pia.
Pia naomba wajue kuwa naungana nao katika kumwomba Mwenyezi Mungu, Mwingi wa Rehema,
aiweke mahali pema peponi roho ya Marehemu Fulgence Kazaura. Amina.”
TAARIFA
KWA VYOMBO VYA HABARI
Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mheshimiwa
Jakaya Mrisho Kikwete ameihakikishia Misri kuwa Tanzania itaunga mkono jitihada za
nchi hiyo kurejeshewa uanachama wake katika Umoja wa Afrika (AU) baada ya kufanyika
kwa uchaguzi mkuu wa kidemokrasia nchini humo Aprili mwaka huu.
Rais Kikwete
pia amesisitiza kuwa msimamo wa Tanzania kuhusu matumizi ya maji ya Mto Nile ni kwamba
nchi zote ambako Mto huo unapitia, kwa namna moja ama nyingine, zina haki sawa ya
kutumia maji ya Mto huo kwa maendeleo ya nchi hizo. Aidha, Rais Kikwete ameishukuru
Misri kwa kuchangia maendeleo ya Tanzania kwa kuunga mkono jitihada hizo kwa misaada
katika sekta mbali mbali na hasa sekta za maji na afya.
Rais Kikwete ameyasema
hayo jioni, Jumamosi, Februari 22, 2014, wakati alipokutana na kufanya mazungumzo
na Waziri wa Mambo ya Nje wa Misri, Mheshimiwa Nabil Fahmy ambaye pia amewasilisha
ujumbe maalum kwa Rais Kikwete kutoka kwa Rais wa muda wa Misri, Mheshimiwa Adly Mansour.
Katika
mazungumzo hayo, Mheshimiwa Fahmy aliiomba Tanzania kuunga mkono jitihada za Misri
kurejeshewa uanachama wake wa AU kufuatia kusikitishwa kwa uanachama huo baada ya
kuondolewa madarakani kwa kiongozi wa nchi hiyo aliyekuwa amechaguliwa kwa njia ya
kidemokrasia, Mheshimiwa Mohamed Morsi mwaka jana.
Rais Kikwete alimhakikishia
Waziri Fahmy kuwa Tanzania haitasita kuunga mkono jitihada hizo lakini baada ya Misri
kuwa imefanya uchaguzi wa kidemokrasia mwezi Aprili mwaka huu. “Kwa mujibu wa Makubaliano
ya Uanzishwaji wa AU, itakuwa vigumu kwa Misri kurejeshewa uanachama wake katika mazingira
ya sasa. Lakini baada ya kuwa kufanyika kwa uchaguzi wa kidemokrasia kuchagua kiongozi
mpya, Tanzania itakuwepo kuunga mkono jitihada hizo za Misri,” Rais kikwete alimwambia
Waziri Fahmy.
Kuhusu matumizi ya maji ya Mto Nile, Rais Kikwete alisisitiza
msimamo wa Tanzania wa kuwa ni haki ya kila nchi ambako Mto huo unapitia kutumia maji
yake kwa maendeleo yake. “Tunaamini katika Haki ya Matumizi ya Maji kwa nchi zote
ambako Mto huu unapitia. Ni aina ya haki hiyo ambayo inatumika hata Tanzania kulingana
na matumizi ya maji ya mito mbali mbali ndani ya Tanzania,”
Mapema Waziri Fahmy
alimwambia Rais Kikwete kuhusu umuhimu wa maji ya Mto Nile kwa nchi ya Misri akisema:
“Sisi katika Misri hupata mvua kwa siku tatu kwa wastani kwa mwaka. Maji yote tunayotumia
yanatokana na Mto Nile. Hivyo, unaweza kuelewa umuhimu wa Mto huo kwa uhaki na ustawi
wa nchi yetu.” Rais Kikwete pia ameishukuru Misri kwa misaada yake ya maendeleo kwa
Tanzania hasa katika sekta za afya na maji.