Papa ateuwa Marais watakaosimamia Maadhimisho ya Sinodi ya Maaskofu kuhusu Familia
Baba Mtakatifu Francisko amemshukuru na kumpongeza Kardinali Walter Kasper aliyewawezesha
Mababa wa Kanisa kufanya tafakari ya kina kuhusu umuhimu wa familia kadiri ya mpango
wa Mungu pamoja na kuangalia changamoto zinazoendelea kujitokeza katika maisha ya
ndoa na familia, ili Kanisa liweze kuibua mbinu mkakati wa kichungaji utakaowawezesha
waamini kuendelea kutambua umuhimu wa familia katika maisha na utume wa Kanisa na
Jamii katika ujumla wake.
Baba Mtakatifu amemwambia Kardinali Kasper kwamba,
tafakari yake ni taalimungu iliyoandikwa kwa njia ya kupiga magoti. Baba Mtakatifu
amewateua Makardinali Andrè Vingt-Trois, Askofu mkuu wa Jimbo kuu la Paris, Ufaransa,
Kardinali Raymundo Damascene Assis kutoka Brazil pamoja na Kardinali Luis Antonio
Tagle kuwa ni Marais wateule wakati wa Maadhimisho ya Sinodi Maalum ya Maaskofu kuhusu
Familia itakayofanyika mjini Vatican mwezi Oktoba, 2014. Majina haya yametajwa na
Baba Mtakatifu Francisko mbele ya Makardinali 150 waliokuwa wanahudhuria Mkutano wa
Makardinali kuhusu Familia hapa mjini Vatican.
Makardinali hawa watasaidiana
na Kardinali Peter Erdo na Askofu mkuu Bruno Forte walioteuliwa na Papa Francisko
kuwa wahamasishaji wakuu wakati wa Maadhimisho ya Sinodi Maalum ya Maaskofu kwa ajili
ya Familia. Makardinali wengi waliweza kuchangia katika mada kuhusu Familia na wengine
wametoa mchango wao kwa njia ya maandishi na utazingatiwa. Makardinali wameangalia
familia ya binadamu mintarafu mafundisho ya Kanisa; mahusiano ya kibinadamu mintarafu
mpango wa Mungu; madhara ya utandawazi na mwelekeo potofu wa maisha ya ndoa na familia.
Mafundisho
ya Kanisa kuhusu ndoa na familia yamejikita katika mchango uliotolewa na Mwenyeheri
Yohane Paulo II katika Waraka wake wa Kichungaji, Familiaris Consortio yaani "Wajibu
wa Familia za Kikristo katika Ulimwengu Mamboleo" pamoja na Katekisimu Mpya ya Kanisa
Katoliki. Makardinali wamedodosa baadhi ya mikakati ya kichungaji kwa ajili ya maisha
ya ndoa na familia; umuhimu wa maandalizi makini kwa wanandoa; tasaufi ya maisha ya
ndoa na familia.
Mababa wa Kanisa wamegusia pia tatizo la wanandoa waliooana
wakaachana na baadaye kuoa au kuolewa tena mintarafu sheria za Kanisa kuhusu uhalali
wa ndoa na sababu zinazoweza kupelekea kufutwa kwa ndoa zilizofungwa Kanisani. Padre
Federico Lombardi anasema, majadiliano yote haya yamefanyika katika hali ya utulivu
pamoja na kuangalia uwezekano kwa waamini wenye shida na mahangaiko haya kupewa Sakramenti
za Kanisa kwa kuangalia: huruma ya Kristo, uaminifu kwa Kristo na Kanisa lake na kwamba,
haya ni mambo yanayopaswa kuangaliwa kwa watu husika.
Mawazo yote haya ni
sehemu ya hija ya Maadhimisho ya Sinodi ya Maalum ya Maaskofu kwa ajili ya Familia.
Tafakari hizi zimejikita katika Neno la Mungu na Mafundisho ya Kanisa. Familia za
wakimbizi na wahamiaji pamoja na familia za Kikristo zinazoishi katika nchi ambazo
zinajikuta zina idadi ndogo ya Wakristo.