2014-02-22 08:57:26

Katiba Mpya ya Zambia iwe ni sehemu ya matunda ya Jubilee ya Miaka 50 ya Uhuru nchini Zambia!


Jubilee ya Miaka 50 ya Uhuru wa Zambia, iwe ni fursa kwa wananchi kujipatia maendeleo makubwa zaidi kwa kuondokana na umaskini wa hali na kipato; magonjwa pamoja na ukosefu wa haki msingi za binadamu. Hii ndiyo changamoto inayotolewa na Jukwaa la Viongozi wa Kikristo nchini Zambia lijulikanalo kama "Oasis Forum" wakati huu Zambia inapojiandaa kuadhimisha Jubilee ya Miaka 50 tangu ilipojipatia uhuru wa bendera.

Jukwaa la Viongozi wa Kikristo linasema, inasikitisha kuona kwamba, Zambia inaadhimisha Jubilee ya Miaka 50 ya Uhuru wa Bendera wakati ambapo kuna umati mkubwa wa wananchi unaoendelea kuogelea katika dimbwi la umaskini, njaa na ujinga, kiasi hata cha kutishiwa usalama wa maisha na viongozi waliowachagua na kuwapatia madaraka.

Jukwaa la Viongozi wa Kikristo linawapongeza wananchi wote wa Zambia waliojifunga kibwebwe wakapigania na hatimaye wakapata Uhuru wa Bendera. Ni kundi la wananchi wa Zambia lililokuwa na mtazamo mpana, vipeo na utume uliotakiwa kutekelezwa kwa ajili ya ustawi na maendeleo ya wananchi wote wa Zambia.

Wazambia walitamani kujenga na kuendeleza uhuru na demokrasia si tu kwa kujitawala kutoka katika makucha ya wakoloni bali pia walitaka kuhakikisha kwamba, wananchi wa Zambia kwa njia ya mshikamano wa upendo na umoja wa kitaifa wangeweza kuupatia kisogo umaskini, njaa na maradhi; tayari kusimama kidete kupinga ukosefu wa haki msingi za binadamu na unyonywaji unaoweza kuendelezwa kwa kuwatumia viongozi wa ndani.

Jukwaa la viongozi wa Kikristo linasema, njia makini na murua kabisa ya kuwaenzi wapigania uhuru kutoka Zambia katika Maadhimisho ya Jubilee ya Miaka 50 ya Uhuru wa Bendera ni kuhakikisha kwamba, Katiba Mpya ya Zambia inapatikana kwa muda muafaka, ili Zambia iweze kufikia malengo, vipeo na utume wake kwa ajili ya ustawi na maendeleo ya wananchi wake.

Kimsingi Jukwaa la viongozi wa Kikristo halipingi Maadhimisho ya Jubilee ya Miaka 50 ya Uhuru wa Bendera nchini Zambia, bali linachotaka ni kuhakikisha kwamba, kumbu kumbu hii inaacha alama ya kudumu kwa wananchi wa Zambia katika harakati na mchakato wa kukuza na kudumisha demokrasia, utawala wa sheria, ustawi na mafao ya wengi.







All the contents on this site are copyrighted ©.