2014-02-20 09:54:05

Askofu mteule wa Jimbo Katoliki Monze, Zambia anatarajiwa kuwekwa wakfu na kusimikwa rasmi hapo tarehe 3 Mei 2014


Askofu mteule Moses Hamungole wa Jimbo Katoliki Monze, Zambia aliyeteuliwa hivi karibuni na Baba Mtakatifu Francisko kuwa Askofu Mpya wa Jimbo Katoliki Monze, Jumatano tarehe 19 Februari 2014 alikiri kanuni ya Imani na kula kiapo cha utii kwa Khalifa wa Mtakatifu Petro, katika Ibada iliyofanyika kwenye Kikanisa cha Baraza la Kipapa la uenezaji wa imani. Askofu mteule Hamungole anatarajiwa kuwekwa wakfu na kusimikwa rasmi kuwa Askofu wa Jimbo Katoliki Monze hapo tarehe 3 Mei 2014 RealAudioMP3

Ibada hii imehudhuriwa na viongozi waandamizi kutoka Baraza la Kipapa la Uenezaji wa Imani, wananchi wa Zambia, wafanyakazi kutoka Radio Vatican pamoja na marafiki. Lengo la Ibada hii ni kumkumbusha Askofu mteule kwamba, baada ya kuteuliwa na Baba Mtakatifu kuongoza, kuwatakatifuza na kuwafundisha Watu wa Mungu Jimbo Katoliki la Monze sasa anakuwa ni chombo cha neema kwa watu wake na hivyo atapaswa kumtegemea Mwenyezi Mungu katika maisha na utume wake, daima akijitahidi kuwa mwaminifu kwa Kristo na Kanisa lake.

Askofu mkuu Protase Rugambwa, Katibu mwambata na Rais wa Mashirika ya Kimissionari ya Kipapa, alimtakia kheri na baraka kwa utume huu mpya. Anaialika Familia ya Mungu Jimbo Katoliki Monze kumwonesha umoja, ushirikiano na mshikamano Askofu mteule Moses Hamungole katika maisha na utume wake kama Askofu wa Jimbo Katoliki Monze.







All the contents on this site are copyrighted ©.