2014-02-19 12:07:23

Jinamizi la vikwazo vya kiuchumi bado linamwandama Rais Robert Mugabe wa Zimbabwe


Mawaziri wa Mambo ya nchi za nje na ushirikiano wa kimataifa Umoja wa Ulaya wameiondolea Zimbabwe vikwazo vya kiuchumi, lakini wamekataa kumwondolea vikwazo hivyo Rais Robert Mugabe wa Zimbabwe. Hivi ni vikwazo ambavyo Zimbabwe iliwekewa kunako mwaka 2002 wakati wa machafuko ya hali ya kisiasa yaliyopelekea kuundwa kwa Serikali ya Umoja wa Kitaifa.

Uvunjwaji wa haki msingi za binadamu na kuchechea kwa mfumo wa demokrasi nchi Zimbabwe ni kati ya mambo msingi yaliyopelekea Umoja wa Ulaya kuiwekea Zimbabwe vikwazo vya kiuchumi. Kutokana na vikwazo hivi, Rais Robert Mugabe hataruhusiwa kusafiri katika nchi za Ulaya hadi tarehe 20 Februari 2015 vikwazo hivi vitakapokwisha muda wake.

Rais Mugabe hapo tarehe 21 Februari 2014 atasherehekea Miaka 90 tangu alipozaliwa na miaka 34 ya kuiongoza Zimbabwe kama Rais, bado anakabiliwa na shinikizo la kutoweza kuhudhuria kwenye mkutano kati ya Nchi za Umoja wa Afrika na Umoja wa Ulaya, unaotarajiwa kufanyika mwezi Aprili 2014.

Wakati huo huo, habari kutoka Zimbabwe zinasema kwamba, Serikali ya Zimbabwe imewaachilia huru wafungwa elfu mbili waliokuwa wanatumikia vifungo katika magereza mbali mbali nchini humo. Hii inatokana na hali ngumu ya uchumi pamoja na makundi ya kutetea haki za binadamu yanayodai kwamba, wafungwa nchini Zimbabwe wanaishi katika mazingira hatarishi sana na kwamba, wengi wao wanafariki dunia kutokana na njaa magerezani.







All the contents on this site are copyrighted ©.