2014-02-17 10:14:56

Zingatieni mambo msingi kwa mafao ya watanzania wote wakati wa kujadili muswada wa Katiba Mpya!


Rais Jakaya Mrisho Kikwete wa Tanzania hivi karibuni alipokuwa anazungumza kwenye kikao cha Baraza la Vyama vya Siasa nchini Tanzania alisema kwamba,

Bunge la Katiba ndilo lenye mamlaka ya kutunga Katiba mpya ya nchi ya Tanzania. Hatua zote zilizopita ni za kutoa mapendekezo jukumu ambalo Tume ya Mabadiliko ya Katiba imelikamilisha vyema. Ipo Rasimu ya Katiba itakayofikishwa kwenye Bunge Maalum kujadiliwa na kufanyiwa uamuzi. Ingekuwa Bunge la kawaida au Baraza la Wawakilishi, Rasimu ya Katiba ndiyo Muswada wa Sheria utakaofikishwa Bungeni na kwenye Baraza.

Wajumbe wa Bunge hilo watambue kuwa wana dhamana isiyokuwa na mfano wake kwa nchi yetu na Watanzania wenzao kwa jumla. Wanalo jukumu la kuwapatia Katiba nzuri itakayodumu kwa zaidi ya miaka 50 ijayo. Katiba itakayoimarisha Muungano badala ya kuudhoofisha. Katiba itakayodumisha umoja, amani na utulivu nchini badala ya kuvuruga.

Vilevile Katiba itakayoweka mazingira mazuri ya kisiasa, kijamii na kiuchumi na kuongeza kasi ya maendeleo ya nchi yetu na ustawi wa watu wake kwa miaka mingi ijayo. Ili haya yafanyike ni vyema Wajumbe wajue vyema kinachopendekezwa, wapambanue kinachofaa na kisichofaa, na kubwa zaidi, watangulize maslahi ya taifa mbele kuliko maslahi yao binafsi au ya makundi yao.








All the contents on this site are copyrighted ©.