2014-02-15 15:25:07

Tokeni kifua mbele kutangaza Habari Njema ya Wokovu na wala msiogope wala kuona soni!


Baba Mtakatifu Francisko ameitaka Jumuiya ya Kikatoliki ya Shalom kupiga moyo konde na kusonga mbele kwa ari na moyo mkuu ili kutangaza Habari Njema ya Wokovu pasi na woga wala makunyanzi! Baba Mtakatifu ameyasema hayo alipokutana na Muasisi wa Jumuiya ya Kikatoliki ya Shalom Moyses de Azevedo Filho, kwenye Makazi yake yaliyoko kwenye Hosteli ya Mtakatifu Martha, yaliyoko mjini Vatican, siku ya Ijumaa tarehe 14 Februari 2014.

Baba Mtakatifu Francisko anaifahamu Jumuiya hii na kwa mara ya kwanza walikutana kunako Mwaka 2007 wakati wa Maadhimisho ya Mkutano wa Aparecida, nchini Brazil. Kanisa likaitambua Jumuiya hii na kuipatia hadhi yake ndani ya Kanisa, kama kumbukumbu endelevu ya Hija ya kichungaji ya Mwenyeheri Yohane Paulo wa Pili aliyoifanya nchini Brazil kunako Mwaka 1980. Leo hii Jumuiya ya Kikatoliki ya Shalom imeenea katika nchi ishirini na mbili na ina jumla ya wanachama 40, 000.

Akizungumza na Radio Vatican kwa njia ya simu Bwana Moyses de Azevedo anasema, mazungumzo yake na Baba Mtakatifu Francisko ilikuwa ni fursa ya kurudia tena majitoleo na sadaka yao kwa ajili ya kutangaza Injili ya Furaha hadi miisho ya dunia. Jumuiya hii imekwisha anza kuona matunda ya utume wake kwa Padre Joao Chagas kuteuliwa kuwa ni Mratibu wa Siku za Vijana Duniani, kwenye Baraza la Kipapa la Walei.

Hii ni neema ambayo Jumuiya ya Kikatoliki ya Shalom imepata kutoka kwa Mwenyezi Mungu kwa njia ya huduma na utume miongoni mwa vijana, ni uthibitisho wa karama ya Jumuiya hii ambayo inatoa kipaumbele cha kwanza kwa ustawi na maendeleo ya Kanisa.







All the contents on this site are copyrighted ©.