2014-02-15 15:16:17

Rais wa Cyprus akutana na Papa Francisko mjini Vatican


Baba Mtakatifu Francisko Jumamosi, tarehe 15 Februari 2014 amekutana na kuzungumza na Rais Nicos Anastasiades ambaye baadaye alikutana na Kardinali mteule Pietro Parolin, Katibu mkuu wa Vatican aliyekuwa ameambata na Askofu mkuu Dominique Mamberti, Katibu mkuu wa mambo ya nchi za nje na ushirikiano wa kimataifa mjini Vatican.

Viongozi hawa wawili wamejadili pamoja na mambo mengine kuhusu uhusiano kati ya Cyprus na Vatican; mchango mkubwa unaotolewa na Kanisa Katoliki nchini humo pamoja na umuhimu wa kuendelea kusimama kidete kulinda na kutetea uhuru wa kidini. Kwa pamoja wameonesha matumaini makubwa baada ya kuanza tena majadiliano ya kisiasa yanayopania kupata ufumbuzi wa kudumu kutokana na hali ngumu inayoendelea nchini Cyprus kwa sasa.

Baba Mtakatifu na mgeni wake wameangalia pia kinzani, migogoro na vita huko Mashariki ya Kati ambayo imesababisha maafa makubwa kwa watu na mali zao. Ni matumaini ya viongozi hawa kwamba, Jumuiya za Kikristo huko Mashariki ya kati zitachangia katika ustawi na maendeleo ya Ukanda huu.







All the contents on this site are copyrighted ©.