Kongamano la Kimataifa kuhusu Waraka wa Liturujia ya Kanisa
Baraza la Kipapa la Ibada na nidhamu ya Sakramenti za Kanisa kuanzia tarehe 18 hadi
20 Februari 2014 litaadhimisha Kongamano la Kimataifa, kuhusu Jubilee ya Miaka 50
tangu Mababa wa Mtaguso mkuu wa Pili wa Vatican walipochapisha Waraka kuhusu Liturujia
ya Kanisa "Sacrosanctum Concilium", litakaloongozwa na kauli mbiu Waraka wa Liturujia,
shukrani na dhamana kwa ajili ya mabadiliko ya Kikanisa".
Kongamano hili litawashirikisha
wadau kutoka sehemu mbali mbali za dunia na utakuwa ni muda muafaka kwa ajili ya
kusali, kutafakari, kuabudu na kuadhimisha Mafumbo ya Kanisa. Ni kipindi cha kuonjeshana
uzoefu na mang'amuzi ya Liturujia ya Kanisa, tayari kutweka hadi kilindini kwa ajili
ya kuendeleza dhamana ya Liturujia katika maisha na utume wa Kanisa.
Akizungumzia
kuhusu Kongamano hili la Kimataifa litakalofanyika kwenye Chuo kikuu cha Kipapa cha
Laterano, Askofu Arthur Roche, Katibu mkuu wa Baraza la Kipapa la Ibada na nidhamu
ya Sakramenti za Kanisa anasema mabadiliko ya Liturujia ya Kanisa ni sehemu ya mchakato
mzima wa mageuzi yaliyofanywa na Mababa wa Mtaguso mkuu wa Pili wa Vatican katika
maisha na utume wa Kanisa, kwa kuhimiza mambo yale yanayoleta umoja na mshikamano
miongoni mwa wafuasi wa Kristo; kwa kujali, kurekebisha na kukuza Liturujia inayodhihirisha
Fumbo la maisha ya Kristo na maumbile halisi ya Kanisa, kwa kuwajenga na kuwaimarisha
waamini katika mchakato wa kuelekea katika ukamilifu.
Ni kwa njia ya Liturujia
Mungu hutukuzwa kikamilifu na wanadamu wanatakatifuzwa na kwamba, Kristo hushiriki
daima katika Kanisa lake, ili Mwenyezi Mungu aweze kuabudiwa milele. Kanisa linapenda
kukazia kwa namna ya pekee umuhimu wa Liturujia katika maisha na utume wake, kwa kuwataka
waamini kufanya rejea mara kwa mara katika mafundisho yanayotolewa na Mama Kanisa
kwa ajili ya ustawi na maendeleo ya maisha yao kiroho.
Changamoto kubwa iliyoko
mbele ya Mama Kanisa ni kutaka kuhakikisha kwamba, waamini wanafundwa kikamilifu kuhusiana
na Liturujia ya Kanisa ili waweze kuwa na ushiriki mkamilifu bila kusahau kuwaandaa
wataalam katika Liturujia, ili kuendeleza mchakato wa mabadiliko yaliyofanywa na Mababa
wa Mtaguso mkuu wa Pili wa Vatican. Tafsiri ya vitabu vya Liturujia katika lugha mbali
mbali pamoja na mchakato wa utamadunisho ni kati ya matunda makuu yaliyoletwa na Mtaguso
mkuu wa Pili wa Vatican.
Jubilee ya Miaka 50 ya Waraka wa Liturujia kiwe ni
kipindi cha kufanya upembuzi yakinifu kuhusu Fumbo la Kanisa linalosali na kuhamasishwa
kuwatangazia watu Habari Njema ya Wokovu kwa njia ya ushuhuda wa imani tendaji. Ushuhuda
huu unabubujika kutoka katika Kanisa linalosali na kuinjilisha.
Kwa upande
wake KardinaliAntonio Canizares Llovera, Mwenyekiti wa Baraza la Kipapa la Ibada na
nidhamu ya Sakramenti za Kanisa anasema, Waraka wa Liturujia ni kielelezo cha Pentekoste
mpya ndani ya Kanisa iliyoleta mwanga wa matumaini mapya katika mchakato wa mabadiliko
ya ndani, kwa kukazia mshikamano wa upendo unaobubujika kutoka ndani ya Kristo na
Kanisa lake kwa ajili ya binadamu wote.
Kanisa likajikuta linaanza mchakato
wa mageuzi na kujitakasa, tayari kutoka kifua mbele kuwatangazia watu Habari Njema
ya Wokovu, changamoto ya kuendeleza dhamana hii katika ulimwengu wa utandawazi. Waamini
wajitaabishe kusoma nyaraka za Mtaguso mkuu wa Pili wa Vatican kwa ajili ya kushiriki
katika maboresho ya maisha na utume wa Kanisa. Liturujia ya Kanisa iwawezeshe waamini
kulifahamu, kuliadhimisha na kushiriki kikamilifu Fumbo la Maisha ya Kristo.
Liturujia
ni chemchemi ya maisha ya kimungu, shule ya kwanza ya moyo wa mwanadamu na zawadi
ya kwanza inayowaunganisha waamini katika imani na maisha ya sala, changamoto ya kumwimbia
Mwenyezi Mungu utenzi wa sifa na shukrani. Katika Liturujia Fumbo la Utatu Mtakatifu
linapaswa kupewa kipaumbele cha kwanza; waamini wajitengee muda wa kutafakari Neno
la Mungu,
Kongamano la Kimataifa kuhusu Liturujia linaongozwa na maneno makuu
mawili: kushukuru na dhamana inayopaswa kufanyiwa kazi kwa sasa ili kuhakikisha kwamba,
mabadiliko yaliyoletwa na Mababa wa Mtaguso mkuu wa Pili wa Vatican kwa kujikita katika
Uinjilishaji Mpya kwa kuendelea kusoma alama za nyakati kwa kujikita katika upendo
kwa Mungu na jirani; ili kujenga na kukuza ari na moyo wa watu wa Mungu waliotakaswa
tayari kujitosa kimasomaso kulinda na kutetea misingi ya haki, amani na upendo.
Akichangia
mada kuhusu Kongamano hili la Kimataifa, Askofu Enrico Covolo, Mkuu wa Chuo Kikuu
cha Kipapa cha Laterano anasema, Kanisa linayo kila sababu ya kumshukuru Mwenyezi
Mungu kwa mang'amuzi na busara iliyooneshwa na Mababa wa Mtaguso mkuu wa Pili wa Vatican
katika maisha na utume wa Kanisa.
Kati ya matunda ya mabadiliko haya ni umoja
na mshikamano wa Kikanisa; umuhimu wa Maadhimisho ya Fumbo la Ekaristi Takatifu lenye
mwelekeo wa Kijumuiya na Kikanisa na kutambua kwamba, waamini wote ni sehemu ya Fumbo
la Mwili wa Kristo, yaani Kanisa. Liturujia inakuwa ni shule ya Sala za Kikristo na
chachu ya kusoma na kulitafakari Neno la Mungu.
Imehaririwa na Padre Richard
A. Mjigwa, C.PP.S. Idhaa ya Kiswahili ya Radio Vatican.