2014-02-13 15:02:23

Wayahudi na Wakatoliki wanaweza kusaidia mchakato wa ujenzi wa misingi ya haki, amani na maendeleo ya wengi!


Kamati ya Wayahudi kutoka Marekani imekuwa na uhusiano mzuri na Vatican na kwamba, imechangia kwa kiasi kikubwa katika mchakato wa majadiliano ya kidini kati ya Wayahudi na Wakatoliki, changamoto iliyotolewa na Mababa wa Mtaguso mkuu wa Vatican yapata miaka hamsini iliyopita. Wayahudi na Wakatoliki wanao urithi mkubwa katika maisha ya kiroho, msingi katika majadiliano ya kidini baina ya pande hizi mbili, kwa kutambua kwamba, uhusiano wa pekee walionao mbele ya Mwenyezi Mungu.

Hayo yamesemwa na Baba Mtakatifu Francisko Alhamisi, tarehe 13 Februari 2014 alipokutana na kuzungumza na wajumbe wa Kamati ya Wayahudi kutoka Marekani waliomtembelea mjini Vatican. Anasema, Wayahudi na Wakatoliki wanaweza kushirikiana kwa pamoja katika kukoleza mchakato wa ujenzi wa misingi ya haki, amani na udugu duniani; kwa kujikita katika huduma makini kwa maskini na wote wanaosukumizwa pembezoni mwa Jamii, kama yanavyohimiza Maandiko Matakatifu. Huu ni utashi na haki ya Mungu dhamana inayopaswa kufanyiwa kazi na waamini wote.

Ili majadiliano ya kidini yaweze kuzaa matunda yanayokusudiwa, kuna haja kwa wahusika kurithisha mang'amuzi ya urafiki, heshima na kuthaminiana ambayo yamefanyiwa kazi katika kipindi cha miaka yote na Tume ya Wayahudi kutoka Marekani. Ni matumaini ya Baba Mtakatifu kwamba, Tume hii itaendeleza tema juu ya uhusiano kati ya Wayahudi na Wakatoliki katika: Seminari na vituo mbali mbali vya elimu kwa waamini walei ndani ya Kanisa Katoliki sambamba na Marabbi nao kujitahidi kufahamu Ukristo.

Baba Mtakatifu amewaambia kwamba, baada ya muda si mrefu anatarajiwa kufanya hija ya kichungaji katika Nchi Takatifu, anawaalika na kuwaomba, ili waweze kumsindikiza katika sala zao ili hija hii ya maisha ya kiroho iweze kuzaa matunda ya umoja, matumaini na amani.







All the contents on this site are copyrighted ©.