2014-02-13 11:53:21

Usipokuwa makini, imani yako inaweza kuzimika kama kibatari!


Mwamini anaweza kupoteza dira na mwelekeo wa imani yake kwa kukumbatia malimwengu na kwa upande mwingine mtu asiyeamini katika unyenyekevu wake anaweza kukirimiwa zawadi ya imani na kuwa ni mfano na kielelezo cha kuigwa kama ilivyojitokeza kwa Mwanamke Myunani aliyempigia Yesu magoti akitaka huruma na upendo kwa ajili ya mtoto wake aliyekuwa anasumbuliwa na pepo mchafu.

Baada ya majadiliano ya kina, Yesu anamponya mtoto wake kutokana na imani kubwa aliyoonesha Mama yule mbele ya Yesu.

Ni maneno ya Baba Mtakatifu Francisko wakati wa mahubiri yake kwenye Ibada ya Misa Takatifu kwenye Kikanisa cha Mtakatifu Martha, kilichoko mjini Vatican siku ya Alhamisi, tarehe 13 Februari 2014. Anasema, kuna kundi kubwa la waamini ndani ya Kanisa linalofanya hija ya kutaka kukutana na Yesu katika maisha yao, kwa kusukumwa na Roho Mtakatifu.

Baba Mtakatifu anaonya kwamba, kuna baadhi ya watu wamelewa mno madaraka pamoja na kumezwa na malimwengu, kiasi cha kuthubutu kuharibu uhusiano mwema waliokuwa nao mbele ya Mwenyezi Mungu, kwa kukumbatia ukahaba uliowasaliti, kama ilivyotokea kwa Mfalme Sulemani, aliyekuwa na hekima, busara na nguvu nyingi, lakini mbele ya wanawake "akanywea na kuzimika kama kibatari kiasi cha kupoteza imani yake! Inaweza pia kutokea kwa waamini kuifahamu Kanuni ya Imani kwa kichwa lakini wakajikuta kwamba, hawana tena imani.

Mfalme Sulemani alikuwa mdhambi kama baba yake Daudi, lakini akaelemewa na udhaifu wake kiasi kwamba, akajikuta anakuwa ni fisadi na jeuri kiasi cha kushindwa kuomba msamaha kama alivyofanya Mfalme Daudi na matokeo yake akapoteza imani kutoka katika undani wa moyo wake.

Neno la Mungu linapaswa kupokelewa na kumwilishwa katika maisha ya unyenyekevu kama alivyofanya yule mwanamke Myunani anayesimuliwa kwenye Liturujia ya Neno la Mungu, kiasi hata cha kukirimiwa ukombozi.







All the contents on this site are copyrighted ©.