2014-02-13 08:53:38

Siku ya wapendanao kwa Mwaka 2014 yaaani we acha tu!


Baba Mtakatifu Francisko, Ijumaa tarehe 14 Februari 2014 Siku ya wapendanao anatarajiwa majira ya mchana kukutana na kuzungumza na wanandoa watarajiwa kutoka sehemu mbali mbali za dunia kwenye Uwanja wa Kanisa kuu la Mtakatifu Petro mjini Vatican kama sehemu ya Maandali ya Sinodi Maalum ya Maaskofu kwa ajili ya Familia itakayoadhimishwa mjini Vatican mwezi Oktoba mwaka huu. RealAudioMP3

Taarifa inaonesha kwamba, wanandoa watarajiwa ni kutoka katika nchi ishirini na nane, hawa ni wale wanaotarajia kufunga ndoa katika siku za usoni, ili kuhakikisha kwamba, upendo wao unadumu hadi pale kifo kitakapowatenganisha kadiri ya mpango wa Mwenyezi Mungu.

Sherehe hizi za wapendanao zinatarajiwa kuanza majira ya saa 5: 00 kwa saa za Ulaya. Wanandoa watarajiwa watashirikishana kwanza mambo msingi katika historia ya maisha yao ya upendo. Saa 6:00 Baba Mtakatifu anatarajiwa kuwasili uwanjani na kuanza kuzungumza na baadhi ya wanandoa kuhusu: matatizo, changamoto, ubora wa maisha ya familia za Kikristo, wajibu na dhamana ya kuchagua kuadhimisha Sakramenti ya ndoa Kanisani.

Kwa bahati mbaya anasema, Askofu mkuu Vincenzo Paglia, Rais wa Baraza la Kipapa la familia baadhi ya wanandoa wamekuwa na tabia ya kuahilisha kufunga ndoa Kanisa kwa visingizio vya matatizo na changamoto za maisha. Kuna haja ya kua na sera makini kuhusu maisha ya ndoa na familia, kwa kutambua na kuheshimu dhamana ya maisha na utume wa ndoa katika Jamii na Kanisa kwa ujumla.

Siku hii ya wapendanao, itakamilishwa kwa Sala iliyotungwa na wanandoa watarajiwa na kila mmoja atapata zawadi maalum iliyoandaliwa na Baba Mtakatifu Francisko kama kumbu kumbu ya Siku yao ya ndoa!








All the contents on this site are copyrighted ©.