Mchango wa Kanisa katika sekta ya elimu ni kielelezo cha uhai wa Injili katika sayansi
na tamaduni za watu
Baraza la Kipapa la Elimu Katoliki kuanzia tarehe 12 hadi tarehe 14 Februari 2014
linafanya mkutano wake mkuu wa mwanzo wa Mwaka. Tarehe 12 Februari, limeendesha warsha
ya siku moja kwenye Chuo Kikuu cha Kipapa cha Urbaniana, kwa kuongozwa na kauli mbiu
"Mchakato wa Uelimishaji leo na kesho".
Wajumbe wamepembua pamoja na mambo
mengine kuhusu mabadiliko katika Waraka wa Kitume unaojadili kuhusu "Hekima ya Kikristo"
sanjari na Maandalizi ya Jubilee ya Miaka 50 ya Waraka kuhusu Elimu uliotolewa na
Mababa wa Mtaguso mkuu wa Pili wa Vatican, sherehe ambazo zitafanyika Mwaka 2015.
Sherehe hizi zinakwenda sanjari na kumbu kumbu ya Miaka 25 ya Waraka wa Kichungaji
kuhusu Elimu Katoliki; changamoto endelevu katika maisha na utume wa Kanisa mintarafu
Uinjilishaji Mpya na mabadiliko ya kihistoria na kitamaduni yanayoendelea kujitokeza
kwa kasi katika ulimwengu wa utandawazi.
Baba Mtakatifu Francisko akizungumza
na Wajumbe wa Baraza la Kipapa la Elimu Katoliki, Silku ya Alhamisi, tarehe 13 Februari
2014 amekazia umuhimu wa kujenga na kudumisha majadiliano katika elimu kama sehemu
ya mchakato unaopania kumwendeleza mtu mzima: kiroho na kimwili pamoja na kutambua
kwamba, kila mtu ana haki ya kupata elimu, kwa kuzingatia uhuru wake, lakini Kanisa
linatoa kipaumbele cha kwanza kwa Kristo kama chimbuko la maisha, historia na ulimwengu
katika ujumla wake. Hapa kuna haja ya kujenga na kudumisha majadiliano katika sekta
ya elimu.
Baba Mtakatifu analitaka Baraza la Kipapa la Elimu Katoliki kuhakikisha
kwamba linawaandaa wataalam na mabingwa watakaojisadaka kwa ajili ya elimu katika
ulimwengu unaobadilika kwa kasi kubwa kwa kutambua kwamba, utoaji wa elimu ni kitendo
cha upendo na urithishaji wa maisha. Walimu wawe na ujuzi wa kuweza kuwamegea ujuzi
na maarifa vijana wa kizazi kipya.
Walimu wanaotekeleza dhamana na utume wao
katika vyuo na taasisi za elimu zinazomilikiwa na kuongozwa na Kanisa Katoliki hawana
budi kuwa ni watu: wenye sifa, ujuzi na maarifa; watu wenye utajiri wa tunu msingi
za maisha ya kiroho na kiutu, kwani vijana wanatamani kuona ushuhuda wa maisha ya
walezi wao. Walimu waendelezwe katika taaluma ili waweze kuchangia kwa hali ya juu
kuhusu weledi, imani na fadhila za maisha ya kiroho zilizoko ndani mwao!
Baba
Mtakatifu anasema, kuna haja kwa Kanisa kufanya upembuzi yakinifu kuhusu mchango unaotolewa
na vyuo vikuu pamoja na taasisi za elimu ya juu zinazomilikiwa na kuendeshwa na Kanisa
Katoliki sehemu mbali mbali za dunia, kama kielelezo cha uhai wa Injili katika sayansi
na tamaduni za watu. Vyuo na Taasisi hizi zioneshe ukomavu na ujasiri wa kushindana
na wadau wengine katika sekta ya elumu kwa kujenga utamaduni wa majadiliano pamoja
na kutambua kwamba, wao wanamchango mkubwa wanaoweza kuwashirikisha pia walimwengu.
Baba
Mtakatifu anasema, sekta ya elimu ni sawa na bahari kwani haina mwisho, Kanisa limekuwa
daima mdau mkuu katika sekta ya elimu, lakini changamoto kubwa kwa sasa ni kuhakikisha
kwamba, elimu inashiriki kikamilifu katika dhamana ya Uinjilishaji Mpya kwa kuzingatia
mahitaji ya mtu mzima: kiroho na kimwili. Baba Mtakatifu Francisko anawashukuru wajumbe
wa Baraza la Kipapa la Elimu kwa mchango wao mkubwa katika maendeleo ya sekta ya elimu.