Siku ya Wapendanao! Uwanja wa Kanisa kuu la Mtakatifu Petro kutimua vumbi!
Katika Maadhimisho ya Siku ya Wapendanao, hapo Ijumaa tarehe 14 Februari 2014, Baba
Mtakatifu Francisko anatarajiwa kukutana na kuzungumza na wanandoa watarajiwa wapatao
ishirini elfu wanaojiandaa kupokea Sakramenti ya Ndoa Takatifu, kwenye Uwanja wa Kanisa
kuu la Mtakatifu Petro mjini Vatican. Hizi ni juhudi za Baraza la Kipapa la Familia
kama sehemu ya Maandalizi ya Sinodi maalum ya Maaskofu kuhusu Familia, itakayofanyika
mwezi Oktoba hapa mjini Vatican.
Baba Mtakatifu Francisko mara nyingi amewataka
wachumba na wanandoa watarajiwa kuhakikisha kwamba, wanamwilisha ndani mwao upendo
wa dhati na furaha ya maisha ya unyumba yanayojikita katika utakatifu wa maisha, daima
wakijitahidi kuiga mfano wa Familia Takatifu ya Yesu, Maria na Yosefu, pamoja na kumkaribisha
Yesu katika maisha yao ya kila siku.
Baba Mtakatifu anasema, Sakramenti ya
Ndoa ni wito mtakatifu na agano ambalo kwa njia yake mwanaume na mwanamke huunda kati
yao Jumuiya kwa maisha yao yote, kwa tabia yake ya asili liko kwa ajili ya manufaa
yao na kwa ajili ya kuzaa na kulea watoto. Hili ni agano ambalo Kristo mwenyewe amelikuza
na kulipatia hadhi ya kuwa ni kati ya Sakramenti za huduma. Wanandoa hawana sababu
ya msingi ya kutojisadaka kwa ajili ya wenzi wao, kwani kwa pamoja wanaweza kukabiliana
na changamoto mbali mbali za maisha kwa njia ya imani, matumaini na mapendo.
Baba
Mtakatifu anasema, tunu msingi za maisha ya ndoa na familia kwa vijana wa kizazi kipya
zinakabiliwa na changamoto kubwa. Hii inatokana na ukweli kwamba, vijana wengi wamemezwa
na malimwengu, ubinafsi unatawala na wakati mwingine hawana msingi thabiti wa maisha
ya kiroho na kiutu. Huu ni utamaduni wa ubinafsi unaoshindwa kuonesha upendo wa dhati
kwa mwenzi wa ndoa.
Mama Kanisa kwa kutambua changamoto hizi, anaendelea kujikita
katika maandalizi makini ya wanandoa watarajiwa pamoja na kuwapatia majiundo endelevu
baada ya kufunga ndoa, ili waweze kuwa kweli ni Kanisa dogo la nyumbani, mahali ambapo
maisha ya: sala, upendo na ukarimu yanamwilishwa katika uhalisia wake. Vyama vya kitume
Parokiani ni tunu msingi katika mchakato wa kuwasaidia wanandoa wapya kuweza kukabiliana
na changamoto za maisha ya ndoa na familia.
Mwenyeheri Yohane Paulo wa Pili
alitoa kipaumbele cha pekee kwa familia na kutaka kuwe'po na maandalizi ya kutosha
kabla ya waamini hawajafunga ndoa, ili kweli ndoa na maisha ya kifamilia yawe ni sehemu
ya hija ya utakatifu wa maisha. Papa mstaafu Benedikto wa kumi na sita aliwahi kusema
kwamba, wanandoa wanapaswa kumpatia Yesu kipaumbele cha kwanza katika maisha yao ya
kila siku, kwa wanandoa kuishi kwa ukamilifu na uaminifu ahadi zao za ndoa kadiri
ya mpango wa Mungu katika maisha yao.
Wanandoa watarajiwa wajitahidi kufahamiana
zaidi kwa kufanya tafakari ya kina na hatimaye, kufanya uamuzi wenye ukomavu, unaodumu
hadi kifo kitakapowatenganisha.