2014-02-12 09:34:38

Changamoto za maisha ya kiroho na kiutu nchini Bulgaria baada ya kuanguka kwa utawala wa Kikomunisti!


Baraza la Maaskofu Katoliki Bulgaria linaanza hija yake ya kitume mjini Vatican kuanzia tarehe 13 hadi tarehe 15 Februari 2014. Hili ni Kanisa dogo lakini lenye umuhimu wa pekee, kwani waamini wa Kanisa Katoliki nchini Bulgaria wanaunda asilimia 1.1% ya idadi ya wananchi wote wa Bulgaria.

Kuna majimbo matatu yaliyoundwa kunako mwaka 1995 na Maaskofu wake wote ni wale walionja "chungu" ya utawala wa Kikomunisti. Kanisa nchini Bulgaria linaendelea kukabiliana na changamoto za ukanimungu, kwa kujikita zaidi na zaidi katika utangazaji na ushuhuda wa Injili ya Furaha. Kanisa limejiwekea mikakati ya kuwahamasisha waamini kuhusiana na masuala ya maisha ya kiroho na kiimani baada ya kukosa uhuru wa kidini kwa miaka mingi chini ya utawala wa Kikomunisti. Familia inaendelea kukabiliana na changamoto mbali mbali kutoka ndani na nje ya familia zenyewe.

Ndoa nyingi hazina misingi thabiti ya imani, kiasi kwamba, zinaendelea kuvunjika hata katika uchanga wake. Uchumba sugu ni kati ya mambo yanayokwamisha ndoa za Kikristo anasema Askofu Christo Proykov, Rais wa Baraza la Maaskofu Katoliki Bulgaria. Vijana nchini Bulgaria baada ya kufungua macho kwa njia ya mitandao ya kijamii na njia za mawasiliano, wanapenda kuiga kila kitu kinachopita machoni mwao, hatari kubwa ni kuona kwamba, vijana hawa wanajikuta wakikabiliana na athari za kumong'onyoka kwa maadili na utu wema.

Maaskofu Katoliki Bulgaria wanaendelea kujiandaa kikamilifu kwa ajili ya Maadhimisho ya Sinodi Maalum ya Maaskofu kwa ajili ya Familia, itakayoadhimishwa mwezi Oktoba, 2014 hapa mjini Vatican. Kuna umoja na mshikamano wa kidugu na kiimani kati ya waamini wa Kanisa Katoliki na Kanisa la Kiorthodox nchini Bulgaria. Wanaendelea kuwa macho na makini kwa Mafundisho Tanzu ya Kanisa, lakini bado wanahitaji majiundo endelevu ili kuweza kukabiliana na changamoto katika maisha ya kiimani.

Waamini wanapaswa kutambua umuhimu wa Makanisa mahalia katika ujenzi wa mshikamano wa upendo na maskini na wote wanaosukumizwa pembezoni mwa Jamii kutokana na athari za myumbo wa uchumi kimataifa. Kanisa nchini Bulgaria linajielekeza zaidi katika matumizi ya njia za mawasiliano ya kijamii kwa ajili ya utangazaji wa Injili ya Furaha miongoni mwa wananchi wa Bulgaria.

Wananchi wengi wa Bulgaria wamempokea na kumkubali Papa Francisko kutokana na mtindo wake wa maisha, lakini zaidi kwa kuguswa na mahangaiko ya maskini na wote wanaosukumizwa pembezoni mwa Jamii. Maaskofu wa Bulgaria walipata fursa ya kukutana na Baba Mtakatifu mstaafu Benedikto XVI na kwa sasa wana furaha ya kukutana na Papa Francisko ili kuweza kusikiliza ushauri wake kutokana na changamoto wanazokabiliana nazo katika medani mbali mbali za maisha, ili kusonga mbele kwa imani na matumaini makubwa zaidi.

Maadhimisho ya Mwaka wa Imani yamekuwa ni fursa kubwa kwa waamini nchini Bulgaria kutambua na kuheshimu zawadi ya imani waliyoipokea kutokana na Sakramenti ya Ubatizo. Imani ni kielelezo cha maisha, ni nguvu na mwanga thabiti. Waamini wanaendelea kuchangamotishwa kuhakikisha kwamba, wanawashirikisha wengine imani yao pamoja na kuitolea ushuhuda, kwani watu wengi wanavutwa zaidi na ushuhuda wa imani tendaji, kielelezo cha wokovu, ukweli na furaha ya maisha. Kimsingi, Maadhimisho ya Mwaka wa Imani, limekuwa ni tukio ambalo limeacha chapa ya kudumu kwa waamini wa Kanisa Katoliki nchini Bulgaria.

Askofu Christo Proykov anasema kwa kutambua na kuthamini maisha ya ndoa na familia sanjari na maandalizi ya Maadhimisho ya Sinodi Maalum ya Maaskofu kwa ajili ya Familia, Baraza la Maaskofu Katoliki Bulgaria limeutangaza Mwaka 2014 kuwa ni Mwaka wa Familia. Kila siku mara baada ya Maadhimisho ya Fumbo la Ekaristi, waamini wanasali kwa ajili ya kuombea familia.

Waamini wanaendelea kufundishwa tunu msingi za maisha ya ndoa na familia kadiri ya mpango wa Mungu. Bado kuna haja ya kujikita katika majiundo makini ya waamini kuhusiana na tunu msingi za maisha ya ndoa na familia mintarafu Mafundisho ya Kanisa.







All the contents on this site are copyrighted ©.