Wahudumieni watu kwa moyo wa upendo, ili waonje huruma na upendo wa Kristo kwa waja
wake!
Waamini wanahamasishwa kuwatangazia watu Injili ya Furaha, Matumaini na Upendo, kwa
njia ya ushuhuda wa maisha yao yanayojikita katika huduma kwa maskini na wote wanaosukumizwa
pembezoni mwa Jamii. Hakuna sababu ya kutaka kuwaongoa watu kuingia katika Ukristo
kwa nguvu, bali wao wenyewe wavutwe kutokana na ukarimu na upendo unaojionesha miongoni
mwa Wakristo katika huduma na maisha adili.
Hayo yamesemwa na Kardinali Polycarp
Pengo, Askofu mkuu wa Jimbo kuu la Dar es Salaam katika ufunguzi wa Kliniki ya Upasuaji
kwa ajili ya Watoto kwenye Hospitali ya Rufaa ya Mtakatifu Gaspar, Itigi, iliyoko
Manyoni, Singida, Tanzania. Anasema, Injili ya kweli inajikita katika kumhudumia mtu
mzima: kiroho na kimwili, na hii ndio maana ya Uinjilishaji wa kina, unaogusa mahitaji
ya mtu mzima, changamoto inayofanyiwa kazi na Mama Kanisa katika mapambazuko ya Millenia
ya tatu ya Ukristo.
Kardinali Pengo amewashukuru na kuwapongeza Wamissionari
wa Damu Azizi ya Yesu nchini Tanzania kwa ushiriki wao katika kuwahudumia watanzania
katika sekta ya afya, elimu na maendeleo endelevu. Wamekuwa ni mfano wa kuigwa katika
sekta ya afya kwa kuendeleza utume ulioanzishwa na Kristo mganga mkuu wa kuwaponya
watu magonjwa yao pamoja na kuwaondolea dhambi zao.
Kardinali Pengo amewataka
wafanyakazi katika sekta ya afya kuhakikisha kwamba, wanajituma bila ya kujibakiza
kwa ajili ya kuwahudumia wagonjwa: kwa kuzingatia: maadili ya kazi, weledi, utu na
heshima ya binadamu. Wagonjwa hata katika magonjwa yao bado wanaendelea kubaki na
chapa ya sura na mfano wa Mungu katika maisha yao, hivyo wathaminiwe, waheshimiwe
na kupendwa kama Kristo mwenyewe alivyowapenda na kuwahudumia.
Amewataka wafanyakazi
katika sekta ya afya nchini Tanzania kutojihusisha na vitendo vya kuomba na kupokea
rushwa kutoka kwa wagonjwa kwani ni kinyume cha haki msingi za binadamu na kielelezo
cha kumong'onyoka kwa maadili na utu wema. Maskini na wote wanaosukumizwa pembezoni
mwa Jamii ndio wanaopaswa kupewa kipaumbele cha kwanza.
Kardinali Polycarp
Pengo alikuwa Singida kwa ajili ya kushiriki katika ufunguzi wa Kliniki ya Upasuaji
wa watoto kwenye Hospitali ya Rufaa ya Mtakatifu Gaspar, Itigi, tukio ambalo limehudhuriwa
na viongozi wa Serikali ya Tanzania. Ujumbe kutoka Vatican ulioongozwa na Professa
Giuseppe Profiti, Rais wa Hospitali ya Bambino Gesù inayomilikiwa na kuendeshwa na
Vatican, ambayo imechangia jumla ya shilingi millioni mia tano na ishirini na tano
pamoja na vifaa tiba kwa ajili ya huduma ya upasuaji kwa watoto wadogo nchini Tanzania.