2014-02-08 07:42:54

Mwenyeheri Yohane Paulo II kutangazwa kuwa Msimamizi wa Siku za Vijana Duniani


Baba Mtakatifu Francisko anawaalika vijana kujiandaa kikamilifu kwa ajili ya Maadhimisho ya Siku ya 29 ya Vijana Duniani kwa Mwaka 2014 itakayoadhimishwa katika ngazi ya Kijimbo, Jumapili ya Matawi, ambayo kwa Mwaka huu inaadhimishwa hapo tarehe 13 Aprili.

Hii ni siku ambayo Maaskofu watazungukwa na umati wa vijana kutoka katika majimbo yao ili kufanya tafakari ya kina kuhusu kauli mbiu inayoongoza Maadhimisho haya: "Heri walio maskini wa roho maana ufalme wa mbinguni ni wao". Hii ni sehemu ya muhtasari wa mafundisho makuu ya Yesu yanayopatikana katika Heri za Mlimani.

Baraza la Kipapa la Walei linasema, huu ni ujumbe ambao unatolewa kwa mara ya kwanza kwa vijana na Baba Mtakatifu Francisko tangu alipochaguliwa kuwa Khalifa wa Mtakatifu Petro. Ni mwendelezo wa changamoto ya majiundo endelevu iliyoanzishwa na Mwenyeheri Yohane Paulo II na kuendelezwa kwa ari kubwa na Baba Mtakatifu mstaafu Benedikto wa kumi na sita.

Papa Francisko bado anakumbuka ule umati wa vijana kutoka sehemu mbali mbali za dunia uliomzunguka wakati wa Maadhimisho ya Siku ya Vijana Duniani kwa Mwaka 2013 iliyofanyika mjini Rio de Janeiro. Baba Mtakatifu anaendeleza yale majadiliano ya kina kati yake na vijana yaliyoibuliwa wakati wa Maadhimisho ya Siku ya Vijana Duniani.

Kumbe, ujumbe wa Baba Mtakatifu kwa Maadhimisho ya Siku ya Vijana Kijimbo kwa Mwaka huu, ni sehemu ya maandalizi ya hija ya maisha ya kiroho, itakayofanyika katika kipindi cha miaka mitatu kuanzia sasa, kabla ya vijana hawajajimwaga kuelekea Jimbo kuu la Cracovia, Poland, kwa Maadhimisho ya Siku ya Vijana Duniani kwa Mwaka 2016.

Wachunguzi wa mambo wanasema, vijana watafunika Poland, ikizingatiwa kwamba, hizi zitakuwa ni mwendelezo wa utenzi wa sifa na shukrani kwa Mwenyezi Mungu baada ya Mwenyeheri Yohane Paulo II kutangazwa kuwa Mtakatifu. Tema zilizochaguliwa na Baba Mtakatifu katika kipindi cha miaka mitatu kutoka katika Heri za Mlimani zinazonesha jinsi ambavyo Baba Mtakatifu Francisko anavyothamini sehemu hii ya Injili kuwa ni kiini cha maisha ya Wakristo, mwaliko wa kuyamwilisha katika vipaumbele vyao vya maisha ya kila siku!

Baba Mtakatifu katika ujumbe kwa Siku ya Vijana Duniani anapenda kuwakumbusha vijana wa kizazi kipya kwamba, hii ni njia ambayo Yesu mwenyewe amewaonesha wafuasi wake, mwaliko wa kumfuasa katika maisha yao yote bila ya kujibakiza hata kidogo. Kumwilisha Heri za Mlimani kwa vijana wa kizazi kipya anasema Baba Mtakatifu ni kazi kweli kweli!

Huu nimwaliko wa kumfuasa Kristo na kushikamana naye kwa dhati, tayari kutolea ushuhuda wa mabadiliko yanayobubujika kutoka katika undani wa maisha ya mwamini. Baba Mtakatifu anawachangamotisha vijana kutokubali kupata furaha ya mpito kwa mambo ya juu juu tu, bali wahakikishe kwamba, wanajitaabisha kutafuta furaha ya kweli inayobubujika kutoka kwa Mwenyezi Mungu.

Katika ujumbe wake, Baba Mtakatifu anafafanua kwa kina na mapana maana ya umaskini wa roho kadiri ya mafundisho ya Yesu, ambaye aliuchagua mwenyewe na hatimaye kuutolea ushuhuda katika maisha na utume wake hapa duniani, mwaliko kwa vijana kuiga mfano wa maisha ya Mtakatifu Francisko, aliyekuwa tajiri wa kutupwa, lakini akaacha yote na kuukumbatia ufukara wa Kiinjili. Hii ndiyo changamoto kubwa iliyoko mbele ya vijana wa kizazi kipya na wala si maji kwa glasi!

Baba Mtakatifu Francisko anawaalika vijana kutubu na kumwongokea Yesu Kristo, huku wakijitahidi kuishi maisha yanayosimikwa katika kiasi, wakitafuta mambo msingi katika maisha yao pamoja na kujenga mshikamano wa upendo na maskini pamoja na wote wanaosukumizwa pembezoni mwa Jamii. Maskini ni sehemu ya Fumbo la Mwili wa Kristo linaloendelea kuteseka, mwaliko kwa kila mwamini kuhakikisha kwamba, anaguswa na umaskini, taabu na mahangaiko ya jirani zake; kwa njia hii vijana wanaweza kuwa kweli ni walimu wa maisha, kwa kuwamegea wengine utajiri wa maisha ya kiroho na kiutu unaobubujika kutoka katika undani wa maisha yao.

Baba Mtakatifu Francisko anasema, kuna uhusiano mkubwa kati ya tema iliyoongoza Maadhimisho ya Siku ya Vijana Duniani kwa Mwaka 2013 huko Rio de Janeiro "Basi, enendeni, mkawafanye mataifa yote kuwa wanafunzi..." na kauli mbiu ya mwaka huu yaani, "Heri walio maskini wa roho maana ufalme wa mbinguni ni wao". Ufukara wa Kiinjili ni muhimu sana katika ujenzi wa ufalme wa Mungu sehemu mbali mbali za dunia. Ni ufukara unaojionesha katika hali ya kawaida pasi na makuu, kiasi cha kuweza kuwa ni chachu ya Uinjilishaji Mpya.

Baba Mtakatifu anawakumbusha vijana wa kizazi kipya kwamba, hapo tarehe 22 Aprili 2014, Kanisa litafanya kumbu kumbu ya Miaka 30 tangu Msalaba wa Jubilee ya Mwaka wa Ukombozi ulipoanza kutembezwa sehemu mbali mbali za dunia. Hizi zilikuwa ni juhudi za Mwenyeheri Yohane Paulo wa Pili kwa ajili ya Kanisa, tangu wakati ule, Msalaba umekuwa ni sehemu ya hija ya maisha ya vijana wa kizazi kipya.

Kwa hakika, baada ya Mwenyeheri Yohane Paulo II kutangazwa kuwa Mtakatifu, Kanisa litaendelea kumshukuru Mungu kwa kumtangaza rasmi kuwa ni Msimamizi wa Maadhimisho ya Siku za Vijana Duniani. Mwenyeheri Yohane Paulo II alikuwa ni muasisi na mhamasishaji mkuu wa Siku za Vijana Duniani, hadi leo hii, tukio hili linaendelea kuwa na mvuto na mashiko makubwa katika maisha na utume wa Mama Kanisa miongoni mwa vijana, kwa kutambua kwamba, vijana ni jeuri na matumaini ya Kanisa kwa sasa na kwa siku za usoni!

Na Padre Richard A. Mjigwa, C.PP.S.
Idhaa ya Kiswahili ya Radio Vatican.







All the contents on this site are copyrighted ©.