2014-02-08 09:16:49

Makanisa yanapenda kujielekeza katika ujenzi wa misingi ya haki na amani duniani


Kamati kuu ya Baraza la Makanisa Ulimwenguni katika mkutano wake ulioanza hapo tarehe 7 Februari na unatarajiwa kufungwa rasmi tarehe 12 Februari 2014, pamoja na mambo mengine unajadili mikakati na utekelezaji wa maamuzi yaliyofikiwa kwenye Mkutano mkuu wa kumi wa Baraza la Makanisa Ulimwenguni uliofanyika mjini Busan, Korea ya Kusini Mwaka 2013. Kamati kuu inapenda kujielekeza zaidi katika hija ya ujenzi wa misingi ya haki na amani duniani.

Wajumbe wa mkutano mkuu wa Baraza la Makanisa Ulimwenguni, walikubaliana kwa pamoja kushirikiana kwa kufanya hija ya pamoja na waamini pamoja na watu wenye mapenzi mema katika utekelezaji wa maazimio na mikakati iliyoainishwa wakati wa maadhimisho ya mkutano mkuu wa Baraza la Makanisa Ulimwenguni.

Dr. Olav Fyske Tveit, Katibu mkuu wa Baraza la Makanisa Ulimwenguni anasema hii ni hija ya maisha ya kiroho na kiutu, itakayowawezesha waamini kujikita katika ukweli kwa ajili yao na jirani zao, tayari kujifunua ili kuona utashi wa Mungu unavyowaongoza katika ulimwengu mamboleo.

Ni changamoto kwa Makanisa kushikamana, ili kufahamu mambo msingi yanayopaswa kubadilishwa, kwa kuangalia mbinu mkakati na majukumu yatakayojitokeza, ili waweze kuyatekeleza kwa pamoja! Baraza la Makanisa Ulimwenguni linataka kuwekeza zaidi katika misingi ya haki hususan katika maeneo ambamo bado mtutu wa bunduki unaendelea kusikika hasa nchini: Syria na Sudan ya Kusini na Jamhuri ya Watu wa Afrika ya Kati. Bado kuna pengo kubwa kati ya maskini na matajiri duniani, jambo linalohitaji kujenga mshikamano wa upendo kwa kuguswa na matatizo ya watu wengine duniani.

Kuna masuala kama vile: Umoja wa Wakristo, utume wa Makanisa, Ekolojia, Mazingira, misingi ya uchumi wa haki na haki msingi za binadamu, yanapaswa kuchambuliwa, kufafanuliwa na kuwekewa mikakati ya utekelezaji wake kwa kutumia Makanisa wanachama!

Baraza la Makanisa Ulimwenguni linasema, Waraka wa Kitume wa Baba Mtakatifu Francisko: Injili ya Furaha ni changamoto kwa Baraza hili kushirikiana kwa karibu na Kanisa Katoliki katika utekelezaji wa mikakati ya kichungaji iliyoainishwa na Papa Francisko katika dhamana ya utangazaji na ushuhuda wa Injili ya Furaha.







All the contents on this site are copyrighted ©.