Simameni kidete kupinga biashara haramu ya binadamu!
Tarehe 8 Februari, kila mwaka, Mama Kanisa anaadhimisha Kumbu kumbu ya Mtakatifu Josephina
Bakhita, Mtawa kutoka Sudan aliyekumbukana na madhulumu na nyanyaso kiasi cha kuuzwa
utumwani. Akaonja huruma na upendo wa Mungu na kubahatika kukombolewa kutoka utumwani.
Katika hija ya
maisha yake, akabahatika kuwa Mtawa wa Shirika la Mabinti wa Upendo wa Mtakatifu Madgalena
wa Canossa. Baraza la Maaskofu Katoliki Marekani, linatumia tarehe 8 Februari kuhamasisha
watu kuhusu madhara ya biashara ya binadamu inayoendelea kushika kasi ya ajabu duniani
kutokana na ubinafsi pamoja na uchu wa mali na utajiri wa haraka haraka. Waamini na
watu wenye mapenzi mema, wanahamasishwa kuangalia madhara yanayotokana na biashara
haramu ya binadamu kwani vitendo hivi ni kinyume cha ubinadamu! Waamini na wananchi
wenye mapenzi mema wanapaswa kusimama kidete kulinda na kutetea utu na heshima ya
binadamu, aliyeumbwa kwa sura na mfano wa Mungu na kukombolewa kwa Damu Azizi ya Yesu
Kristo.