Bunge Maalum la Katiba kuanza kutimua vumbi hapo tarehe 18 Februari 2014
Hotuba ya Dr. Jakaya Mrisho Kikwete, Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania kwenye
kikao cha Baraza la Vyama vya Siasa, ukumbi wa Mikutano wa Kimataifa wa Mwalimu Nyerere,
tarehe 6 Februari, 2014, Dar es salaam
Ndugu Peter Mziray, Mwenyekiti wa Baraza
la Vyama vya Siasa; Ndugu Vuai Ali Vuai, Makamu Mwenyekiti wa Baraza la Vyama vya
Siasa; Mheshimiwa Jaji Francis Mutungi, Msajili wa Vyama vya Siasa; Ndugu Wenyeviti
wa Vyama vya Siasa; Ndugu Wajumbe wa Baraza la Vyama Siasa; Wageni Waalikwa; Mabibi
na Mabwana;
Utangulizi Nakushukuru ndugu Peter Mziray, Mwenyekiti
wa Baraza la Vyama vya Siasa na viongozi wenzako kwa kunishirikisha kwenye kikao hiki
maalum cha Baraza na kwa maelezo mazuri ya utangulizi. Tutayatafakari ya kufanyika
yafanyike. Nawapongeza kwa uamuzi wenu wa busara wa kuzungumzia nafasi ya vyama vya
siasa katika Bunge Maalum la kutunga Katiba. Jambo hili ni muhimu kwa uhai, maendeleo
na ustawi wa nchi yetu na watu wake. Mmeonesha moyo wa uzalendo na ukomavu wa kisiasa
wa hali ya juu.
Tangu Baraza hili la vyama vya siasa lizinduliwe mwezi Mei,
2010, nimekuwa nikifuatilia kwa karibu shughuli zake na jinsi linavyofanya kazi.
Kwa kweli nimeridhishwa na hatua mliyopiga. Ndiyo maana mliponiita sikusita kuja.
Nawaahidi kuwa nitaendelea kufanya hivyo katika siku zijazo ili mradi tu nafasi iwepo.
Serikali
Kuimarisha Uwanja wa Siasa
Ndugu Wajumbe; Mtakubaliana nami kuwa Tanzania
imepiga hatua kubwa katika kujenga na kuendeleza demokrasia ya vyama vingi na ushindani
wa kisiasa. Kuwepo kwa vyama 21 vyenye usajili wa kudumu vilivyo huru kuendesha shughuli
zao na Baraza la Vyama vya Siasa ni kielelezo tosha cha ukweli huu. Wazo la kuwa
na Baraza hili liliibuka wakati wa mchakato wa kutatua mgogoro wa kisiasa wa Zanzibar
uliozuka baada ya Uchaguzi Mkuu wa mwaka 2000. Kamati ya Pamoja ya Mwafaka iliyokuwa
na wajumbe kutoka CCM na CUF iliundwa ili kutafuta suluhu ya mgogoro ule. Mojawapo
ya mambo ambayo Kamati hiyo ilipendekeza ni kuundwa kwa chombo kitachowezesha viongozi
wa vyama vya siasa kukutana mara kwa mara kujadili masuala ya kisiasa ili kuepusha
migogoro ya kisiasa.
Baada ya Baraza kuundwa, mwaka 2009, Serikali ikaona
haja ya kupanua wigo wa ushiriki na kukifanya chombo hiki kuendesha kazi zake kwa
mujibu wa Sheria. Matokeo yake Wenyeviti wa vyama vyote vya siasa wakajumuishwa kufuatia
marekebisho ya Sheria ya Vyama vya Siasa yaliyofanyika mwaka 2009. Baraza la Vyama
vya Siasa likatambulika kisheria na majukumu yake kuorodheshwa katika Sheria husika.
Ofisi ya Msajili wa Vyama vya Siasa ikapewa jukumu la kuratibu na kugharimia shughuli
za Baraza la Vyama vya Siasa.
Mabibi na Mabwana; Nimeamua kueleza
chimbuko la Baraza la Vyama vya Siasa, ili Wajumbe wa Baraza na watu wote wanaonisikiliza
wajue kwamba Baraza hili limetokeaje kuwepo na lina nafasi gani katika jamii na siasa
za Tanzania. Ni chombo kilichotokana na mafunzo tuliyopata katika migogoro ya kisiasa
huko nyuma. Baraza hili ndicho chombo ambacho kikitumiwa vizuri na vyama vya siasa
matatizo na malalamiko yao na masuala mengine ya kisiasa yana mahali pa kujadiliwa
na kupatiwa ufumbuzi. Aidha, ni jukwaa linalotoa fursa kwa vyama vya siasa kuzungumzia
masuala mbalimbali yenye maslahi kwa taifa na kukubaliana kuhusu nini vyama vyenyewe
vifanye au vishauri yafanyike na mamlaka husika. Ushauri unaotolewa unawasilishwa
Serikalini kupitia Ofisi ya Msajili wa Vyama vya Siasa ambayo ndio Sekretarieti ya
Baraza hili.
Hakuna chombo kingine zaidi ya Baraza hili kinachowakutanisha
viongozi wote wa kitaifa wa vyama vya siasa kujadili masuala ya kisiasa yenye maslahi
ya kitaifa. Kwa kuzingatia nafasi yake na majukumu ya Baraza hili, nawasihi viongozi
wenzangu hususan Wenyeviti wa vyama vya siasa tulipe uzito na tulitumie ipasavyo.
Nawaomba tuwe tunashiriki kwa ukamilifu katika vikao na shughuli za Baraza.
Natambua
kwamba kwa vile Baraza linajumuisha vyama vyote hata Mwenyekiti wa Chama kidogo anaweza
kuongoza Baraza inaweza kutokupendeza kwa vyama vikubwa. Si jambo la ajabu wala si
jambo baya ndiyo maana na faida ya demokrasia. Wale wanaotoka vyama vikubwa wasichukie,
wakifanya hivyo wanakiuka kanuni moja ya msingi ya uongozi nayo ni “kiongozi mzuri
pia huwa ni mfuasi mzuri”. Hata mdogo analo la maana la kuwanufaisha wote wadogo
na wakubwa. Naamini Baraza likitumika vizuri litatunufaisha wote: vyama vyote, nchi
yetu na wananchi wote.
Mimi na Mheshimiwa Ali Mohamed Shein, Rais wa Zanzibar
na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi kwa nafasi zetu hatushiriki moja kwa moja katika
mikutano ya Baraza hili. Pamoja na hilo bado tunalitambua, tunalithamini na tunayachukulia
maamuzi ya Baraza hili kwa uzito unaostahili. Ndiyo maana Chama changu kimemteua
kiongozi mzito anayenifuata kwa madaraka yaani Makamu Mwenyekiti, ndugu Philip Mangula
kuwa Mjumbe wa Baraza. Kutoka Zanzibar tumemteua Naibu Katibu Mkuu wa CCM, Ndugu Vuai
Ali Vuai.
Kwa kweli ingependeza sana kama viongozi wa vyama vingine nao wangetoa
uzito unaostahili kwa Baraza hili. Natoa rai kwa viongozi wakuu wa vyama vya siasa,
hususan wenyeviti kwa wao wenyewe kuwa Wajumbe wa Baraza hili adhimu ili kulipa uzito
na hadhi stahiki. Baraza hili lilianzishwa kwa ajili yetu, kujadili masuala ya kuimarisha
na kuboresha uwanja wa siasa nchini na kuweka mazingira na uwanja ulio huru na sawa.
Kusudi la kutaka wenyeviti wote wa kitaifa wa vyama vya siasa wawe wajumbe
wa Baraza ni kuhakikisha kuwa Baraza linakuwa na uwakilishi wa watu wenye mamlaka
kamili kufanya maamuzi kwa niaba ya vyama vyao. Ni muhimu sote tuone hoja hiyo na
kuitumia fursa inayotolewa na Baraza. Napenda kuwahakikishia ndugu wajumbe kuwa Serikali
itaendelea kusikiliza na kuheshimu ushauri wa Baraza hili kwani ni chombo muhimu sana
kwa mustakabali wa ustawi wa siasa na maendeleo ya nchi yetu.
Ndugu Wajumbe
wa Baraza la Vyama vya Siasa; Jambo lingine muhimu tunaloendelea kufanya ni kuimarisha
Ofisi ya Msajili wa Vyama vya Siasa ili iweze kumudu vyema majukumu yake. Mwaka
jana (2013) niliidhinisha muundo mpya wa Ofisi ya Msajili wa Vyama vya Siasa wenye
vitengo vingi kuliko ilivyokuwa kabla ya hapo. Muundo mpya unaoongozwa na watumishi
wenye taaluma nyingine mbalimbali badala ya kutegemea wanasheria peke yake. Changamoto
zinaongezeka na mazingira ya kufanya kazi yanabadilika, hivyo Ofisi ya Msajili wa
Vyama vya Siasa itafaidika na kuwa na watumishi wa kada nyingine kama vile wa sosholojia,
sayansi ya siasa na kadhalika.
Ili kuhakikisha ufanisi zaidi, Serikali imedhamiria
kuongeza bajeti ya ofisi ya Msajili wa Vyama vya Siasa katika mwaka ujao wa fedha.
Bila ya kufanya hivyo tutakuwa hatukufanya kitu cha maana. Ofisi haitaweza kutimiza
wajibu wake. Kwa kweli itakuwa ni kuwaonea kuwadai wafanye zaidi.
Ndugu Mwenyekiti
na Wajumbe wa Baraza la Vyama vya Siasa; Nimeelezwa na Msajili wa Vyama vya Siasa
kuwa, jambo moja linaloikwaza ofisi yake ili waweze kutimiza ipasavyo jukumu lao la
kuwa mlezi wa vyama vya siasa nchini ni mfumo wa Sheria ya Vyama vya Siasa. Nimeelezwa
kuwa Sheria hii imeweka adhabu moja tu ambayo ni kukifuta Chama kinachofanya makosa
yaliyoainishwa katika Sheria badala ya kutafuta taratibu za kurekebisha. Kwa maoni
yake Sheria haitoi nafasi ya kutosha ya kuvilea vyama vikue, vikomae na vijiepushe
na migogoro ya kisiasa ndani ya vyama na ndani ya jamii. Kwa sababu hiyo, inamfanya
Msajili aonekane kuwa ni mtu wa kutoa vitisho vya kufungia vyama. Kwa maoni yake
hatuna budi kuangalia sheria hiyo upya ili iweze kushughulikia changamoto hizo.
Naiona
hoja ya Msajili na nampongeza sana kwa kuliona jambo hilo. Leteni mapendekezo yenu
tuyatazame ili hatua zipasazo zichukuliwe. Pamoja na hayo usisubiri sheria. Mlezi
hutoa ushauri na kusaidia kupata ufumbuzi wa mambo mbalimbali yanayowatatiza viongozi
na wanachama wa vyama vya siasa. Usisite kututembelea mara kwa mara kuzungumza nasi
na kutushauri unavyoona inafaa. Itasaidia sana wakati tunasubiri Sheria kufanyiwa
marekebisho. Nafurahi kwamba kazi hiyo unaifanya. Tafadhali endelea. Pia usisite
kutuita wote au mmoja mmoja unapoona inafaa kufanya hivyo.
Nimeambiwa mchakato
wa kupitia upya Sheria hiyo na ile ya Gharama za Uchaguzi umeanzishwa na Ofisi ya
Msajili wa Vyama vya Siasa. Bila ya shaka marekebisho ya Sheria ya Vyama yatasaidia
kuboresha uratibu wa shughuli za kisiasa hapa nchini bila kuingilia uhuru wa vyama
vya siasa. Vilevile marekebisho ya Sheria ya Gharama za Uchaguzi yatasaidia kuhakikisha
wananchi wetu wanachagua viongozi kwa kuzingatia uwezo wao, mwenendo na ubora wa sera
za vyama vyao na si uwezo wao wa kifedha. Nimefurahi na nimefarijika sana na hatua
hiyo. Ongezeni kasi ya kukamilisha zoezi hilo.
Ndugu Washiriki;
Naomba kurudia tena kusema kuwa tunafanya hayo yote ili kuimarisha demokrasia ya vyama
vingi na ushindani wa kisiasa nchini. Kwetu sisi Serikalini, vyama vya siasa ni wadau
muhimu wa maendeleo ya nchi yetu na watu wake. Kwa maana hiyo tunapenda vyama viwe
na uwezo wa kutekeleza wajibu huo. Kinyume chake, yaani vyama vinaweza kugeuka na
kuwa wakala wa kurudisha nyuma maendeleo. Hii haikubaliki, itashangaza na kusikitisha.
Mada
ya Kikao
Ndugu Mwenyekiti; Kama wote mnavyofahamu, nchi yetu
ipo katika mchakato wa kuandika Katiba Mpya. Hatua inayofuatia sasa ni Bunge Maalum
la Katiba kukutana na kujadili Rasimu ya Pili na kuamua ipasavyo. Kazi ya uteuzi
wa Wajumbe 201 wa kuungana na Wabunge na Wawakilishi katika Bunge hilo imekamilika
na kesho watatangazwa. Ilikuwa kazi ngumu sana. Watu wengi wazuri walipendekezwa
hivyo hujui umchague nani na umuache nani. Kwa vile hatuwezi kuwapeleka wote basi
tumewateua hao 201 na kuwaacha maelfu ya watu wazuri. Kama wote wanaofaa wangechukuliwa
nchi ingenufaika sana. Lakini hatuwezi kuwa na Bunge la watu 5,000 hata China haifanyi
hivyo. Ilikuwa hapana budi kuchagua baadhi yao tu. Kwa ajili hiyo nawasihi wale
wote wasioteuliwa wasisononeke. Hawajapungukiwa sifa ila nafasi hazitoshi.
Ndugu
Wajumbe; Wiki iliyopita nilitembelea ukumbi wa Bunge Dodoma na kujionea mwenyewe
maandalizi ya Ukumbi na vifaa unavyoendelea. Mambo yanakwenda vizuri. Nimeelezwa
kuwa ifikapo tarehe 10 Februari, 2014 kila kitu kitakuwa tayari na majaribio kufanywa
ya vifaa vilivyofungwa. Nimeona tujipe wiki moja baada ya hapo ili tuweze kurekebisha
panapostahili. Kwa ajili hiyo nimekubaliana na Rais wa Zanzibar niangalie uwezekano
wa kuliitisha Bunge Maalum tarehe 18 Februari, 2014. Tutaitangaza rasmi siku hiyo
kupitia gazeti la Serikali.
Bunge la Katiba ndilo lenye mamlaka ya kutunga
Katiba mpya ya nchi yetu. Hatua zote zilizopita ni za kutoa mapendekezo jukumu ambalo
Tume ya Mabadiliko ya Katiba imelikamilisha vyema. Ipo Rasimu ya Katiba itakayofikishwa
kwenye Bunge Maalum kujadiliwa na kufanyiwa uamuzi. Ingekuwa Bunge la kawaida au
Baraza la Wawakilishi, Rasimu ya Katiba ndiyo Muswada wa Sheria utakaofikishwa Bungeni
na kwenye Baraza.
Wajumbe wa Bunge hilo watambue kuwa wana dhamana isiyokuwa
na mfano wake kwa nchi yetu na Watanzania wenzao kwa jumla. Wanalo jukumu la kuwapatia
Katiba nzuri itakayodumu kwa zaidi ya miaka 50 ijayo. Katiba itakayoimarisha Muungano
badala ya kuudhoofisha. Katiba itakayodumisha umoja, amani na utulivu nchini badala
ya kuvuruga. Vilevile Katiba itakayoweka mazingira mazuri ya kisiasa, kijamii na
kiuchumi na kuongeza kasi ya maendeleo ya nchi yetu na ustawi wa watu wake kwa miaka
mingi ijayo. Ili haya yafanyike ni vyema Wajumbe wajue vyema kinachopendekezwa, wapambanue
kinachofaa na kisichofaa, na kubwa zaidi, watangulize maslahi ya taifa mbele kuliko
maslahi yao binafsi au ya makundi yao.
Ndugu Mwenyekiti na Wajumbe wa Baraza
la Vyama vya Siasa; Mabibi na Mabwana; Vyama vya siasa vina nafasi
ya pekee katika majadiliano ya Bunge Maalum la Katiba na katika mchakato mzima wa
kutunga Katiba mpya. Mafanikio ya mchakato huu yatategemea sana kauli, mwenendo na
matendo ya vyama vya siasa. Ukweli ni kwamba vitendo na kauli za viongozi, wanachama
na wafuasi wa vyama vya siasa ndivyo vitakavyojenga au kubomoa, na ndivyo vitakavyowezesha
au kukwamisha mchakato huu.
Mimi nataka vyama vijenge na kuwezesha mchakato
ufanikiwe na Katiba mpya ipatikane kwa wakati tunaoutarajia sote. Yaani tufanye uchaguzi
wa Serikali za Mitaa na Uchaguzi Mkuu 2015 tukiwa na Katiba Mpya. Mimi naamini kwa
dhati ya moyo wangu kuwa vyama vya siasa vikiamua Katiba ipatikane, itapatikana.
Hivyo basi, kama vyama vya siasa vitaamua kishirikiana kwa dhati, na kwa nia njema
tutapata Katiba mpya bila kelele wala mikwaruzo. Kama vyama vya siasa vitatambua
kuwa tunatengeneza jambo la kutunufaisha wote, yaani nchi yetu na watu wake na siyo
maslahi binafsi ya vyama vyao itakuwa hatua kubwa ya mwanzo ya kufanya kazi ya Bunge
kuwa rahisi. Pia kama vyama vitakubali kuongozwa kwa nguvu ya hoja alizotoa Mjumbe
na siyo Mjumbe anatokea Chama gani au kundi gani, tutapata Katiba yenye maslahi kwa
taifa letu. Tutapata Katiba itakayoridhiwa na wananchi bila ya taabu.
Ninaposema
hayo sina maana kuwa vyama vya siasa au Wajumbe wanaotokana na vyama wasiende Bungeni
na maoni yao au na misimamo ya vyama vyao. La hasha! Nikifiria hivyo sitakuwa mkweli
kwangu mwenyewe. Nitakuwa najidanganya. Ninachosema ni kwamba, pamoja na kuwa na
maoni, mwongozo na misimamo ya vyama vyenu, lazima muwe na unyumbufu wa mawazo kwa
kiasi fulani ili mpate nafasi ya kusikiliza hoja za wengine zinazotofautiana na zenu,
kuzivumilia na kuzikubali pale ambapo kuna mantiki. Kwa lugha ya Kiingereza natoa
wito wa “flexibility”. Muungwana hukubali mawazo bora na yenye ukweli ya watu wengine.
Hata wengine nao wanaweza kuwa na mawazo bora kuliko yako. Muungwana ni yule anaekiri
ukweli huo na yuko tayari kupokea mawazo bora ya watu wengine hata kama watu hao hawapendi.
Kama tutakwenda kwenye Bunge na azimio la kupinga kila wazo litakalosemwa na mtu fulani,
hatutafikia kupata Katiba mpya. Haitawezekana.
Ndugu Mwenyekiti wa Baraza
la Vyama vya Siasa; Ndugu Wajumbe; Mtakubaliana nami kuwa Baraza hili na hasa
ninyi viongozi mliokusanyika hapa leo mnayo dhamana na jukumu la kipekee la kuipatia
nchi yetu Katiba nzuri yenye maslahi kwa nchi yetu na inayojali maslahi ya watu na
kukubalika na watu wote. Katiba ambayo itakapotangazwa watu waseme naam, hii ni Katiba
inayojali maslahi ya nchi zetu mbili zilizoungana na kuwa nchi moja miaka 50 iliyopita.
Katiba inayojali maslahi ya raia wa Tanzania ndani ya Muungano na ule upande wa Muungano
anakoishi au unakotoka kwa asili yake au historia yake.
Ni kwa kutambua umuhimu
huu wa vyama vya siasa ndiyo maana nilitoa wito kwa vyama vya siasa kukutana na kuzungumza
miongoni mwenu. Ningependa mzungumze kuhusu namna bora ya kujadili rasimu ili mwishowe
tupate Katiba nzuri. Ningependa mzungumze jinsi vyama vya siasa vitakavyoshirikiana
hasa kutafuta ufumbuzi wakati majadiliano yanapokuwa magumu kwa baadhi ya mambo.
Si
vyema mkadhani jawabu ni kushindana mpaka mwenye nguvu ashinde. Mnaweza kushindwa
wote. Na mkishindwa, mjue sote tumeshindwa na nchi imekwama. Msikubali kuifikisha
nchi hapo. Tuzidi kumuomba Mola atusaidie tusifike hapo. Lakini, Mwenyezi Mungu
husaidia wanaojisaidia. Na sisi tutengeneze namna bora ya kujisaidia ili Mungu akitia
mkono wake mambo yanajipa. Lililoonekana kuwa zito linakuwa jepesi kama kanda la
usufi.
Ndugu Mwenyekiti wa Baraza la Vyama vya Siasa; Nawaamini nyote mliopo
hapa mnaweza kutengeneza mfumo huo na taratibu hizo. Sina majibu wala maelekezo ya
mfumo huo ni upi. Nimekuja kutoa rai. Nimekuja kutoa maombi. Majibu mnayo ninyi.
Mimi nasubiri jibu jema kama wanavyosubiri Watanzania wengine. Nawaomba myatafakari
ninayosema na myape uzito unaostahili.
Mwisho
Narudia kuwashukuru
Mwenyekiti wa Baraza la Vyama vya Siasa na Msajili wa Vyama vya Siasa, kwa kunialika
kuja kuongea na viongozi wa vyama vya siasa kupitia Baraza hili. Ni matumaini yangu
kuwa, miaka ishirini na mbili tangu mfumo wa vyama vingi uanzishwe tena hapa nchini
kwetu mwaka 1992, vyama vya siasa vimekomaa na vinaelewa nafasi na umuhimu wake katika
jamii. Hivyo basi, tutegemee matokeo mema katika mkutano wenu huu wa kihistoria na
mchakato utakaozaa matunda mema katika Bunge Maalum la Katiba.
Kabla ya kumaliza
napenda kurudia kuwahakikishia kuwa mimi na Serikali ninayoiongoza tutaendeleza ushirikiano
wetu na Baraza. Tuko tayari kuitikia wito wa kuja kuongea nanyi wakati wowote. Baada
ya kuyasema maneno yangu mengi, nawatakia kila heri katika Mkutano wenu. Mungu
Ibariki Afrika! Mungu Ibariki Tanzania! Ahsanteni kwa kunisikiliza.