2014-02-06 10:34:33

Maaskofu wanashirikishana Injili ya Furaha pamoja na kuangalia mbinu mkakati wa kudumisha haki na amani duniani!


Maaskofu kutoka Afrika, Asia, Amerika ya Kusini na Ulaya, ni kati ya mahujaji waliokuwa kwenye Uwanja wa Kanisa kuu la Mtakatifu Petro mjini Vatican, Jumatano tarehe 5 Februari 2014, kusikiliza kwa makini Katekesi ya Baba Mtakatifu Francisko kuhusu umuhimu wa Sakramenti ya Ekaristi Takatifu katika maisha na utume wa Kanisa. Maaskofu hawa wako mjini Roma ili kushiriki katika Maadhimisho ya Miaka 46 tangu Jumuiya ya Mtakatifu Egidio yenye makao makuu yake mjini Roma ilipoanzishwa.

Mkutano huu wa kumi na sita unaongozwa na kauli mbiu "Injili ya Furaha", tema inayotoa mwanya kwa Maaskofu kubadilishana uzoefu, mang'amuzi na vipaumbele vyao katika mchakato wa kuwatangazia watu Injili ya Furaha ili kuwajengea matumaini mapya yanayobubujika kutoka kwa Kristo na Kanisa lake.

Maaskofu hawa wanatumia fursa hii kushirikishana uzoefu na mang'amuzi yao katika: kutakatifuza, kufundisha na kuwaongoza watu wa Mungu. Mama Kanisa anaendelea kuwahamasisha Maaskofu kutoa kipaumbele cha kwanza kwa maskini na wote wanaosukumizwa pembezoni mwa Jamii.

Baadhi ya Maaskofu ni wale wanaotoka katika maeneo ambayo yameguswa kwa namna ya pekee na mashambulizi ya kigaidi, vita na kinzani za kijamii na kisiasa kama vile: Nigeria, DRC, Uganda, Syria na maeneo mengine ambako bado damu ya watu wasiokuwa na hatia inaendelea kumwagika.

Maaskofu katika mkutano huu ulioandaliwa na Jumuiya ya Mtakatifu Egidio wanajadili pamoja na mambo mengine umuhimu wa kusimama kidete kulinda na kudumisha misingi ya haki, amani na udugu pamoja na kuhakikisha kwamba, wanatafuta mbinu mkakati wa kutatua vita na migogoro inayoendelea kufuka moshi sehemu mbali mbali za dunia.

Mkutano huu unawajumuisha pia Maaskofu kutoka Kanisa la Kiorthodox na Kianglikani. Katika hotuba yake ya ufunguzi, siku ya Jumatano tarehe 5 Februari, 2014 Professa Andrea Riccardi amezungumzia kuhusu changamoto za kichungaji zinazoendelea kutolewa na Baba Mtakatifu Francisko katika maisha na utume wa Kanisa.

Alhamisi tarehe 6 Februari 2014, Maaskofu watahudhuria Ibada ya Misa Takatifu kwenye Kanisa kuu la Mtakatifu Yohane wa Laterano kama sehemu ya Maadhimisho ya Miaka 46 tangu Jumuiya ya Mtakatifu Egidio ilipoanzishwa. Maaskofu pia wamepata nafasi ya kutembelea Makatacombe ya Ardeatine yaliyoko mjini Roma.







All the contents on this site are copyrighted ©.