Kliniki ya Upasuaji wa Watoto Katika Hospitali ya Rufaa ya Mtakatifu Gaspar, Itigi,
kufunguliwa rasmi na Kardinal Pengo!
Kardinali Polycarp Pengo, Askofu mkuu wa Jimbo kuu la Dar es Salaam, hapo tarehe 7
Februari 2014 anatarajia kufungua Kliniki ya Upasuaji wa Watoto Wadogo katika Hospitali
ya Rufaa ya Mtakatifu Gaspar, Itigi, Singida, Tanzania.
Tukio hili
linatarajiwa kuhudhuriwa pia na Professa Giuseppe Profit, Rais wa Hospitali ya Bambino
Gesù inayomilikiwa na kuendeshwa na Vatican mjini Roma pamoja na viongozi mbali mbali
kutoka Serikali ya Tanzania.
Kliniki ya Upasuaji kwa Watoto kutoka Kanda ya
Kati nchini Tanzania ni kielelezo cha ushirikiano wa huduma ya upendo na mshikamano
kati ya Hospitali ya Bambino Gesù na Hospitali ya Mtakatifu Gaspar Itigi inayoendeshwa
na kusimamiwa na Shirika la Wamissionari wa Damu Azizi ya Yesu.
Katika mahojiano
maalum na Padre Seraphine Lesiriam, Mkurugenzi wa Hospitali ya Rufaa ya Mtakatifu
Gaspar, Itigi, anabainisha kwamba, Kliniki hii imeanzishwa ili kukabiliana na changamoto
za magonjwa mbali mbali yanayowakabili watoto hususan kutoka Kanda ya Kati nchini
Tanzania; magonjwa ambayo yanahitaji matibabu maalum pamoja na kupunguza gharama za
matibabu kwa watoto ambao walikuwa wanalazimika kupelekwa nje ya nchi kwa ajili ya
kupata matibabu zaidi.
Tangu Mwaka 2005 Hospitali ya bambino Gesù ilianzisha
uhusiano wa tiba na Hospitali ya Mtakatifu Gaspar kwa ajili ya kuwasaidia watoto waliokuwa
na magonjwa ya moyo. Kuanzia mwaka 2006 hadi kufikia Mwaka 2012 jumla ya watoto 13
wamenufaika na huduma ya upasuaji wa moyo iliyokuwa inatolewa na Hospitali ya Bambino
Gesù. Mtoto mmoja amepewa huduma ya marekebisho ya ngozi. Kwa bahati mbaya katika
kipindi hiki, mtoto mmoja alifariki dunia, hali yake ilikuwa mbaya tangu alipowasili
nchini Italia kwa ajili ya kufanyiwa Operesheni ya moyo.
Padre Serafini anasema,
Hispitali ya Bambino Gesù imechangia kiasi cha Euro 250, 000; sawa na shilingi za
kitanzania Millioni 525 kwa ajili ya ujenzi na ukarabati wa majengo yatakayotumiwa
na Kliniki ya Upasuaji kwa ajili ya Watoto, Hospitali ya Mtakatifu Gaspar. Lengo ni
kuwa na uhakika wa huduma za kibingwa za upasuaji kwa ajili ya watoto badala ya kulazimika
kuwasafirisha kwenda Italia kwa matibabu zaidi, kama ilivyokuwa hapo awali.
Hopistali
ya Rufaa ya Mtakatifu Gaspar kwa sasa imekamilisha huduma za tiba zifuatazo kwa ajili
ya watoto wagonjwa: Upasuaji wa moyo; meno na macho; huduma ya tiba kwa njia ya mtandao,
yaani “tele-medicine”. Idara ya wagonjwa mahututi pamoja na kitengo cha elimu na burudani
kwa watoto wanaolazwa Hospitalini.
Hospitali ya Mtakatifu Gaspar ilizinduliwa
rasmi hapo tarehe 15 Mei 1989 na Rais wa Awamu ya Pili Mzee Ali Hassan Mwinyi. Tarehe
12 Oktoba 2010 ikapandishwa hadhi na kuwa ni Hospitali ya Rufaa ngazi ya Mkoa. Kwa
sasa ina uwezo wa kulaza wagonjwa 320 kwa wakati mmoja.
Takwimu zinaonesha
kwamba, Idadi ya wagonjwa waliohudumiwa Hospitalini hapo katika kipindi cha Mwaka
2013ni wagonjwa wa nje chini ya umri wa miaka mitano walikuwa ni 9, 404 na wagonjwa
wa nje wenye umri zaidi ya miaka 5 walikuwa ni 36, 353. Wagonjwa waliolazwa na kupatiwa
huduma Hospitalini hapo walikuwa ni 8, 133, kati yao wagonjwa 3, 711 walikuwa ni watoto
wadogo. Ndiyo maana Hospitali ya Rufaa ya Mtakatifu Gaspar inaendelea kuwekeza katika
huduma kwa watoto ili kupunguza vifo vya watoto wadogo chini ya umri wa miaka 5 mintarafu
mpango mkakati wa Jumuiya ya Kimataifa.
Padre Serafini anaendelea kubainisha
kwamba, ili kuendeleza mchakato wa maboresho ya huduma ya afya kwenye Hospitali ya
Mtakatifu Gaspar, kunako tarehe 4 Septemba 2006, Chuo cha Uuguzi cha Mtakatifu Gaspar,
kilianzishwa. Chuo kinatoa stashahada na cheti ili kukidhi mahitaji ya rasilimali
watu katika sekta ya afya nchini Tanzania.
Padre Serafini anasema, zote hizi
ni juhudi za Uinjilishaji wa kina unaofanywa na Shirika la Wamissionari wa Damu Azizi
ya Yesu ili kujibu kilio cha damu kwa ajili ya maskini na wote wanaosukumizwa pembezoni
mwa Jamii. Shirika linaendelea kutoa huduma katika sekta ya elimu na mradi wa maji
safi na salama kwa ajili ya mikoa iliyoko Kanda ya kati, nchini Tanzania. Shirika
limekuwa ni mdau mkuu wa maendeleo endelevu Kanda ya kati.
Padre Serafini Lesiriam,
Mkurugenzi wa Hospitali ya Rufaa ya Mtakatifu Gaspar, Itigi anasema, Kanisa litaendelea
kushirikiana na Serikali ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania katika huduma za kiushauri,
rasilimali watu, dawa na vifaa. Mafanikio yaliyopatikana hadi sasa ni kutokana na
ushirikiano mkubwa kati ya Hospitali ya Rufaa Bugando, inayomilikiwa na kuendeshwa
na Baraza la Maaskofu Katoliki Tanzania pamoja na Tume ya Kikristo ya Huduma za Kijamii,
CSSC bila kuwasahau AMREF.
Hospitali ya Rufaa ya Mtakatifu Gaspar inakabiliana
pia na changamoto kubwa kama vile: upungufu wa rasilimali watu na fedha kutokana na
kupungua kwa kiasi kikubwa ruzuku iliyokuwa inatolewa na wafadhili kutoka ndani na
nje ya Tanzania kutokana na athari za myumbo wa uchumi kimataifa. Ongezeko kubwa la
gharama za dawa na vifaa tiba pamoja na upatikanaji wake kwa wakati muafaka.
Itakumbukwa
kwamba, Hospitali ya Rufaa ya Mtakatifu Gaspar iko Kanda ya Kati, nchini Tanzania,
eneo ambalo halina nguvu kubwa ya kiuchumi, kumbe, sehemu kubwa ya wagonjwa wanaotibiwa
Hospitalini hapo hawana uwezo mkubwa kiuchumi. Wananchi wengi bado hawana mwamko wa
kupata elimu ya kukinga na kutibu magonjwa, kiasi kwamba, wanalazimika kwenda Hospitalini
pale wanapokuwa wamezidiwa sana!
Habari hii imeandaliwa na Rodrick Minja
kutoka Radio Mwangaza, Dodoma na kuhaririwa na Padre Richard A. Mjigwa, C.PP.S. Idhaa
ya Kiswahili ya Radio Vatican.