2014-02-04 14:14:40

Walengwa washirikishwe kikamilifu katika Jukwaa la Ardhi Tanzania


Waziri Mkuu wa Tanzania Mizengo Pinda amesema Jukwaa la Ardhi linapaswa kushirikisha walengwa katika ngazi zote ili liweze kufanikiwa kuisaidia Serikali katika kutatua migogoro ya ardhi. “Amani ni tunu ya pekee ambayo kila mmoja wetu hana budi kuidumisha na kuipa uzito ili kuleta maendeleo ya Taifa letu.
Ametoa kauli hiyo wakati akizindua Jukwaa la ardhi Tanzania Jumanne, Februari 04, 2014 katika Ukumbi wa Golden Jubilee Towers jijini Dar es Salaam. “Pasipo amani, utulivu wa kufanya kazi iwe ni kilimo ama ufugaji hautapatikana na hivyo maendeleo ya mtu, kikundi cha watu ama Taifa yatabaki kuwa ndoto isiyoweza kutimia,” alisema.
Alisema kuzinduliwa kwa Jukwaa hili ni njia mojawapo itakayosaidia katika kutatua migogoro ya ardhi ambayo imekuwa na viashiria vya kupotea kwa amani ya Taifa: “Badala ya Ardhi kuwa msingi wa amani, na chanzo kikuu cha maendeleo na uzalishaji, inaanza kutugawa na kutuleea migogoro ya mara kwa mara”.
“Mtazamo wa Serikali kwa chombo hiki ni kwamba kitaleta na kukutanisha wadau mbalimbali ili kupeana uzoefu na kushirikishana na baadaye kuona mambo ya migogoro ya ardhi yanakuwa historia katika nchi yetu nina imani mtafanikisha”, alisema.
Ameagiza Jukwaa lijipange kujitegemea na kujitoa kufanyakazi kwani katika utekelezaji wa maazimio hayo lazima watakutana na changamoto nyingi sana, hivyo washirikishe jamii katika kila hatua ili kuweza kutekeleza maazimio yao: ”Kila mmoja atoke na dhamira kwamba tulichokizindua leo hakina msamiati wa kushindwa”.
“Jukwaa hili liwe chanzo cha elimu yenye tija itakayowezesha wanajamii kuiona na kuitumia ardhi yao huku wakizingatia sheria na kutumia zaidi tafiti mbalimbali,mipango na mikakati ya kimaendeleo kuhusisiana na ardhi”, alisema Waziri Mkuu. Viongozi wa Dini mna nguvu ya kipekee kwani wananchi wana imani kubwa nanyi hivyo tumieni imani hiyo vizuri ili muweze kutatua migogoro ndani ya Jukwaa hili”, alisisitiza.
Akimkaribisha Waziri Mkuu kuzungumza na wadau walioshiriki uzinduzi huo, Askofu Mkuu wa Kanisa la Kiinjili la Kilutheri Tanzania(KKKT), Dkt. Alex Malasusa alisema ardhi aliyoumba Mungu, haiongezeki bali wanadamu wanaongezeka na kama watu hawana mipango mizuri ya ardhi ni lazima patokee migogoro. “Usimamizi mzuri utazuia migogoro na kuepuka gharama zisizo za lazima. Tuko tayari kutoa mchango wetu kupitia Jukwaa la Ardhi la Tanzania ili wananchi wapate nafasi ya kushirikishwa kwa ukaribu zaidi”.
Mapema, akiongea katika uzinduzi huo Askofu Dk. Steven Munga amesema Jukwaa hili limeanzishwa ili kuelimisha na kuhabarisha jamii kwa njia ya ushirikishwaji wa taarifa kupitia jukwaa mbalimbali ambayo itasaidia watu kupata uelewa wa ukweli utaopunguza migogoro ya Ardhi. Alisisitiza kuwa Jukwaa la Ardhi litatumia dhana ya ushirikishwaji katika kujadili mambo yamayowahusu watu, na tunaamini kuwa ndio dhana bora ya Uongozi. “Nia ya Jukwaa ni kutoa nafasi kwa watu kutoa mawazo yao na kuayafanyiakazi kwa kushirikishwa”.








All the contents on this site are copyrighted ©.