2014-02-04 08:29:25

Nafasi ya wanawake katika Vituo vya Radio!


Jumuiya ya Kimataifa hapo tarehe 13 Februari 2014 itaadhimisha Siku ya Radio Duniani inayokazia Radio kama chombo muhimu sana katika mawasiliano ya kijamii, changamoto kwa wadau mbali mbali kushirikiana kwa karibu zaidi pamoja na kuendelea kuhamasisha matumizi ya mitandao ya kijamii kwa ajili ya kutoa habari, kukuza na kuendeleza uhuru wa mtu kujieleza. Ni fursa ya kukuza na kuimarisha usawa na umoja kati ya watu!

Radio bado inaendelea kufanya kazi zake msingi hata katika maendeleo ya teknolojia ya digitali, jambo ambalo linaviwezesha vituo vingi vya Radio kuweza kuufikia umati mkubwa wa watu sehemu mbali mbali za dunia. Shirika la Elimu, Sayansi na Utamaduni la Umoja wa Mataifa, UNESCO, linasema, kuna haja kwa Radio kusaidia kampeni ya Umoja wa Mataifa katika kujenga na kudumisha usawa kati ya watu pamoja na kuimarisha mchango wa wanawake ndani ya Jamii.

Huu ni mchango unaoweza kutekelezwa na waandishi wa habari kwa kukazia usawa kati ya mwanaume na mwanamke katika utekelezaji wa majukumu yao. Kuna haja kwa wadau mbali mbali kuwa na matumizi makubwa zaidi ya mitandao ya kijamii pamoja na kusaidia kulinda na kutetea usalama wa waandishi wa habari wanawake wanaotekeleza jukumu lao katika Vituo vya Radio sehemu mbali mbali za dunia.







All the contents on this site are copyrighted ©.