Kadiri ya misale ya mwaka 1962 ya Papa Yohane 23 kipindi cha noeli kinaisha kwa sikukuu
ya leo. Lakini baada ya marekebisho ya kalenda mwisho wa kipindi cha Noeli ni baada
ya Sikukuu ya Epifania, yaani baada ya sikukuu ya ubatizo wa Bwana wetu. Aidha, ni
mwisho wa kipindi cha Epifania.
Zamani sikukuu hii ilijulikana kama sikukuu
ya Mweuo wa Bikira Maria, lakini sasa ni “Kutolewa Bwana”. Kabla kabisa sikukuu hii
ilikuwa inaadhimishwa huko kwenye Kanisa la Mashariki likijulikana kama sikukuu ya
Maonano, au sikukuu ya kukutana kwa kigiriki wanaita Hypapante; au kwa kimombo ni
“encounter”.
Ni kutokana na maana hiyo ya kukutana tarehe 6 Januari mwaka
1997, Papa Yohane Paulo II akaiweka tarehe 2 Februari kuwa ni siku rasmi kwa watawa
kiulimwengu. Yaani ni Sikukuu ya wale wanaofuata maisha ya wakfu. Siku hiyo watawa
hukutanika na kuisherekea siku hiyo pamoja kwa sala. Hadi siku leo zimeshapita siku
40 tangu tusherehekee Noeli. Leo ndiyo Kanisa linatuletea sherehe ya kuonana au kukutana.
Ni siku rasmi ya kukutana na huyu mgeni aliyetufikia. Muda wote huu alikuwa
na wazazi tu na majirani wa karibu. Kuhusu mahali pa kukutana na mgeni huyu, Mwinjili
Luka anatutolea uvivu wa kumfuata nyumbani, bali anatuletea mtoto hekaluni, ambako
wazazi wake. Mungu aliyekuwa anasubiriwa na taifa lake sasa amejileta mwenyewe hapo
Hekaluni. Kwa sikukuu hii mnaalikwa nyote mkitaka kukutana na mtoto Yesu nendeni hekaluni
huko ameletwa na wazazi wake ili kumtolea hekaluni. Kama una mazoea ya kwenda kanisani,
unaweza kubahatika kumtambua, na si mazoea yako, hata hivyo mimi ninakualika leo kwenda,
pengine utabahatika kumtambua na pengine hata kumshika mkononi huyo mtoto.
Kwa
vile siku ya leo ni ya kukutana, tujaribu kuifanyia fikara dhamira hii ya kukutana,
ya kuonana, na kuangalia kama tunaweza kufaidika na dhamira hiyo ya kukutana. Hebu
tuangalie kwanza aina tatu za kukutana unazoweza kuziona katika sikukuu ya leo.
Aina
ya kwanza ya kukutana ni ya Mahekalu: Hekalu la Yerusalemu lilikuwa ni pahala patakatifu
pa kumwabudu Mungu kwa Wayahudi. Hata Yesu alipowakurupusha kwa fimbo watu waliofanya
biashara humo hekaluni alisema: “Nyumba yangu itakuwa nyumba ya sala”. Kwa hiyo hekalu
lile lilikuwa ni nyumba ya Mungu Baba yake, na ilikuwa pia ni nyumba yake. Yesu Kristu
ni Hekalu kama yeye mwenyewe alivyosema: “Bomoeni hekalu hili, nami nitalijenga kwa
siku tatu”, aliyasema maneno haya akimaanisha mwili wake mwenyewe.
Hivi Yesu
Kristo ni Hekalu la Agano jipya. Leo Yesu aliye hekalu, ameingizwa kwenye Hekaluni
la Yerusalem walimoabudia watu wa Agano la kale. Hapo Mahekalu yamekutana. Ni mwonano
mzuri, wa Hekalu la Agano jipya kulitakatifuza na kuliimarisha Hekalu la Agano la
Kale. Wewe ukiwa kama hekalu la Mungu kwa ubatizo, usiliambae kanisa.
Aina
ya pili ya Makutano ya Neno la Mungu: Ndani ya Hekaluni la Yerusalemu kuliwekwa
daima Torah yaani Maandiko Mtakatifu au Neno la Mungu, ikiwakilisha Agano la Kale.
Yesu Kristu ni Neno kama tunavyosoma “Neno la Mungu akatwa mwili akakaa kwetu”. Hapa
Neno la Agano Jipya linakutana na Neno la Agano la Kale ndani ya Hekalu. Wewe ni uliye
Neno hali la Mungu, hekalu la Roho Mtakatifu kwa kipaimara, usiache kulisoma Neno
la Mungu-Agano la Kale na Jipya.
Aina ya tatu ya Makutano ni ya Mtoto Yesu
na aina mbalimbali ya watu:
Tuko mwanzoni tu mwa ujio wa Yesu hapa duniani
na tayari tunaona msururu wa watu waliojaa dukuduku moyoni za kutaka kumwona hata
kabla hajafikia kiwango cha kutamka neno yaani kuhubiri, kwa vile bado ni mtoto mchanga.
Mtoto Yesu amebebwa na kuletwa kanisani (hekaluni. Huko daima kuna watu kama vile
makuhani, na baadhi ya waumini wanaofikafika tu kusali. Tunategemea kusikia kwamba
leo anaonana na mapadre, maparoko, watawa, na waumini kibao. Hebu sasa tuione furaha
ya binadamu anayefikiwa na Mungu wake.
Aina ya kwanza ya watu ni wazazi wake
: Yosefu na Maria Kabla ya kuwazungumzia watu wengine walioonana na Yesu, hebu
tuone jinsi wazazi wake waliomleta walivyofanya: Imeandikwa kwamba “Zilipotimia siku
za kutakasika kwao, kama ilivyo torati ya Musa, wazee wa Yesu walikwenda naye hata
Yerusalemu, wamweke kwa Bwana (kama ilivyoandikwa katika sheria ya Bwana, kila mtoto
mwanaume aliye kifungua mimba ya mamaye na aitwe mtakatifu kwa Bwana). Wakatoe na
sadaka, kama ilivyonenwa katika sheria ya Bwana: Hua wawili au makinda ya njiwa wawili.”
Kuna
maana mbili: Mosi: wazazi (Yosefu na Maria wanamtolea mtoto wao wa kwanza). Ujumbe
muhimu kwetu ni kuwa, wazazi hawa walitambua kwamba mtoto huyo si wao, bali ni wa
Mungu, wao wamekabidhiwa na kuaminishwa tu ili kumwandaa kwa ajili ya utume aliotumwa
kuja kuutekeleza hapa duniani. Wao wanamwandaa tu ili aweze kuwa kama anavyotakiwa
kuwa kadiri ya hali inayotegemewa na Bwana aliyemtuma.
Kwa hiyo fundisho ni
kwamba kila mtu na kila mtoto anayeingia hapa duniani ni zawadi tu kwetu ni mali ya
Mungu. Anachotakiwa kukifanya kila mzazi ni kumtolea mtoto huyo kwa Mungu na siyo
kumhodhi tu. Wazazi wanatakiwa wamtunze na kumhudumia ili aweze kutimiza utume alioitiwa
kwa kuzaliwa hapa duniani. Pili, Wazazi hawa hawatoi kondoo kama wafanyavyo wenye
kipato, bali wanatoa njiwa ili kuonesha jinsi walivyokuwa fukara. Huu ni mfano kwa
mwumini kuwa mtu wa kawaida siyo wa kutaka makuu na kupaparikia mali na kutawaliwa
nayo.
Aina ya pili ya watu ni kukutana Simoni na Anna: Tunaletewa mtu wa
kwanza aliyeonana na Yesu ikisema: “Palikuwa na mtu, jina lake Simeoni, naye ni mtu
mwenye haki, mcha Mungu, akiitarajia faraja ya israeli. Na Roho mtakatifu alikuwa
juu yake.” Mtu huyu Simeoni tuliyeletewa tunaambiwa kuwa ni mtu mwenye haki na wa
kumcha Mungu (mtu wa sala). Maana yake, hapa kuna makutano kati ya mwisraeli wa kwelikweli
na Masiha wa kweli anayesubiriwa. Simeoni ameoneshwa Masiha aliyekuwa anasubiriwa
katika kipindi chote cha Agano la Kale lililokuwa linasubiriwa kutimilizwa.
Cha
ajabu ni kwamba pale hekaluni palikuwa pamejaa lukuki ya binadamu. Lakini ni watu
wawili tu ndiyo wanaomtambua mtoto huyu kuwa ni Masiha. Aidha watu hawa wala si mapadiri
wala watawa, bali ni vizee vya kawaida tu. Ni tofauti na vijana tu wazazi wa mtoto
(Yosefu na Maria). Kulikoni? Je, vizee hivi vilifanya nini cha ajabu hadi vikafaulu
kumtambua mtoto huyu kuwa ni Masiha wa Bwana?
Jibu linapatikana katika Maandiko
hayohayo pale inaposema kwamba: “Simeoni alikuwa mtu mwenye haki na mcha Mungu, alikuwa
na roho safi na nyeupe”. Heri wenye moyo safi maana hao watamwona Mungu. Watu wenye
moyo safi ndiyo wanaweza kuona zaidi ya kile kinachoonekana kwa macho. Watu wengine
waliofika pale hekaluni walikuwa wanamwona mtoto huyu kama vile angekuwa kama watoto
wengine wa kawaida. Yaani mtoto asiye na la pekee.
Simone kumbe, analo jicho
la pekee na anafaulu kuona hadhi ya pekee aliyokuwa nayo mtoto huyu kuwa siyo wa kawaida,
yaani ni Masiha wa Bwana. Kuna pia hoja nyingine inayomsaidia Simoni kuona mambo tofauti
na wanavyoona wengine. “Ni kwamba Roho Mtakatifu alikuwa juu yake, kwamba Roho mtakatifu
alimtaarifu mapema kwamba hatakufa kabla ya kumwona Kristu wa Bwana. Aidha alikuja
hekaluni ameongozwa na Roho” Kwa mantiki hiyo Simoni alikuwa amesukumwa na Roho. Alikuwa
daima katika maisha yake anaongozwa na Roho wa Bwana na siyo kuburuzwa na vionjo vya
ulimwengu huu. Kumbe Roho huyo anaongea pia ndani yetu.
Yabidi kumsikiliza,
badala ya kumvuruga, na kumdharau na kumpurukusha hadi anashindwa kusikika anapootuongelesha
nafsini mwetu. Tunabaki tumeng’ang’ana na hoja zetu na fikra zetu tu. Roho anaongea
nasi, hasa tunapokutana na Kristo anapoongea nasi katika Neno lake, katika watu wanaotushauri
na kutuhubiria, hapo ndipo kuna sauti ya huyo Roho anayetuwezesha kumtambua na kusema
huyu ndiye Kristu, hii ni sauti ya Roho mtakatifu.
Mzee Simoni alikuwa alisikiliza
daima sauti hiyo. Kwa kufanya hivyo alimtukuza Bwana na ameweza kuyapa maana maisha
yake. Kwa vile ni mzee unamwona pia anaimba. Watawa daima tunaimba wimbo wa mzee Simoni
katika sala za mwisho (kompleto): “Sasa Bwana wamruhusu mtumishi wako, kwa amani,
kama ulivyosema; kwa kuwa macho yangu yemeuona wokovu wako, nuru ya kuwa mwangaza
wa mataifa na kutukufu wa watu wako Israeli”.
Kwa maneno haya Umruhusu mtumishi
wako mzee Simoni anatufundisha jinsi nzuri ya kuzeeka na kukabiliana na kifo. Mzee
huyu anaangalia mbele katika maisha. Siyo kulalamika na kunung’unikia maisha yaliyoishapita
au yaliyopo. Haangalii nyuma kwamba maisha hayana maana. Kwake kifo ni kama kwenda
kwenye amani. Ni kama kusema, nimeishi maisha yangu nikiongozwa na Roho wa Bwana,
sasa sihitaji tena kitu kingine bali ni kuachana na maisha haya. Nimeshaona mwanga
tayari. Sasa kumebaki ni kwenda mbele kuelekea kwenye amani.
Kuhusu neno kuruhusu,
halimaanishi kukimbia majukumu kama wasemavyo wengi. Mimi ni mzee mniache nipumzike.
La hasha, bali ni kwenda kutangaza habari njema. Mzee Simeoni hajifikirii yeye mwenyewe
tu, bali anafikiria juu ya mwanga utakaoangaza ulimwengu. Kisha anashukuru Maria na
Yosefu, na anafanya utabiri. Mtoto huyu ni anguko na ufufuko kwa wengi Israeli. Yaani
ni upanga utakaochoma moyo. Kuna woga wa lengo la mtoto huyu. Wengine watampokea wengine
watamkataa. Mtoto huyu anao wito wa kufanya. Yeye mwenyewe atakataliwa na itamwumiza
pia huyu mtoto huko kukataliwa.
Kuhusu Nabii huyu wa kike Anna siyo yule mke
wa Yoakim ambao ni wazazi wa mama wa Maria. Mama huyu anatajwa hapa kama alama tu
inayotaka kutufundisha au kutuletea ujumbe fulani wa maana. Tunaambiwa alikuwa na
miaka 84. Miaka hii ina maana yake zaidi ya kutuonesha umri wake. Namba hii inapatikana
kwa kuzidisha 7 mara 12. Namba saba inamaanisha ukamilifu, pindi namba kumbi na mbili
ni alama ya watu yaani makabila kumi na mbili ya Israeli, na pia mitume kumi na wawili.
Mama huyu anawakilisha taifa hili la waisraeli wanaompokea Masiha wa Mungu. Watu hawa
waisraeli ndiyo wale wanaotegemewa kumpokea Masiha wa Mungu.
Alama nyingine
anayotuonesha mama huyu Anna ni kwamba alikuwa ni mwanamke aliyeolewa na kukaa na
mume wake kwa miaka saba (hata hapa namba inayoonesha ukamilifu) kisha anabaki mjane
(ingawa haisemwi kama alifiwa na mume au aliachika tu) lakini jambo muhimu linaloonekana
kwake ni kwamba, anabaki hivi mjane bila kuolewa tena na mume mwingine. Mama huyu
ni alama ya uaminifu yaani anawakilisha uaminifu.
Aliamua kutopenda tena mtu
mwingine, bali ni kubaki mwaminifu kwa mume wake wa kwanza (ndoa) aliyemfungia nadhiri
zake. Katika kipengee hiki Anna anawakilisha uaminifu kwa mume au Bwana mmoja ambaye
kwa wana Taifa la Israeli, ni uaminifu kwa Bwana mmoja yaani Mungu. Yeye ndiye mume
wa ndoa ambaye si mtoa amri, mwamrishaji, siyo katili. Ni mume aliyempenda mke wake
yaani ulimwengu. Huyo Bwana arusi wa kanisa ni Yesu Kristu. Mke wake ndoa ni Kanisa,
huyo ndiye anampokea na kumkumbatia Bwana wake. Hapa unakuta tena kukutana kwingine,
kati ya Bwana na Bibi arusi. Mungu na binadamu. Bi arusi (Anna) anamtambua Bwana arusi
na wanakumbatiana.
Alama nyingine anayotuonesha Anna inatokana na asili yake.
Hasahasa jinsi asivyoogopa wala kuona aibu kujionesha mbele za watu licha ya utofauti
huo. Imeandikwa kwamba Mama huyu alikuwa biti Fanueli wa kabila la Asheri. Kabila
hili, lilikuwa na bahati ya kukabidhiwa ardhi yenye rutuba sana, hivi wakajiendeleza
sana kiuchumi. Kwa vile ardhi hiyo ilikuwa ni sehemu ya upagani, wakachangamana nao,na
kujizamisha katika raha za utajiri, kisha kabila likajikuta limepoteza utamaduni na
imani yake na hatimaye likafifia kabisa. Kwa hiyo wakati wa (enzi za Yesu) kabila
hili lilikuwa limeshafifia kabisa. Kama kulikuwa na watu waliobakia wa kabila hili,
waliona aibu sana kujionesha kadamnasi.
Kumbe ni mama huyu tu aliyebaki mwaminifu
kwa imani yake kwa Mungu mmoja bila kuyumbishwa na miungu mingine ya kipagani. Mama
huyu anawakilisha waisraeli waliobaki waaminifu bila kuyumbishwa na miungu mbalimbali
inayowazunguka. Mama huyu anajiwakilisha tofauti na wengine. Ndugu zangu ni ngumu
sana kumfuata Kristu katika mazingara yenye thamani fulani za dunianhii zinazovutia
kwa nguvu sana. Yabidi wakati mwingine kujikaza na kubaki katika msimamo wako.
Hata
kiutamaduni. Makabila mengine yanapoteza utamaduni wake kutokana na kushabikia utamaduni
wa makabila mengine. Kadhalika utamaduni wa nchi, unaweza kufifia wenyewe bila kujitambua
kwa kuyumbishwa na utamaduni wa mataifa mengine, iwe lugha, mavazi, muziki, nk. Kazee
haka kanatufundisha kutojivua nguo za utamaduni zilizohifadhi utu wetu na kujifunika
maua ya utamaduni wa mataifa mengine kwa vile yanapendeza kuyatazama.
Ujumbe
wa Papa kwa siku ya 17 ya Siku ya Watawa ulimwenguni: “Katika Kristo tunajigundua
kuwa tumependwa na Mungu, kwamba tayari tulishatiwa wakfu kwake katika ubatizo, tukaitwa
kujitolea sadaka wewe katika upendo, tukitegemezwa na neema ya Roho mtakatifu. Katika
yeye tunakuta kila siku maana ya mwito wetu na kupata furaha ya kuwa wanafunzi na
mashuhuda wake.”
Tafakari hii imeandaliwa na Padre Alcuin Nyirenda, OSB.