2014-02-02 13:59:18

Vinana na wazee wanakutana; wanaongozwa na Roho Mtakatifu kutekeza sheria na unabii!


Siku kuu ya kutolewa Bwana Hekaluni ni kielelezo ambacho kwa mara ya kwanza Yesu anakutana na watu wake; ni mkutano kati ya vijana yaani Bikira Maria na Mtakatifu Yosefu wakiwa na Mtoto wao Yesu Kristo na wazee wanaowakilishwa na Mzee Simeoni na Anna, waliokuwa Hekaluni. Ni Siku ya 18 ya Watawa Duniani iliyoanzishwa na Mwenyeheri Yohane Paulo wa Pili kunako mwaka 1997.

Watawa wa Mashirika ya Kitawa na Kazi za kitume wamekusanyika, Siku ya Jumapili tarehe 2 Februari 2014 kwenye Kanisa kuu la Mtakatifu Petro mjini Vatican ili kuungana na Baba Mtakatifu Francisko aliyeadhimisha Ibada ya Misa hii kwa mara ya kwanza kama Khalifa wa Mtakatifu Petro. Baba Mtakatifu katika mahubiri yake anasema, Wazazi wa Yesu walitaka kutekeleza kwa furaha kile kilichokuwa kimeandikwa katika Sheria ya Mungu, kwani walitambua kwamba, furaha ya kweli inabubujika kutoka katika Amri za Mungu.

Baba Mtakatifu anasema, Mzee Simeoni na Anna: wachamungu na watu wa haki waliongozwa na Roho Mtakatifu, huku wakiwa wamesheheni maisha, wakakutana Hekaluni. Ni mkutano ambao unawaonesha vijana wakiwa wamejaa furaha katika kutekeleza Sheria ya Mungu na wazee wakiwa wanafurahia kazi ya Roho Mtakatifu. Kwa pamoja wanakutana katika kutekeleza sheria na unabii. Vijana katika tukio yaani Maria na Yosefu wanatekeleza sheria na Wazee wanatimiza Unabii.

Hii inaonesha kwamba utekelezaji wa sheria ni kazi na hamasa kutoka kwa Roho Mtakatifu na kwamba, Unabii unatekelezeka kwa kufuata mkondo wa sheria. Bikira Maria alikuwa amejaa nguvu ya Roho Mtakatifu na mnyenyekevu kwa Roho Mtakatifu.

Baba Mtakatifu anasema, huu ndio mwanga ambao Mama Kanisa anapenda kuuangalia mintarafu maisha ya kuwekwa wakfu ndani ya Kanisa. Huu ni mkutano kati ya Watawa na Kristo. Yesu anakuja kuwatembelea watu wake, akiwa amebebwa na Bikira Maria Mtakatifu Yosefu, changamoto kwa watawa na waamini katika ujumla wao, kumwendea ili waweze kukutana naye, huku wakiwa wameongozwa na nguvu ya Roho Mtakatifu.

Waamini wanakumbushwa kwamba, kiini cha mkutano huu ni Yesu mwenyewe, anayeongoza na kuwavuta watu kumwendea Hekaluni, Kanisani na mahali popote ambapo, waamini wanaweza kukutana, kumtambua, kumpokea na kumkumbatia Yesu.

Baba Mtakatifu anawaambia Watawa kwamba, Yesu anakutana nao ndani ya Kanisa kwa njia ya karama za waanzilishi wa Mashirika yao ya kitawa na kazi za kitume na huu ndio mwanzo wa maisha na wito wao wa kitawa. Maisha haya yanamwilishwa ndani ya Kanisa kwa njia ya karama iliyotolewa ushuhuda na mwanzilishi wa Shirika, hili ni jambo linaloshangaza na mwaliko wa kumwimbia Mwenyezi Mungu utenzi wa shukrani.

Baba Mtakatifu anasema kwamba, katika maisha ya kitawa kuna mwingiliano kati ya wazee na vijana; kiini cha utekelezaji wa sheria na unabii. Mambo haya mawili ni sawa na chanda na pete na wala hakuna ukinzani wowote. Ni mwaliko kwa watawa kumwachia nafasi Roho Mtakatifu ili awasaidie kutekeleza majukumu haya mawili kwa ufanisi mkubwa, katika furaha ya kutekeleza na kumwilisha sheria ya maisha. Ni furaha ya mtu anayeongozwa na Roho Mtakatifu; bila ya kuwa na moyo mgumu wala kujifungia katika ubinafsi wake, bali mkweli na muwazi katika kuisikiliza sauti ya Mungu inayozungumza naye; ni Mungu anayefungua na kuelekeza.

Baba Mtakatifu anawaalika wazee kuhakikisha kwamba, wanajitahidi kuwashirikisha na kuwamegea vijana hekima na busara; vijana nao wawe tayari kupokea na kumwilisha hazina hii kubwa ya uzoefu na hekima ili kuweza kuiendeleza mbele kwa ajili ya mafao na ustawi wa Mashirika ya Kitawa na Kanisa katika ujumla wake. Baba Mtakatifu mwishoni mwa mahubiri yake awaombea wote akisema, neema ya Fumbo hili la kukutana, liwe ni mwanga na faraja katika hija ya maisha yao ya kiroho!

Itakumbukwa kwamba, Ibada hii ya Misa Takatifu ilianza kwa Maandamano ya Watawa waliokuwa wamebeba mishumaa, alama ya Kristo Mwanga wa Mataifa anayeingia Hekaluni, yaani nyumbani mwa Baba yake.







All the contents on this site are copyrighted ©.