Shirikianeni na Maaskofu Mahalia na Tume za Mafundisho Tanzu ya Kanisa ili kulinda
na kutunza hazina ya imani ya Kanisa
Baba Mtakatifu Francisko, Ijumaa tarehe 31 Januari 2014 amekutana na kuzungumza na
wajumbe wa Baraza la Kipapa la Mafundisho Tanzu ya Kanisa waliohitimisha mkutano wao
wa Mwaka hapa mjini Vatican. Baraza hili lina uhusiano wa pekee na utume wa Khalifa
wa Mtakatifu Petro, yaani wa kuwaimarisha ndugu zake katika imani sanjari na kuendelea
kulinda na kutetea Mafundisho ya Mama Kanisa.
Wajumbe wa Baraza hili wanapaswa
kuhakikisha kwamba vigezo vya imani vinapewa kipaumbele cha kwanza katika maneno na
matendo ili kuendeleza uwepo wa Mungu unaozaa matunda! Imani kwa Yesu Kristo inaufungua
moyo wa Mungu na maisha ya mwanadamu ili kuweza kuuona ukweli na mazuri yanayobubujika
kutoka kwa Mwenyezi Mungu.
Mafundisho tanzu ya Kanisa si sera wala siasa,
ni mambo msingi yanayopania kuwasaidia Watu wa Mungu ili kuwa na msingi imara wa imani,
bila kumiliki zawadi ya ukombozi inayotoka kwa Mwenyezi Mungu.
Baba Mtakatifu
Francisko anawakumbusha wajumbe wa Baraza la Kipapa la Mafundisho Tanzu ya Kanisa
kwamba, wamekabidhiwa dhamana nyeti, inayowahamasisha kushirikiana kwa karibu zaidi
na Maaskofu mahalia na Tume za Mafundisho tanzu ya Kanisa katika Mabaraza ya Maaskofu
Katoliki sehemu mbali mbali za dunia. Ili kulinda na kudumisha hazina ya imani ya
watu wa Mungu katika usafi na utimilifu wake.
Wajumbe wanapaswa kujenga majadiliano
endelevu na yenye kuheshimiana na wahusika. Ukweli hauna budi kujikita katika uaminifu
na upendo, ili kujenga na kuimarisha udugu na ukomavu katika mawazo ya mtu! Baraza
hili linajipambanua kwa kujikita katika umoja na majadiliano, kwa kutambua kwamba,
Kanisa ni mahali pa kujenga umoja kila mtu akijaribu kutekeleza wajibu wake aliokabidhiwa
na Kristo.
Utume huu, uwajengee ndani mwao ari ya furaha inayobubujika kutoka
kwa Kristo mwenyewe. Watambue kwamba kwa neema wamebahatika kuwa ni wafuasi wa Kristo
wanaoshiriki katika utume wa Kanisa katika azma ya Uinjilishaji, jambo linalowakirimia
furaha ya kweli.
Wajumbe wamejadili pamoja na mambo mengine kuhusu Imani na
uhusiano wake katika Sakramenti ya Ndoa, changamoto iliyokuwa imetolewa na Baba Mtakatifu
mstaafu Benedikto XVI alipokutana nao kwa mara ya mwisho. Kuna haja ya kufanya tafakari
ya kina kuhusu uhusiano uliopo kati ya imani ya mtu binafsi na Maadhimisho ya Sakramenti
ya Ndoa, mintarafu utamaduni mambo leo.
Amewapongeza kwa kazi kubwa waliyoijadili
kuhusiana na changamoto katika maisha ya ndoa na falimia, nyanyaso za kijinsia dhidi
ya watoto wadogo na kwamba, watoto wadogo wanapaswa kulindwa katika mazingira ya Kanisa
ili waweze kukua na kukomaa kiutu na kiroho!
Baba Mtakatifu anasema anapenda
kuunganisha Tume ya Kipapa ya kulinda na kutetea watoto katika Baraza la Kipapa la
Mafundisho Tanzu ya Kanisa, ili wawe kweli ni mfano bora wa kuigwa kwa wadau mbali
mbali wanaotaka kulinda na kutetea mafao ya watoto.