Pinda azindua rasmi mapitio ya mfumo wa uwekezaji Tanzania
Waziri mkuu Mizengo Pinda amesema Tanzania ni miongoni mwa nchi zitakazonufaika katika
masuala ya uwekezaji nchini endapo itatekeleza kikamilifu Mapitio ya Mfumo wa Uwekezaji
yaliyowasilishwa na Taasisi ya Ushirikiano wa Kiuchumi na Maendeleo (OECD). Ametoa
kauli hiyo leo Ijumaa, Januari 31, 2014, wakati akizungumza na waandishi wa habari
mara baada ya kuzindua kitabu cha Mapitio ya Mfumo wa Uwekezaji kwenye ukumbi wa
Kimataifa wa Mwalimu Nyerere jijini Dar es Salaam.
Akizungumza katika uzinduzi
huo, Waziri Mkuu Pinda alisema kuwa malengo ya mapitio ya mfumo huo ni kuboresha
hali ya uwekezaji na biashara nchini ambayo matokeo yake yatasaidia kuongeza wawekezaji
katika maeneo mengi. “Kuna maeneo ya uwekezaji yanayopata uwekezaji wa moja kwa moja
kutoka nje ya nchi (Foreign Direct Investment -FDI) ambayo ni umeme, mafuta, gesi,
madini, viwanda, ujenzi na huduma za jamii.”
Amesema kuwa matokeo ya jitihada
hizi ni makubwa na yameonekana ndani ya miaka miwili tu. Akitoa mfano, alisema: “Kilimo
kimeweza kukua kutoka dola za marekani milioni 304.5 mwaka 2010 hadi dola za marekani
milioni 355.4 katika mwaka 2011. Vilevile kwenye sekta ya Umeme na Gesi imekua kutoka
dola za kimarekani milioni 328.6 hadi dola za kimarekani 539.8 mwaka 2011.”
Kutokana
na matokeo hayo, Waziri Mkuu ameeleza kuwa Tanzania ina fursa nyingi zikiwemo rasilimali,
nafasi yake kijiografia na historia ya siasa safi ambazo zinaifanya iwe kivutio kikubwa
cha uwekezaji. Hali hiyo Waziri Mkuu alisema, imesaidia Pato la Taifa kuendelea kukua
kwa asilimia sita kwa miaka 10 mfululizo na mwaka jana ilikua kwa asilimia saba na
sasa inatarajiwa kufika asilimia 7.2 kwa mwaka huu.
Miongoni mwa maeneo yanayohusishwa
na mfumo huu wa mapitio ya Uwekezaji ni yale yaliyoainishwa katika Matokeo makubwa
sasa ambayo ni Kilimo, Maji, Uchukuzi, Elimu na Nishati. “Ili kufanikisha maeneo hayo
ni muhimu tukajenga mazingira bora ya uwekezaji, hivyo Serikali inawataka wadau wote
kwa kushirikiana na Sekta binafsi kuchambua kwa makini mapendekezo ya mapitio ya mfumo
huo ambayo yanatumika pia kuharakisha mafanikio ya Matokeo makubwa sasa”, alisisitiza
Waziri Mkuu.
Waziri Mkuu alisema Serikali ya Tanzania inashukuru sana Taasisi
ya Ushirikiano wa Kiuchumi na Maendeleo (OECD) kwa kuweka sura maalum kwenye kitabu
hicho inayozungumzia changamoto za uwekezaji kwenye sekta ya kilimo na jinsi ya kukabiliana
na changamoto hizo.
“Ninatumaini kuwa utekelezaji wa mapendekezo haya utaongeza
ufanisi wa mchakato huu na kuhakikisha kuwa tunazitumia fursa zilizopo na nyingine
zaidi katika kuboresha uwekezaji katika kilimo nchini. Na kwenye kilimo ninamaanisha
kilimo mazao, mifugo, uvuvi na nyuki,” aliongeza.
Mapema, Naibu Katibu Mkuu
wa Taasisi ya OECD, Bw. Rintaro Tamaki, alisema mazingira ya uwekezaji nchini yanabadilika
kila mara kutokana na kuvumbuliwa kwa rasilimali mpya kama vile gesi, makaa ya mawe
ambazo zinasababisha watu wavutive kuwekeza nchini. ”Kutokana na kugunduliwa na sekta
hizo, Serikali isizipuuzie sekta za zamani hususan Sekta ya kilimo, cha msingi ni
kuboresha sekta hii kwa kuanzisha viwanda ili kuongeza thamani ya mazao yenu”.