2014-01-30 15:43:40

Vyuo vikuu vinahamsishwa kushiriki kikamilifu katika mchakato wa Uinjilishaji Mpya!


Baba Mtakatifu Francisko, Alhamisi tarehe 30 Januari 2014 amekutana na kuzungumza na Wajumbe wa Chuo Kikuu cha Notre Dame, chenye makao yake makuu huko Indiana, Marekani; chuo ambacho kilianzishwa kunako mwaka 1842 na Padre Edward Sorin, kutoka Shirika la Santa Croce.

Chuo hiki kwa sasa kimeamua kufungua tawi lake mjini Roma, ili kuendeleza mchakato wa kuwarithisha vijana wa kizazi kipya utajiri unaofumbatwa katika historia, tamaduni na maisha ya kiroho. Roma ni mji ambamo watakatifu Petro na Paulo waliyamimina maisha yao, kielelezo cha imani inayoendelea kuungamwa na mashahidi wa nyakati zote pamoja na kurithishwa kutoka kizazi kimoja hadi kingine kwa njia ya: familia, shule na parokia.

Baba Mtakatifu amekipongeza Chuo Kikuu cha Notre Dame kutokana na mchango wake katika elimu ya maisha ya kiroho kwa vijana wa kizazi kipya pamoja na kutoa fursa za masomo ili wanafunzi waweze kunoa akili kwa kuweka uwiano sawia kati ya imani na uwezo wa mtu kufikiri na kutenda, katika mchakato wa kutafuta ukweli. Vyuo vikuu vina mchango mkubwa katika utume wa Uinjilishaji Mpya na kwamba, Chuo Kikuu cha Notre Dame, kimechangia kwa kiasi kikubwa katika maboresho ya elimu ya msingi nchini Marekani

Utambulisho, dhamana. mchango na huduma ya Chuo Kikuu cha Notre Dame imeendelea kubaki bila mabadiliko makubwa hata katika Karne ya 21. Baba Mtakatifu anasema Kanisa halina budi kuendelea kukazia utambulisho wake wa kimissionari kwa njia ya ushuhuda unaotolewa na wafuasi wa Kristo wanatekeleza majukumu yao hata katika taasisi zinaendeshwa na kusimamiwa na Mama Kanisa; utume huu kwa namna ya pekee, ujioneshe kwa Vyuo vikuu na Taasisi za elimu ya Juu, ili kuweka sawia imani na uwezo wa mwanadamu kufikiri na kutenda; mambo yanayomwezesha mwanadamu kuishi katika ukamilifu wake.

Baba Mtakatifu Francisko anasema, ushuhuda wa vyuo vikuu ni jambo la muhimu sana katika utekelezaji wa mafundisho ya maadili yanayotolewa na Mama Kanisa; kwa kusimama kidete kulinda na kutetea uhuru sanjari na kuendeleza Mafundisho ya Kanisa katika medani mbali mbali za maisha ya mwanadamu. Ni matumaini ya Baba Mtakatifu kwamba, Chuo Kikuu cha Notre Dame, kitaendelea kutolea ushuhuda wa tunu hizi msingi katika maisha na utume wake, kwa kulinda utambulisho wa Kikristo.

Baba Mtakatifu amewaomba wajumbe kumwombea katika maisha na utume wake kwa ajili ya Injili ya Kristo na kwamba, anawakumbuka kwa sala na sadaka yake. Mwishoni, amewapatia baraka zake za kitume!







All the contents on this site are copyrighted ©.