2014-01-30 08:11:22

Upatu unadhalilisha utu na heshima ya binadamu!


Baba Mtakatifu Francisko wakati wa Katekesi yake Siku ya Jumatano, tarehe 29 Januari 2014 alikemea vikali tabia ya michezo ya upatu inayodhalilisha utu na heshima ya binadamu na kwa kusema kwamba, huu si Ukristo wala si ubinadamu; ni tabia ambayo inapaswa kukomeshwa ndani ya Jamii kwani inawasababishia watu majanga ya maisha!

Baba Mtakatifu ameyasema hayo wakati alipokuwa anawasalimia wawakilishi wa kitaifa wa Mfuko wa Yohane Paulo II dhidi ya upatu kitaifa, ambao baadaye jioni waliadhimisha Ibada ya Misa Takatifu kwenye Kanisa kuu la Mtakatifu Petro mjini Vatican na kuongozwa na Kardinali Angelo Comastri, Askofu msaidizi wa mji wa Vatican.

Katika mahubiri yake Kardinali Comastri anasema mwelekeo wa watu kupenda na kuthamini mno fedha na mali, umewatumbukiza watu wengi katika majanga ya maisha. Baadhi yao wamejikuta wakikabiliana na mkondo wa sheria kwa kuikiuka sheria, kanuni na maadili jamii. Watu wanaabudu sana fedha kiasi cha kuifanya kupoteza ile thamani yake kwa kunyanyasa na kudhalilisha utu na heshima ya binadamu. Baadhi ya watu wanaifanya fedha kuwa eti sabuni ya roho na mtawala wa maisha ya baadhi ya watu, hata utu na heshima ya mtu inapimwa kwa viti alivyonavyo mtu na wala si utu wake kwa vile ameumbwa kwa sura na mfano wa Mungu.

Tamaa ya utajiri wa haraka haraka umewatumbukiza watu katika michezo michafu ya upatu na kamari, mambo yanayochafua utu na heshima ya binadamu. Habari Njema ya Wokovu inayotangazwa na kushuhudiwa na Mama Kanisa ni kwamba, mtu anapaswa kupewa kipaumbele cha kwanza; jambo msingi linalojidhihirisha katika Amri ya Upendo kwa Mungu na jirani; muhtasari wa mafundisho makuu ya Yesu yanayopaswa kumwilishwa kwa njia ya matendo ya huruma.

Kardinali Comastri anasema, watu wanapaswa kujenga utamaduni wa upendo na mshikamano na wala si kunyanyasana na kufedheheshana. Watu wasisahau kwamba, mara baada ya kifo, mali na utajiri wa dunia hii wataiacha hapa duniani na watasindikizwa na sanda ya matendo mema waliyowatendea jirani zao. Mshikamano wa upendo na kidugu ndiyo changamoto inayofanyiwa kazi na Baba Mtakatifu Francisko kwa njia ya mafundisho na ushuhuda wa maisha yake.

Anawakumbusha watu wasitawaliwe mno na fedha na mali, bali mambo haya yawe ni kikolezo cha mshikamano wa upendo na udugu kwa kuwajali na kuguswa na shida pamoja na mahangaiko ya jirani zao kwa hali na mali! Kanisa linawapongeza mashujaa wanaosimama kidete kuwalinda na kuwatetea maskini na wanyongwe wanaoendelea kudidimizwa na watu wenye uchu na tamaa ya mali na fedha kwa njia ya mkato.

Watu wasikubali na kujidekeza hatimaye wakajikuta wanatumbukizwa kwenye mchezo wa upatu na kamari kwani ni hatari kwa maisha na maendeleo yao! Anasema Kardinali Angelo Comastri wakati anahitimisha mahubiri yake!







All the contents on this site are copyrighted ©.