2014-01-30 11:21:19

Fadhila ya unyenyekevu, uaminifu na maisha ya sala ni muhimu sana kwa utambulisho wa Mkristo ndani ya Kanisa!


Ni dhana isiyoweza kueleweka kwa mtu kujiita Mkristo pasi ya kuwa sehemu ya Kanisa! Unyenyekevu, uaminifu na maisha ya sala ni mambo muhimu sana yanayoweza kumtambulisha mwamini kuwa kweli ni Mkristo.

Mfalme Daudi alitambua kwamba, alikuwa ni sehemu ya Taifa la Mungu, anafurahia kuzungumza na Mwenyezi Mungu kwa njia ya Sala na kupokea changamoto zinazowekwa mbele yake, changamoto kwa waamini kujisikia kuwa ni sehemu ya Kanisa na ndani ya Kanisa.

Haitoshi kwa mwamini kupokea Sakramenti ya Ubatizo na baadaye kutokkomea "mitini" akaendelea kujiita kuwa ni Mkristo; kwa kudhani kwamba, anamsikiliza Kristo lakini kwa upande mwingine analibeza na kulitweza Kanisa lililoanzishwa na Kristo mwenyewe! Huwezi kuwa Mkristo wa kweli kwa kusimama pembezoni mwa Kanisa, Kanisa linajengwa na kuimarishwa kwa njia ya utakatifu na mshikamano unaowawezesha waamini kujisikia kuwa kweli ni sehemu ya Fumbo la Mwili wa Kristo, yaani Kanisa.

Kama fadhila ya unyenyekevu inapwelea katika maisha ya mwamini hapa kuna shida, kwani mtu atashindwa pia kuutambua ukuu na utukufu wa Mungu kama alivyofanya Mfalme Daudi kama anavyosimuliwa kwenye Liturujia ya Neno la Mungu, Alhamisi, tarehe 30 Januari 2014.

Hii ni sehemu ya mahubiri yaliyotolewa na Baba Mtakatifu Francisko kwenye Kikanisa cha Mtakatifu Martha kilichoko mjini Vatican. Anasema, historia ya ukombozi ni mchakato ulioanzishwa na Mwenyezi Mungu na kuendelezwa na Mama Kanisa kwa watu wa nyakati mbali mbali. Unyenyekevu uwasaidie watu kutambua kwamba, wao ni sehemu ya Familia kubwa ya Mungu ulimwenguni.

Unyenyekevu, uaminifu na utii ni fadhila muhimu sana katika maisha na utume wa Kanisa. Waamini wanapaswa kuwa waaminifu kwa Kristo na Kanisa lake; waaminifu kwa Kanuni ya Imani na Mafundisho ya Kanisa, kwa kutambua kwamba, wamebarikiwa kupata Injili ya Kristo kama zawadi, changamoto na mwaliko wa kuhakikisha kwamba, wanawashirikisha wengine zawadi hii kwa uaminifu mkubwa.

Baba Mtakatifu anawaalika waamini na watu wote wenye mapenzi mema kuendelea kuliombea Kanisa katika maisha na utume wake! Utume huu upate chimbuko lake kuanzia kwenye familia ili waamini waendelee kutambua na kuthamini hija hii inayowasaidia kujisikia kuwa wao ni sehemu ya Fumbo la Mwili wa Kristo yaani Kanisa.







All the contents on this site are copyrighted ©.