2014-01-30 07:22:01

Changamoto katika maisha ya kitawa na Kipadre! 2015 ni Mwaka wa Watawa


Uaminifu na udumifu wa wito wa kitawa katika tamaduni za mpito ni mada ambayo imepembuliwa kwa kina na mapana hivi karibuni kwenye Kongamano la siku moja lililoandaliwa na Chuo Kikuu cha Kipapa cha Antonianum kilichoko mjini Roma na kuwashirikisha viongozi wakuu kutoka Baraza la Kipapa la Mashirika ya Kitawa na Kazi za Kitume. RealAudioMP3

Askofu mkuu Josè Rodriguez Carballo, Katibu mkuu wa Baraza la Kipapa la Mashirika ya Kitawa na Kazi za Kitume akichangia mada kwenye Kongamano hili anabainisha kwamba, hali ya miito kwa Mashirika mengi ya kitawa na kazi za kitume ni tete!

Mashirika haya yanahamasishwa zaidi na zaidi kujikita katika malezi msingi na endelevu kwa ajili ya watawa ili kuweza kuimarisha hali ya miito inayoendelea kulega lega siku hadi siku na hivyo kusababisha watawa wengi kutoona tena thamani ya maisha na wito wao wa kitawa na hivyo kuamua kuachia ngazi! Inasikitisha kuona kwamba, hata wale ambao wameishi kwa miaka mingi katika utawa wanaanza kukata tamaa na kuondoka.

Idadi kubwa ya watawa wa kiume na kike wanaoacha utawa ni dalili za mtikisiko wa maisha ya kitawa ndani ya Kanisa. Haya ni matokeo ya myumbo wa tunu msingi za maisha ya ndoa na familia; imani, maadili na utu wema. Haya ni matokeo ya utandawazi yanayojionesha hata ndani ya Kanisa, kwa sababu watawa ni watu waliochaguliwa kutoka katika Jamii kwa ajili ya mambo ya Kimungu, lakini bado wanaendelea kubakia na ubinadamu wao uliojeruhiwa kwa dhambi ya asili. Kimsingi anasema Askofu mkuu Carballo hizi ni athari za myumbo wa: uchumi, kijamii, kitamaduni na kimaadili.

Anasema, si rahisi kutambua kwa haraka haraka idadi ya watawa wanaoachia ngazi ya wito na maisha ya kitawa, kwani kuna Mabaraza mawili ya Kipapa yanayoshughulikia kesi za namna hii. Kwa watawa, kesi hii inashughulikiwa na Baraza la Kipapa la Mashirika ya Kitawa na Kazi za Kitume na kwa upande wa Watawa Makleri, kesi zao zinashughulikiwa na Baraza la Kipapa kwa ajili ya Makleri na kesi zenye utata wa imani na maadili zinashughulikiwa na Baraza la Kipapa la Mafundisho Tanzu ya Kanisa.

Katika kipindi cha Miaka mitano iliyopita, yaani kuanzia Mwaka 2008 hadi mwaka 2012, Baraza la Kipapa la Mashirika ya Kitawa na Kazi za Kitume, limetoa ruhusa kwa watawa 11, 805 kuacha rasmi wito na maisha ya kitawa. Huu ni wastani wa watawa 2, 361 wanaoacha maisha ya kitawa kwa Mwaka.

Baraza la Kipapa kwa ajili ya Makleri katika kipindi cha Miaka mitano iliyopita, limetoa kibali cha kuwasimamisha Mapadre 1, 188 na Mashemasi 130. Kwa pamoja idadi hii ya Watawa na Mapadre walioacha ni 13, 123. Hali hii inatisha na kusikitisha sana. Wote hawa ni wastani wa Watawa na Mapadre 3,000 wanaoacha wito na maisha yao kitawa na kipadre kwa mwaka. Pengine kuna mambo mengi ambayo yamefichika chini ya idadi hii na kwamba, kuna haja kwa Kanisa kuliangalia tatizo hili kwa jicho la pekee ili kuweza kuimarisha miito ya kitawa na kipadre kwa ajili ya maisha na utume wa Kanisa kwa sasa na kwa siku za usoni.

Askofu mkuu Carballo anasema kuna baadhi ya mambo yanayochangia kasi kubwa ya watawa na mapadre kuacha wito na maisha yao. Jambo kubwa na sababu msingi ni ukavu wa maisha ya kiroho. Watawa na Mapadre wanajikuta hawana tena hamu yak usali, kutafakari wala kushiriki Sakramenti za Kanisa zinazowakirimia neema na baraka katika maisha na wito wao.

Sala za binafsi na zile za Kijumuiya hazina nafasi tane, pengine kwa kisingizio cha kuelemewa mno na kazi za kitume! Hizi ni dalili za kumong’onyoka kwa tunu msingi za maisha ya kiroho na kiimani na matokeo yake kuitema zawadi ya utawa na upadre, waliyoipokea kwa shangwe na nderemo wakati walipokuwa wanaweka nadhiri au kupadrishwa.

Katika hija ya maisha ya kitawa na kipadre, baadhi yao hupoteza utambulisho wao kwa Jumuiya, Shirika na hata wakati mwingine kwa Kanisa lenyewe. Dalili zake ni watu kutoridhika na maisha ya Kijumuiya, kinzani, migogoro na hali ya kudhaniana vibaya. Ubaguzi na upendeleo unaofanywa na baadhi ya viongozi wa Mashirika na Jumuiya za Kitawa, ni mambo yanayochangia kuwafanya baadhi ya watawa na mapadre kutoshiriki kikamilifu katika maisha ya Kijumuiya kwa kutindikiwa uwiano makini kati ya maisha ya mtu binafsi na yale ya Kijumuiya au Kishirika. Matokeo yake, watu hawa watatafuta fursa hizi nje ya Jumuiya na Mashirika yao, mwanzo wa kuchanganyikiwa na kuanza pole pole kupoteza dira na mwelekeo wa maisha ya kitawa na kipadre.

Kumbu kumbu zinaonesha kwamba, uhusiano kati ya mtawa na mtawa, au kati ya mtawa na viongozi wake ni chanzo cha watawa na mapadre wengi kuachia ngazi. Hii ni kutokana na hali ya kutoelewana, ukosefu wa majadiliano ya kina yanayosimikwa katika msingi wa ukweli na uwazi; upendo na huruma. Majadiliano ya kina yanapogeuka kuwa ni majanga ya Kijumuiya, hapo kuna hatari ya watawa kuacha utawa.

Baadhi ya watawa na mapadre hawakubaliani kimsingi na Mafundisho tanzu ya Kanisa, hali inayoonesha mpasuko wa kiimani na kimaadili katika utekelezaji wa wito na maisha ya kitawa na kipadre. Wengine wanashindwa kutatua kinzani hizi kwa njia halali na matokeo yake wanakosa mwelekeo. Baadhi ya mafundisho ambayo yanasadikiwa kuwa ni chanzo cha kinzani na migogoro ya kitawa na kipadre ni suala la useja na hata wakati mwingine, kumongo’onyoka kwa maadili katika fadhila hizi na hivyo kuwafanya baadhi ya watawa na mapadre kuwa na mwelekeo potofu hata wakati mwingine kusababisha kashfa.

Hawa ni watu ambao mioyo yao imegawanyika na mara wanapoacha wanaona hakuna kitu cha thamani ambacho wamekipoteza, kwani: utawa au upadre ilikuwa ni sawa na Hoteli au nyumba ya mapumziko

Askofu mkuu Carballo anasema, pengina kuna haja ya kuangalia kwa makini historia, maisha na mahali wanapotoka vijana wanaoomba kujiunga na maisha ya kitawa na kipadre. Jumuiya zinazowapokea na kuwaanzishia mchakato wa malezi na majiundo yao msingi zinapaswa kuwa makini kwa kusoma alama za nyakati kwani sasa mambo mengi yamebadilika kutokana na athari za utandawazi na maendeleo ya sayansi na teknolojia. Kuna mabadilio ya vipaumbele katika maisha; kuna vielelezo vipya vya maisha na tunu msingi; mambo ambayo yanasambazwa kwa kasi ya ajabu na hata pengine kusababisha mmong’onyoko wa tunu msingi za kimaadili.

Mwingiliano wa tamaduni na kinzani hizi unawachanganya watu kiasi cha kushindwa wakati mwingine kutambua mambo msingi katika maisha na wito wa kitawa na kipadre! Thamani na utu wa mtu unapimwa kwa mchango wake katika Jumuiya! Wanathaminiwa wale wanaochangia kwa kiasi kikubwa na wengine wanaambulia patupu! Watu wanaelemewa na utamaduni wa mpito, hawataki kufungwa na maisha ya kitawa na kipadre, wanataka kwenda nje, kula kuku kwa mrija! Lakini wanapofika huko, baada ya muda si mrefu wanatambua kwamba, wamejichumia “majanga” ya maisha!

Ubinafsi unatawala zaidi kuliko maisha ya Kijumuiya na kwamba, watu wanataka uhuru usiokuwa na mipaka, kinyume cha Mashauri ya Kiinjili. Njia za mawasiliano ya jamii na mawasiliano kwa ujumla yameboreshwa, lakini bado watu wengi wanashindwa kukutana na jirani zao, wanabaki wamejifungia katika ubinafsi wao!

Askofu mkuu Carballo anasema, licha ya hali hii inayoonesha mtikisiko wa maisha na wito wa kitawa na kipadre, lakini bado kuna idadi kubwa ya watawa na mapadre wanaoishi na kufurahia wito wao kwa ajili ya Mungu na jirani katika sekta mbali mbali za maisha: katika katekesi, elimu, afya na maendeleo endelevu yanayomgusa mtu mzima: Ni watu wanaorutubisha maisha yao ya kiroho kwa Ibada, Sakramenti, Neno la Mungu na matendo ya huruma. Hawa ndio wale wanaomtafuta na kutaka kuishi karibu na Mwenyezi Mungu, wakimpatia kipaumbele cha kwanza katika maisha na utume wao, tayari kuwa ni kielelezo cha ushuhuda wa kinabii ambao wakati mwingine unasigana na malimwengu.

Kanisa linahitaji watawa na mapadre wema na watakatifu; bila kusahau kwamba, hata katika kundi hili bado wadhambi wataendelea kuwamo, jambo la msingi ni kujitambua na kuanza hija ya toba na wongofu wa ndani, inawezekana kufurahia wito na maisha kitawa na kipadre, kila mtu akitekeleza wajibu na dhamana yake barabara!

Kanisa liendelee kuwekeza katika majiundo msingi na endelevu, daima likijitahidi kusoma alama za nyakati. Watawa na Mapadre katika miaka yao ya kwanza kwanza, wasaidiwe kikamilifu kuwa na dira na mwongozo wa maisha, wasije wakamezwa na malimwengu.

Imehaririwa na Padre Richard A. Mjigwa, C.PP.S.
Idhaa ya Kiswahili ya Radio Vatican.








All the contents on this site are copyrighted ©.