2014-01-29 11:24:25

Wadau wa mawasiliano ya kijamii wanapaswa kutekeleza wajibu wao kwa kuwajibika!


Mabingwa na wadau katika sekta ya mawasiliano ya Jamii baada ya warsha ya siku moja iliyofanyika mjini Roma, wamekubaliana kimsingi na changamoto iliyotolewa na Baba Mtakatifu Francisko kwamba, kuna haja ya kujenga mawasiliano katika msingi wa maadili na uwajibikaji, kwa kutambua kwamba, mawasiliano yanapaswa kuwa ni kwa ajili ya huduma na ujenzi wa utamaduni wa watu kukutana.

Askofu mkuu Claudio Maria Celli, Rais wa Baraza la Kipapa la Mawasiliano ya Jamii katika mkutano huu, amewasilisha muhtasari wa ujumbe wa Baba Mtakatifu Francisko kwa ajili ya Siku ya Upashanaji Habari Ulimwenguni, itakayoadhimishwa na Mama Kanisa hapo tarehe Mosi, Juni, 2014 sanjari na Siku kuu ya Kupaa Bwana Mbinguni. Neno msingi ni ujenzi wa umoja, mshikamano na udugu.

Warsha hii iliandaliwa na Mfuko wa Uinjilishaji kwa njia ya vyombo vya mawasiliano ya kijamii, kwa kuongoza na kauli mbiu "mawasiliano yajayo yanasimikwa katika uwajibikaji". Askofu mkuu Celli anasema, tatizo kubwa linaloikabili sekta ya mawasiliano ya jamii si teknolojia bali ni mtu anayepaswa kupewa kipaumbele cha kwanza ili kujenga na kudumisha mahusiano kati ya watu. Hii ni changamoto inayoligusa Kanisa katika maisha na utume wake sehemu mbali mbali za dunia kwa kujikita zaidi katika ushuhuda wa imani tendaji.

Mabingwa na wadau hawa wanasema watu wamechoka kusikia mafuriko ya maneno, wataka sasa kushuhudia imani katika matendo! Maadili ni jambo la msingi linalopaswa kupewa kipaumbele katika sekta ya mawasiliano ya Jamii! Wafanyakazi katika sekta ya mawasiliano wanapaswa kuwa waaminifu kwa kazi yao, kwa kuzingatia utu na heshima ya binadamu.

Baba Mtakatifu Francisko anaendelea kupeta katika mchakato wa mawasiliano ya kijamii kiasi cha kumpiku hata Rais Barack Obama wa Marekani. Watu wanavutwa zaidi na Papa Francisko kwa maneno yake yanayogusa sakafu ya mioyo ya wengi, vitendo vyake vinaonesha kujali na kuthamini maskini na wote wanaosukumizwa pembezoni mwa Jamii.

Wadau wa habari wajenge na kuzingatia maadili kwani vyombo vya mawasiliano ya Jamii kwani vina umati mkubwa wa watu wanaotumia mitandao ya kijamii kwa shughuli mbali mbali. Wawe makini kutunza na kudumisha tunu msingi za maisha ya kijamii na kiutu.







All the contents on this site are copyrighted ©.