Walimu wa Sekondari Tanzania kuanza kufundisha kwa kutumia "tabuleti"
Serikali ya Jamhuri ya Muungano ya Tanzania inakusudia kutoa maelfu kwa maelfu ya
tabuleti za kufundishia masomo mbali mbali kwa wanafunzi na walimu wa shule za sekondari
nchini kama njia ya ubunifu zaidi, ya kisayansi na ya uhakika ya kukabiliana na changamoto
zinazoikabili sekta ya elimu kwa kutumia Teknolojia ya Habari na Mawasiliano (ICT).
Ili kufanikisha mpango huo, Serikali inakusudia kuingia ushirikiano (partnership)
na taasisi isiyokuwa ya kiserikali ya Opportunity Education Trust ya Marekani ambayo
leo, Jumatatu, Januari 27, 2014, inazindua mpango wa majaribio wa utoaji wa tabuleti
hizo kwa wanafunzi na walimu wao wa shule za sekondari nchini.
Mpango wa Serikali
wa kusambaza tabuleti kwa wanafunzi na walimu wa shule za sekondari ulitangazwa Jumapili,
Januari 26, 2013 na Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mheshimiwa Jakaya Mrisho
Kikwete wakati alipokutana na kuzungumza na Bwana Joe Ricketts, mwenye taasisi ya
Opportunity Education Trust na mmoja wa matajiri wa Marekani.
Katika mazungumzo
hayo yaliyofanyika Ikulu, Dar es Salaam, Rais Kikwete amemweleza kwa undani Bwana
Ricketts hatua ambazo zimechukuliwa na Serikali yake kupania na kuboresha elimu tokea
mwaka 2006, hatua ambazo zimechangia kupanua kwa kasi na kwa kiwango kikubwa wigo
wa utoaji elimu nchini na changamoto ambazo zimezuka kutokana na upanuzi huo mkubwa.
Rais
Kikwete amesema baadhi ya changamoto hizi ni ukosefu wa walimu, na hasa walimu wa
masomo ya sayansi, na ukosefu wa vitabu vya kufundishia changamoto mbili kubwa ambazo
zinatatuliwa na matumizi ya tabuleti. “Mbali na upanuzi mkubwa wa nafasi za wanafunzi
kupata elimu ya ngazi mbali mbali, pia tumepanua sana ufundishaji wa walimu. Mwaka
2005, vyuo vyetu vyote vilikuwa vinatoa walimu 500 sasa tunatoa walimu 12,000 kwa
mwaka. Hivyo, tunaamini kuwa katika mwaka mmoja ama miwili ijayo, tutakuwa tumemaliza
tatizo la walimu wa masomo ya sanaa,” Rais Kikwete alimwambia Ricketts na kuongeza:
“Lakini
bado tunakabiliwa na upungufu mkubwa wa walimu wa sayansi, kama zilivyo nchi nyingine.
Tuna upungufu wa walimu 26,000 na kwa mwaka vyuo vyetu vyote vinahitimisha walimu
2,100 tu. Hii ina maana kuwa itabidi kusubiri miaka 13 kuweza kumaliza tatizo hili
kwa mahitaji ya sasa. Hili haliwezekani na hii ndiyo maana halisi ya kutumia sayansi
na teknolojia ya namna hii kufundishia wanafunzi wetu.”
Rais Kikwete alisema
kuwa matumizi ya teknolojia kufundishia nchini ni jambo linalowezekana kwa urahisi
kwa sababu mtandao wa mawasiliano wa National Fibre Network ambao karibu umefikia
kila wilaya sasa. Rais Kikwete alimshukuru Bwana Ricketts na taasisi yake kwa kukubali
kuchangia maendeleo ya sekta ya elimu nchini kwa kusambaza teknolojia ya kisasa kama
moja ya njia za ubunifu zaidi za kufundishia hasa masomo ya sayansi.
Chini
ya mpango huo wa majaribio wa kusambaza teknolojia hiyo ya kisasa, taasisi ya Opportunity
Education Trust inatoa tabuleti 1100 kwa ajili ya walimu na wanafunzi wa sekondari
katika shule 33.
Bwana Ricketts ambaye ni mwenyeji wa Omaha, Nebraska alimwambia
Rais Kikwete: “Hapa tunafanya majaribio na Tanzania ni nchi ya kwanza duniani miongoni
mwa nchi ambazo tunaunga mkono mipango ya maendeleo kunufaika na mpango huo wa majaribio.
Ni azma yetu kuwa baada ya kuwa tumefanya tathmini ya mafanikio na changamoto za hatua
hii ya majaribio, tutaupanua mpango huu kushirikisha shule nyingi zaidi kwa kushirikiana
na Serikali kwenye mpango wake mkubwa wa kusambaza teknolojia hii katika shule zote
za sekondari hapa Tanzania.”
Bwana Ricketts na wataalam wake pamoja na maofisa
wa Serikali wameanza kutekeleza mpango huo Jumatatu, Januari 27, 2014, kwa kutoa tabuleti
kwa wanafunzi wa Shule ya Sekondari ya Wama Nakayama iliyoko Mkoa wa Pwani. Baadaye
shughuli hiyo itahamia Zanzibar na Pemba, kabla ya Bwana Ricketts na wataalam wake
kutoa tabuleti kwa shule zilizoko mikoa ya Arusha, Dar es Salaam, Dodoma, Mwanza,
Kagera na Morogoro.
Shule zinazonufaika katika mpango huo ni za Serikali na
binafsi na kwa kuanzia masomo ambayo yanapatikana katika tabuleti hizo ni hesabu,
jiografia, historia na kiingereza.