2014-01-28 08:33:33

Upembuzi yakinifu wa Mapapa katika matumizi ya vyombo vya upashanaji habari!


Maendeleo ya sayansi na teknolojia ya njia za mawasiliano ya jamii yamewawezesha viongozi wa Kanisa kuufikia umati mkubwa watu sehemu mbali mbali za dunia. Matumizi ya vyombo vya upashanaji habari imekuwa ni changamoto kwa Mama Kanisa katika Uinjilishaji mpya katika mapambazuko ya millenia ya tatu. Ni changamoto iliyovaliwa njuga kwa namna ya pekee kabisa na Mwenyeheri Yohane Paulo wa Pili, ikaendelezwa na Baba Mtakatifu mstaafu Benedikto XVI na kwa sasa Papa Francisko anaonekana kushika usukani katika njia ya za mawasiliano ya jamii ndani na nje ya Vatican.

Ni tafakari iliyotolewa na Padre Federico Lombardi, msemaji mkuu wa Vatican na mkurugenzi wa Radio Vatican, Jumatatu tarehe 27 Januari 2014, wakati wa maadhimisho ya kumbu kumbu ya miaka 20 tangu ilipozinduliwa Radio Maria Toledo na Kituo cha Televisheni cha Jimbo vilipoanzishwa. Katika maadhimisho haya Padre Federico Lombardi amepewa tuzo ya heshima kwa kutambua mchango wake mkubwa katika maisha na utume wa Kanisa la Kiulimwengu katika masuala ya vyombo vya upashanaji habari.

Padre Lombardi anasema kwamba, changamoto ya matumizi makini ya vyombo vya habari iliyotolewa na Mwenyeheri Yohane Paulo II ilifanyiwa kazi na majimbo mbali mbali dunia kwa kuanzisha vituo vya Radio na Televisheni. Padre Lombardi anakumbuka baadhi ya matukio ambayo watu walitamani kumwona Baba Mtakatifu akishiriki katika mateso na mahangaiko ya watu!

Baada ya shambulio la kigaidi lililofanyika tarehe 11 Septemba huko Marekani, liliwashtua watu wengi wakajiona wanyonge sana mbele ya macho ya magaidi. Katika hali kama hii, watu wengi walitamani kumwona na kumsikia Mwenyeheri Yohane Paulo wa Pili akiwapa neno la faraja. Kituo cha Televisheni cha Vatican kikamwonesha Papa akisali kwa ajili ya waathirika wa shambulio la kigaidi.

Watu wengi bado wanakumbuka ile hija ya upatanisho na msamaha iliyofanywa na Baba Mtakatifu Yohane Paulo II kwenye gereza ili kumtembelea na kuzungumza na Ali Agca, aliyemshambulia kwa risasi kwenye Uwanja wa Kanisa kuu la Mtakatifu Petro mjini Vatican. Huu ulikuwa ni ushuhuda wa Injili ya Huruma ya Mungu iliyomwilishwa katika matendo adili. Ni kwa njia ya Televisheni hadi leo hii, ile picha ya Mwenyeheri Yohane Paulo II bado iko mioyoni mwa watu!

Padre Lombardi anasema, Baba Mtakatifu Yohane Paulo II alikuwa ni mtu aliyefahamu kutumia vyema vyombo vya mawasiliano ya kijamii, kwa njia ya maneno na vitendo vyake. Kwa njia ya televisheni watu wengi walishuhudia hija za kichungaji zilizofanywa na Papa Yohane Paulo II sehemu mbali mbali za dunia. Wengi bado wanakumbuka siku ile Mwenyeheri Yohane Paulo wa Pili aliposali na kutumbukiza ujumbe wake kwenye ukuta wa Yerusalem, kama sehemu ya Maadhimisho ya Jubilee kuu ya Miaka 2000 ya Ukristo. Papa Yohane Paulo II alikwenda Yerusalem kuomba msamaha kwa dhambi zilizotendwa na Watoto wa Kanisa.

Padre Lombardi anasema miaka 25 ya Utume na Maisha ya Baba Mtakatifu Yohane Paulo wa Pili, yameacha kumbu kumbu za kudumu katika akili na miyo ya watu. Hii ni kazi kubwa iliyofanywa na vyombo vya mawasiliano ya Jamii. Hata katika unyonge na magonjwa yake, Kituo cha Televisheni cha Vatican kilimwonesha Papa Yohane Paulo wa II kwa heshima na taadhima; watu wakaonja na kushiriki Njia ya Msalaba hadi pale alipokata roho na kujikabidhisha mikononi mwa Mwenyezi Mungu, mwingi wa huruma na mapendo.

Papa Yohane Paulo II alipenda daima kufanya tafakari ya hija zake za kichungaji na wasaidizi wake wa karibu ili kusikia mwangwi wa ujumbe wake na kuona ikiwa kama kweli ujumbe aliokusudia kuutoa umewafikia wengi. Kwa maneno machache, Papa Yohane Paulo II alikuwa ni rafiki wa vyombo vya habari.

Padre Federico Lombardi ambaye kwa miaka saba ya maisha na utume wa Baba Mtakatifu mstaafu Benedikto XVI alikuwa naye bega kwa bega anasema, Papa aliendeleza uhusiano wake na vyombo vya habari, lakini kwa bahati mbaya, uhusiano huu ulikuwa tenge. Mara kwa mara waandishi wa habari walimtupia "madongo" Baba Mtakatifu mstaafu Benedikto wa kumi na sita. Alijitahidi kujenga uhusiano wa karibu na vyombo vya habari kadiri alivyoweza. Majibu kwa maswali yaliyoulizwa na waandishi wa habari ni yale ambayo yalibubujika kutokana na tafakari na maandalizi ya kina na hitimisho kwa ajili ya wasikilizaji wake.

Baba Mtakatifu mstaafu Benedikto alianzisha mtindo wa kuzungumza na waandishi wa habari wakati wa hija zake za kichungaji, ili kujadili kuhusu lengo na kiini cha hija zake za kichungaji. Wakati mwingine majibu yake yaliyosheheni msimamo wa Kanisa kuhusu maadili na utu wema yalizua kinzani na matusi kutoka kwa baadhi ya wanaharakati waliotumia vyombo vya habari ili kumshambulia Papa mstaafu Benedikto XVI. Ni kurasa chungu, lakini zilipita kwa amani na utulivu.

Baba Mtakatifu mstaafu Benedikto XVI atakumbukwa sana na Mama Kanisa kwa kuliachia Kanisa urithi wa tafakari ya kina kuhusu maisha ya Yesu wa Nazareti, akionesha umahiri wake katika tafakari ya Neno la Mungu, Taalimumungu, Tasaufi, Katekesi na Mafundisho ya Kanisa. Watu bado wanakumbuka maneno na unabii wa Papa Mstaafu Benedikto wa kumi na sita katika mahojiano na Peter Seewald kuhusu: Mwanga wa Ulimwengu".

Alijitahidi kujibu maswali hata yale yaliyokera katika maisha na utume wake kama Khalifa wa Mtakatifu Petro, lakini bado aliendelea kuwa ni kiongozi mwenye imani na matumaini. Hata hivi karibuni waandishi wa habari "walimtwanga" swali Papa Francisko kuhusu "mashoga". Kumbe, si rahisi kuweza kuwaridhisha waandishi wa Habari, kwani kila chombo kina mtazamo na malengo yake.

Kimsingi Baba Mtakatifu mstaafu Benedikto XVI ameacha urithi mkubwa kwa Kanisa katika maisha ya kiroho, Tafakari ya Neno la Mungu, Katekesi, kwa kuzingatia ukweli na uwazi. Kuna mambo ambayo alikuwa anaandika kwa mkono wake mwenyewe anasema Padre Lombardi. Katekesi zake alizokuwa anatoa kila Jumatano zimekuwa ni msingi mkubwa wa Katekesi endelevu katika maisha na utume wa Kanisa.

Makleri wa Jimbo kuu la Roma wanakumbuka ile Katekesi ya kina kuhusu Maadhimisho ya Mtaguso mkuu wa Pili wa Vatican aliyoitoa kwa muda wa masaa matatu yote akiyachambua kutoka katika hazina ya moyo wake! Matendo makuu ya Mungu! Siki tatu baadaye, akatangaza kung'atuka kutoka madarakani kwa ajili ya ustawi na maendeleo ya Kanisa la Kristo! Ulimwengu ukapigwa na butwaa! Kwa hakika Papa Mstaafu Benedikto XVI hakubahatika kuwa na umati mkubwa wa watu waliomfuata na kumsikiliza, kama ilivyo kwa Papa Francisko, lakini waliobahatika kumsikiliza walibaki wakiwa wameshika tama!

Padre Federico Lombardi anasema, Papa Francisko anaonekana kuwa na mvuto pamoja na mashiko kwa vyombo vya habari hata vile ambavyo vilikuwa vinafuatilia maisha na utume wa Kanisa kwa "makengeza" sasa wanaanza kubadili mwelekeo. Ni Kiongozi mwenye mvuto kwa watu wengi; mnyenyekevu, mkweli na muwazi. Ni kiongozi anayeguswa na mahangaiko ya watu na kuyafanyia kazi.

Ni kiongozi anayeendelea kuwashangaza wengi kwa kuvunja kuta za utengano, ili kujenga utamaduni wa kukutana na kushirikishana imani, matumaini na mapendo. Ni kiongozi mwenye karama kubwa ya mawasiliano. Si mtaalam sana wa lugha, lakini kile kidogo alichojaliwa na Mwenyezi Mungu anakitumia kikamilifu! Papa Francisko ambaye hazungumzi Kiingereza hivi karibuni alichaguliwa na TIME MAGAZINE kuwa ni mtu mashuhuri kwa Mwaka 2013.

Padre Lombardi anasema, Papa Francisko pengine anaweza kuongoza kwa kupigwa picha na watu mbali mbali katika kipindi hiki kifupi cha maisha na utume wake. Ni picha zinazoonesha uwepo wa karibu kwa wagonjwa, maskini na wote wanaosukumizwa pembezoni mwa Jamii; wote hawa anapenda kuwaonjesha: upendo na huruma ya Mungu. Radio Vatican inatasiri ujumbe wa picha hizi katika lugha 40 zinatumika katika matangazo yake kila siku!

Papa Francisko analichangamotisha Kanisa kupembua mbinu mkakati wa mawasiliano katika maisha na utume wake, kwa kuhakikisha kwamba, linatumia vyombo vya mawasiliano ya Jamii kwa ajili ya kutangaza Injili ya Furaha sanjari sanjari na utekelezaji wa mikakati ya kichungaji. Watu wanatamani kuona kwamba, vyombo vya habari vinawasaidia kumwona, kumsikia na kumfuasa. Hapa kunaonekana uhusiano wa dhati kati ya utume wa Baba Mtakatifu Francisko na dhamana ya vyombo vya habari.

Ni matumaini ya Padre Federico Lombardi, msemaji mkuu wa Vatican kwamba, vyombo vya habari kitaifa na kimataifa vitamsaidia Baba Mtakatifu Francisko kuwahudumia watu wa mataifa, ili kuwaonjesha: huruma na upendo wa Mungu; ili kusimamia haki na amani; ili kulinda na kutetea utu na heshima ya binadamu. Waandishi wa habari watambue dhamana na wajibu wao katika Jamii, daima watafute mafao ya wengi!

habari hii imehaririwa na
Padre Richard A. Mjigwa,
Idhaa ya Kiswahili ya Radio Vatican.







All the contents on this site are copyrighted ©.